Social Icons

Pages

Tuesday, December 08, 2015

JAJI ATUPA PINGAMIZI LA WAKILI MWALE NA WENZAKE

Jaji Gadi Mjemas anayesikiliza kesi inayomkabili wakili maarufu jijini Arusha, Medium Mwale na wenzake watatu, ametupilia mbali pingamizi lililowekwa na upande wa utetezi kupinga kupokelewa maelezo ya  mshitakiwa, Elias Ndejembi, kwa madai wakati akiyatoa hayakurekodiwa na pia muda alioitwa polisi na aliomaliza kutoa maelezo hayo haukutajwa.
Pia upande huo wa utetezi unadai wakati mshtakiwa huyo akitoa maelezo hayo, mke wake ambaye alikuwa shahidi wake alitolewa nje. Akitoa uamuzi wa pingamizi hilo, Jaji Mjemas alihoji endapo mke wa mshitakiwa Ndejembi alitolewa nje, alikubalije kuandika maelezo yake  wakati akijua ndiye shahidi wake.
Jaji huyo pia alisema hakuna kifungu chochote cha sheria kinamtaka ofisa wa polisi kurekodi muda wa mtuhumiwa kuanza kutoa maelezo ya onyo na anapomaliza na kwamba hana mashaka kuwa haki za mshitakiwa zilizingatiwa kwani sheria inataka ahojiwe si zaidi ya saa nne na inaonyesha ilizingatiwa.
“Natupilia mbali hoja ya kwanini mtuhumiwa wakati anarekodiwa maelezo yake mkewe alitoka nje wakati katika maelezo ya Mdemu inaonyesha kabla ya kumhoji alimkumbusha kosa analoshtakiwa nalo pamoja na jina lake na mahali anapokaa, kwa hiyo hakuna ukiukwaji uliofanywa wakati wakuchukuliwa maelezo yake," alisema.
Awali, Mrakibu wa Msaidizi wa Polisi, Fadhili Mdemu, wakati akitoa ushahidi wake, kuliibuka malumbano ya kisheria baada ya Mdemu kudai aliandika maelezo ya mshtakiwa wa nne, Ndejembi na mshtakiwa wa pili Don Bosco Gichana ambaye ni raia wa Kenya.
Baada ya shahidi huyo kueleza hayo, wakili wa utetezi, Albert Msando, alikataa kupokelewa kwa maelezo ya Ndejembi kwa kile alichodai  yanaonyesha alihojiwa saa 9:18 alasiri, lakini hayaonyeshi alikamatwa na kushikiliwa na polisi kuanzia muda gani.
Msando alidai maelezo hayo yana mapungufu kisheria kwani hayajaambatanishwa na fomu ya uthibitisho kuonyesha mshtakiwa aliyasoma na kuridhia kuwa ni yake.
“Inaonyesha mshtakiwa alipigiwa simu saa 2:00 asubuhi lakini haielezi alikuwa chini ya ulinzi wa polisi kuanzia saa ngapi na muda gani ulipita kabla hajahojiwa. Sheria iko wazi mtuhumiwa anapaswa kuhojiwa ndani ya saa nne baada ya kuwa chini ya ulinzi wa polisi,” aliendelea kudai Msando.
 
KESI NDANI YA KESI
Baada ya malumbano hayo ya kama maelezo ya mshtakiwa yakubaliwe kama kielelezo au la, Jaji Mjemas aliamua suala hilo kusikilizwa kwenye kesi ndani ya kesi, ambapo upande wa serikali uliahidi kupeleka mashahidi watatu, huku upande wa utetezi ukiahidi kupeleka wawili.
Mawakili wa utetezi kwa pamoja walipinga kupokelewa kwa maelezo hayo, huku wakitoa hoja mbalimbali za kisheria.
Wakili wa utetezi, Moses Mahuna, alipinga kupokelewa kwa maelezo hayo, akidai yaliandikwa bila kuonyesha kifungu cha sheria kilichokiukwa na mshtakiwa.
Alidai kutoandikwa kwa kifungu cha sheria kilichokiukwa kunamfanya mtuhumiwa ashindwe kuelewa mtiririko mzima wa maelezo ya onyo.
Hata hivyo, kesi hiyo ilishindwa kuelendelea kusikilizwa, kutokana na wazee wa baraza kutokuwapo na imepangwa kuendelea leo. Washtakiwa hao wanne wanakabiliwa na mashtaka 44, ikiwamo ya kula njama kutenda kosa, utakasaji fedha haramu na kughushi.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: