Mbunge wa Jimbo la Kibamba, John Mnyika, ameomba
ripoti za kamati za uchunguzi zilizoundwa na mawaziri wa Wizara ya
Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe na Samuel Sitta, kuhusu Mamlaka ya
Bandari Tanzania (TPA) ziwekwe hadharani.
Amesema kuwekwa hadharani kwa ripoti hizo kutaondoa usiri na
kusaidia kubaini ufisadi uliokithiri katika mamlaka hiyo ili hatua za
kuwasimamisha vigogo wa TPA na wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ziwe
na mafanikio.
Mnyika ambaye amekua kimya kwa muda mrefu tangu kumalizika kwa
uchaguzi mkuu Oktoba 25, mwaka huu, alisema hayo wakati akizungumza na
waandishi wa habari, jijini la Dar es Salaam jana.
“Kama kweli serikali ya awamu ya tano ina lengo la kufichua
mafisadi, inapaswa kuweka wazi ripoti mbalimbali za uchunguzi ili ziwe
dira ya kujua kiini cha matatizo kujitokeza katika mamlaka hiyo,”
alisema na kuongeza:
“Nafahamu yapo mambo mazuri kwa nchi yaliyonainishwa, lakini
kutokana na ripoti hizo kuwa siri hakuna anayejua huku fedha za walipa
kodi zikiwa zimetumika bila mafanikio. Dawa ya jipu siyo kulitumbua bali
ni kulipasua ili kiini cha ndani kitoke, ukikiacha jipu linaanza
kuvimba upya tena linakuwa hatari zaidi.”
Aidha, Mnyika alisema wakati wa kampeni, Rais Dk. John Magufuli,
aliahidi kutatua tatizo la maji na kumtaka kutekeleza ahadi hiyo kwa
kutembelea mradi wa maji wa Ruvu Juu ili apasuwe majipu yaliyoiva.
Alisema iwapo Rais atatembelea mtambo huo atabaini ufisadi
unaokwamisha ulazaji wa mabomba ya Mchina yasitoe maji, pampu za maji
kuharibika mara kwa mara na mradi wa maji kutoka Mlandizi hadi Kimara
kukwama wakati fedha zimetolewa.
“Wizara ya maji ilisema bungeni kuwa ulazaji wa mabomba ya maji
ulifikia asilimia 70 na ifikapo Agosti, mwaka huu mabomba yangetoa maji
lakini bado wananchi wanaendelea kuteseka,” alisema.
Mnyika alisema serikali ya awamu ya tano ikishindwa kutoa ufumbuzi
wa hoja hizo mbili, ataziwakilisha bungeni katika kikao cha Bunge
kinachotarajia kufanyika Januari mwakani.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment