Social Icons

Pages

Tuesday, December 08, 2015

WAILALAMIKIA DAWASCO KUKOSA MAJI MIEZI MITATU


Wananchi  na wamiliki wa viwanda katika eneo la Salasala Kinondoni, jijini Dar es Salaam, wamelilalamikia Shirika la Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (Dawasco), kwa kushindwa kuwapa huduma ya maji kwa takribani miezi mitatu sasa.
Wakizungumza na Nipashe kwa nyakati tofauti  jana, wananchi hao walisema awali  Dawasco  lilikuwa likiwapatia huduma hiyo kwa wiki mara mbili, lakini kwa sasa limekatisha huduma hiyo bila taarifa yoyote kwa wananchi kwa miezi mitatu.
Meneja Masoko wa kiwanda cha sabuni cha Family, Watambura Chishagimbi, alisema kukosekana kwa huduma hiyo katika kipindi hicho kimewaongezea gharama za uzalishaji kutokana na kununua kiasi kikubwa cha maji kwa gharama kubwa, huku dumu moja la ujazo wa lita 20 wakilazimika kununua  kwa Sh. 500.
Badhi ya maeneo yaliyoathirika na tatizo hilo ni makazi ya watu, kiwanda cha kuzalisha biskuti, kuku, shule ya msingi Green Acres, G&B Soap Industries Ltd,  pamoja na wafanyabiashara wadogo wanaozunguka eneo hilo kwa ujumla.
“Kwa muda wa miezi mitatu sasa tunaweza kupata maji siku moja kwa wiki au tusipate kabisa, hivyo tunalazimika kununua maji kwa wachuuzi wa magari ambapo lita 1,000 tunanunua kwa Sh. 15,000, hali hiyo inatuweka katika wakati mgumu wa uzalishaji bidhaa,” alisema Chishagimbi.
Naye mkazi wa eneo hilo, Bakari Kitomari, alisema kukosekana kwa huduma hiyo kumewaongezea makali ya maisha na kuiomba Dawasco kunususru hali hiyo na kuishauri iwarudishe katika utaratibu wa awali kwa wiki mara tatu.
Akizungumzia suala hilo, Msemaji wa Dawasco, Evalasting Lyaro, alisema eneo lililokumbwa na adha hiyo ni linalozunguka eneo la kampuni ya IPTL, ambapo wananchi wamekosa huduma hiyo kutokana na  bomba kubwa la Ruvu  kukaliwa na vifaa vigumu vilivyosababisha kushindwa kusukuma maji.
“Hata hivyo, wananchi hao wategemee kupata huduma hiyo leo (jana), baada ya wataalamu kufunga kijiko eneo la bomba lililosababisha tatizo hivyo hakutakuwa mgawo kama awali,” alisema.
CHANZO: NIPASHE

No comments: