Tambua kuwa lugha ya Kiswahili ni lugha
kamili na wala si lugha chotara kwa maana ya mchanganyiko wa lugha ya
Kiarabu na lugha ya Kibantu kama watu wengi wanavyodhani. Endelea kujifunza juu ya asili na chimbuko la lugha ya Kiswahili.
Wataalamu wa lugha wameandika kuhusu lugha ya Kiswahili kama lugha ya taifa na lugha rasmi inayokadiriwa kutumiwa na watu wapatao zaidi ya milioni 60 duniani kote. Hutumika katika nchi za Afrika Mashariki na Kati kama Tanzania, Kenya, Uganda na katika eneo la mashariki mwa nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC). Vilevile katika nchi za Burundi, Rwanda, Msumbiji, Zambia, Comoro na Malawi. Kiswahili kinazungumzwa pia katika nchi za Uarabuni kama Dubai, Umoja wa Nchi za Falme za Kiarabu (UAE), Yemen, Dubai, n.k.
Wataalamu wa lugha wameandika kuhusu lugha ya Kiswahili kama lugha ya taifa na lugha rasmi inayokadiriwa kutumiwa na watu wapatao zaidi ya milioni 60 duniani kote. Hutumika katika nchi za Afrika Mashariki na Kati kama Tanzania, Kenya, Uganda na katika eneo la mashariki mwa nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC). Vilevile katika nchi za Burundi, Rwanda, Msumbiji, Zambia, Comoro na Malawi. Kiswahili kinazungumzwa pia katika nchi za Uarabuni kama Dubai, Umoja wa Nchi za Falme za Kiarabu (UAE), Yemen, Dubai, n.k.
Kwa kipindi cha miaka zaidi ya miaka elfu moja,
kumekuwa na mawasiliano kwa viwango tofauti katika nchi za Mashariki ya
Kati, Uajemi, India, China, Ureno na Uingereza. Nchi hizi zimechangia
kwa kiwango kikubwa kwa kukopesha maneno mengi ya lugha zao katika lugha
ya Kiswahili. Katika sehemu mbalimbali duniani viko vyuo
vinavyofundisha lugha hii. Pia viko vituo vingi vya utangazaji vya redio
na runinga vinavyotumia Kiswahili.
Ukichunguza muundo wa maneno na miundo wa sentensi
za Kiswahili utagundua kuwa Kiswahili kinafanana sana na lugha za
Kibantu kuliko Kiarabu, Kiajemi na Kihindi. Inasemekana kuwa idadi ya
maneno ya mikopo kutoka lugha za kigeni katika lugha ya Kiswahili
inaweza kulinganishwa na mikopo ya maneno katika lugha kongwe kama
Kilatini, Kigiriki na Kifaransa ambazo zimechangia sana katika kuikuza
lugha ya Kiingereza. Ni dhahiri kuwa ukopaji wa maneno katika lugha
yoyote ile ni dalili ya kukua kwa lugha husika.
Nchini Tanzania na Kenya, lugha ya Kiswahili ni
lugha za rasmi za mataifa haya. Kwa upande wa Kenya, Kiswahili ni somo
la lazima linalofundishwa katika shule za msingi na sekondari. Nchini
Tanzania, Kiswahili ni somo la lazima pia katika shule za sekondari hadi
kidato cha nne na pia ni lugha ya kufundishia katika shule za msingi.
ASILI YA KISWAHILI
Yako maneno mawili ambayo tunayochanganya katika
matumizi nayo ni asili ya lugha ya Kiswahili na chimbuko lake. Neno
asili lina maana ya jinsi jambo lilivyoanza au lilivyotokea. Ama kwa
neno chimbuko, maana yake ni mahali kitu au jambo lilipoanza. Kwa hiyo
asili na chimbuko yanatofautiana katika maana.
Zimewahi kutokea nadharia kadhaa kuhusu asili ya
Kiswahili ambazo nitazieleza hivi punde. Kwanza ipo nadharia kuwa
Kiswahili kimetokana na lugha ya Kiarabu. Pili iko nadharia kuwa
Kiswahili ni mchanganyiko wa Kiarabu na lugha za Kibantu zilizotumika
katika upwa wa Afrika Mashariki. Tatu, ni kuwa Kiswahili ni lugha ya
Kibantu iliyoathiriwa sana na Kiarabu hasa kimsamiati. Nne, Kiswahili
kilitokana na mchanganyiko wa lugha kadhaa za Kibantu zilizokuwa katika
upwa wa Afrika Mashariki.
Nadharia isemayo kuwa Kiswahili kilitokana na
Kiarabu inaegemea sana wingi wa maneno yenye asili ya Kiarabu na pia
dini ya Kiislamu. Inadaiwa kwamba kwa kuwa Kiswahili kilianza pwani na
kwa kuwa idadi kubwa ya wananchi wa pwani ni Waislamu na kwa kuwa
Uislamu uliletwa na Waarabu, basi Kiswahili nacho kinashabihiana na
Kiarabu. Madai haya hayana mashiko kwani Kiswahili ni lugha kamili
iliyokopa maneno kutoka katika lugha za Kiarabu, Kiajemi, Kireno,
Kihindi, Kijerumani na Kiingereza kutokana na mawasiliano ya karne
nyingi kati ya wenyeji wa pwani na wafanyabiashara wa kigeni
Uchunguzi uliofanywa na wataalamu wa Kiswahili
hasa wanaisimu wamegundua kuwa mabadiliko yalihusu msamiati tu na wala
siyo maumbo ya maneno wala miundo ya tungo za Kiswahili. Ikumbukwe pia
kwamba uchunguzi ulikwishafanywa kuwa kwa kipindi kirefu Kiswahili
kilitumia maneno mengi kutoka katika lugha za Kibantu kwa kuwa wasemaji
wengi wa Kiswahili ni Wabantu.
KUENEA KWA KISWAHILI
Jambo la msingi ni kuwa lugha kuwa na maneno mengi ya kukopa
kutoka katika lugha nyingine haifanyi lugha hiyo ionekane imetokana na
hiyo lugha ngeni. Inabidi kuzingatia zaidi msingi wa lugha kwa upande wa
fonolojia, mofolojia, semantiki na sintaksia ya lugha husika. Kimsingi,
vigezo pekee vinavyoweza kutumika ili kuibainisha lugha ni vya kisimu
kama vile fonolojia, mofolojia na sintaksia lakini msamiati siyo msingi
pekee wa kuzingatia. Nadharia ambazo zinazaweza kuwa ni msingi wa
uhakika ni mbili. Moja ni ile isemayo kuwa Kiswahili kina asili ya
Kibantu. Msingi wa pili ni kuwa Kiswahili ni lugha iliyotokana na lugha
kadhaa za Kibantu katika eneo la pwani.
Kiisimu lugha ya Kiswahili ina utaratibu maalumu
ambao ni herufi kama konsonanti na irabu ambapo huweza kuunda silabi
kama ba, ma, ka, la; au konsonanti, konsonanti na irabu kama kwa, gha,
mwa, n.k.; au konsonanti, konsonanti, konsonati na irabu kama, mbwa,
ng’we n.k.
CHIMBUKO LA KISWAHILI
Ni vigumu kusema kwa uhakika mahali ambapo ni
chumbuko la Kiswahili. Pengine tunaweza kusema kuwa Kiswahili kilianzia
sehemu maalumu na kuenea hadi mahali fulani. Inadaiwa kuwa chimbuko la
Kiswahili liko katika maeneo ya Kaskazini Mashariki mwa Kenya lakini
madai haya hayajawahi kuthibitishwa kwa hoja zenye mashiko. Ni wazi kuwa
wanahistoria waliowahi kuandika kuwa mawasiliano na maelewano kati ya
watu wa eneo fulani kwa kiasi fulani kulizuka lugha moja iliyoeleweka
kwa watu wote katika eneo hilo. Mawasiliano ya aina hii yalizua lugha
ambazo zilitofautiana kuanzia kaskazini hadi kusini mwa pwani ya Afrika
Mashariki ambazo zilijulikana kama lahaja za Kiswahili. Kuanzia
Kaskazini kuna lahaja ya Ci Miini ambayo huzungumzwa katika eneo la
Barawa, pwani ya Somalia. Kusini zaidi kulikuwa na lahaja za Kitukuu na
Kibajuni katika eneo la kusini mwa Somalia na Kaskazini mwa Kenya.
Nyingine ni Kisiu sehemu za Pate, Kiamu huko Lamu, Kimvita sehemu za
Mombasa, Kivumba na Kimtang’ata katika sehemu za pwani ya kaskazini mwa
Tanzania, Kimakunduchi, Kihadimu, Kitumbatu sehemu za Unguja na Kipemba
eneo la Pemba. Lahaja hizi zinafanana na lugha nyingine za Kibantu.
Lahaja hizi zinatofautiana kidogo na Kiswahili sanifu kwa sababu
Kiswahili sanifu kina maneno mengi ya mkopo. Lahaja zote hizo ni lugha
zinazojitegemea.
KUENEA KWA KISWAHILI
Kama inavyofahamika, chimbuko la Kiswahili ni upwa
wote wa Afrika Mashariki. Hata hivyo lugha hii haikubaki tu katika eneo
la pwani bali ilienea katika sehemu kubwa ya Afrika Mashariki. Sababu
za kuenea katika sehemu mbalimbali za Afrika Mashariki kulisababishwa na
mambo mengi. Yako mambo yaliyosababisha kuenea kwa Kiswahili kutoka
pwani hadi bara. Mambo hayo ni shughuli za biashara, dini, ukoloni na
hatimaye harakati za kupata uhuru. Tuangalie mchango wa mambo haya manne
katika kukieneza Kiswahili.
Biashara
Kuenezwa kwa dini za kigeni
Katika maelezo yaliyotolewa na wanahistoria ni
kwamba wageni walikuja Pwani ya Afrika Mashariki kwa ajili ya kufanya
biashara. Hata hivyo walikuwapo wenyeji wa pwani waliosafiri kwenda bara
kwa ajili ya kufanya biashara na wageni walipokuja waliwaonyesha njia
walizowahi kuzitumia na hivyo Kiswahili kilienezwa kwa njia hiyo. Kwa
maana hiyo yalikuwapo mawasiliano baina ya wenyeji wa bara na pwani kwa
kipindi kirefu kabla hata ya kuwasili kwa wageni. Wafanya biashara wa
Kiarabu walijikita sana katika biashara ya pembe za ndovu, madini na pia
utumwa. Waafrika waliokuwa wapagazi ndiyo waliokieneza Kiswahili kwa
kuwasiliana na wenzao huko bara.
Wafanyabiashara hawa walifika maeneo ya mbali hadi
Mashariki mwa Kongo na Burundi. Kutokana na umbali kutoka pwani hadi
Kongo, ilitokea lahaja ya pekee iliyojulikana kama Kingwana ambayo
ilitumika na kuenea katika maeneo Kongo. Kimuundo na kimsamiati lahaja
ya Kigwana inafanana sana na lugha nyingine za Kibantu zina zotumika
huko.
Kuenezwa kwa dini za kigeni
Kuenea kwa dini za kigeni kama Uislamu na Ukristo
kulichukua nafasi kubwa katika maisha ya wenyeji. Waarabu waliotopea
katika dini ya Uislamu walitumia Kiswahili. Wahubiri wa Kiislamu
walilazimika kujifunza Kiswahili kwani wenyeji hawakujua Kiarabu.
Wahubiri hawa walilazimika kujifunza Kiswahili kueleza mafungu ya Korani
kwa lugha inayoeleweka kwa wengi. Wahubiri hawa walianza kutumia
maandishi ya Kiswahli wakitumia alfabeti za Kiarabu. Kwa kufanya hivyo,
walisaidia sana kukieneza Kiswahili.
Kwa upande wa dini ya Kikristo, Wamisionari hawakutaka sana
kuitumia lugha ya Kiswahili na waliifananisha na Uislamu. Wao
walipendelea kutumia lugha za asili lakini walikosea kwani ilikuwa
vigumu kujifunza lugha zote za wenyeji pamoja na kuziandika.
Wangefanikiwa zaidi kama wangetumia lugha ya Kiswahili kwani ingetumiwa
na waumini wengi. Baadaye walilazimika kutumia Kiswahili kuhubiri na
kuandika. Kwa kuanzia walianzisha shule za dini kwa ajili ya
mafundisho ya Kikristo. Wamisionari ndiyo walioanza kutumia alfabeti za
Kirumi kuandikia mahubiri yao.
Kwa kuanzia wamisionari waliandika vitabu na hata
kuchapisha magazeti kwa kutumia Kiswahili. Tunayo magazeti
yaliyochapishwa na yalisaidia sana kukieneza Kiswahili, kwa mfano:
- Habari za mwezi -1988
- Pwani na bara - 1910
- Barazani - 1910
- Rafiki yangu
- Habari za Wakilindi 1903
- Gazeti la Msimulizi
- Kitabu cha Wakilindi.n.k.
Wakati wa Ukoloni
Viko vipindi vitatu vya ukoloni vilivyokuwa na
athari kubwa kwa lugha ya Kiswahili. Kipindi cha kwanza kilikuwa ni
ukoloni wa Kiarabu. Kipindi hiki kilihusika moja kwa moja na ueneaji wa
Kiswahili. Wakati huo Sultani wa Zanzibar alitawala Visiwa vya Pemba na
Unguja pamoja na ukanda wa maili kumi wa eneo la Pwani ya Kenya na
Tanganyika. Kiswahli kilitumika katika kuandika na kutafsiri mafundisho
ya dini ya Kiislamu.
Shule za madrasa zilitumia Kiswahili kote bara na visiwani.
Kiswahili wakati wa kupigania uhuru
Ukoloni wa Kijerumani ulikuta Kiswahili kimeanza kutumika kwa
wingi na hivyo Wajerumani wakaanza kukitumia katika utawala wao. Shule
za awali zilizojulikana kama kindergarten zilianzishwa pamoja
na vituo vya elimu watu wazima. Wafanyakazi kama Maakida, Matarishi na
Maliwali walitakiwa wafahamu Kiswahili kabla ya kuajiriwa. Kwa upande wa
Kenya, shule nyingi za madrasa zilifundisha kwa lugha za kienyeji na
baadhi kwa Kiswahili.
Baada ya Wajerumani waliofuata ni Waingereza.
Waingereza walifanya kazi kubwa ya kukiendeleza na kukikuza Kiswahili.
Azma ya Waingereza ya kukikuza Kiswahili ni kwa ajili ya kupata
wafanyakzi wa kiwango cha chini kwa ajili ya kuwapata wasaidizi katika
ngazi ya chini. Kwa Waingereza, sera zao hazikuruhusu Kiswahili kitumike
kwa kiwango cha juu kwa ajili ya kufundishia. Kiwango kilichoruhusiwa
ni kufundisha shule za msingi tu. Kiswahili kilichukuliwa kama lugha
ya kitwana. Lugha ya mabwana ilikuwa ni Kiingereza ambayo ilitumika
kuanzia shule za sekondari na katika mawasiliano kama lugha ya kazi. Hii
ililandana na sera yao ya lugha katika nchi zote za Afrika Mashariki
kama Kenya, Uganda na Zanzibar na Tanganyika.
Mwaka 1925 ulifanyika mkutano wa wakuu wa elimu
wa nchi za Afrika Mashariki na kupendekeza kuwa ipatikane lugha ya
Kibantu itakayotumika kama lugha ya kufundishia. Ilionekana kuwa
Kiswahili ndiyo lugha itakayoweza kutumika katika kiwango cha elimu ya
msingi. Tatizo lililokuwapo ni kuwa kulikuwa na lahaja nyingi za
Kiswahili. Ilibidi iamuliwe kuwa lahaja ya Kiunguja itumike baada ya
kusanifiwa. Uamuzi huo ulifanyika mwaka 1928 wa kukiteua Kiunguja kuwa
ni lugha rasmi ya kufundishia elimu katika kiwango cha msingi. Kwa
msingi huo iliundwa Kamati ya Lugha ya Afrika Mashariki
(Inter-Territorial Language (Swahili) Committee ambayo ilianza kazi
rasmi mwaka 1930. Kazi za kamati hii ilikuwa:
- Kusanifisha ortografia itakayotumika katika nchi za Afrika Mashariki.
- Kuweka ulinganifu wa maneno yaliyopo na yale mapya kwa kusimamia uchapishaji wa kamusi za shule.
- Kuwa na ulinganifu wa sarufi utakaotumika katika uchapishaji wa vitabu.
- Kuwatia moyo na kuwasaidia waandishi wa vitabu wanaokusudia kuandika.
- Kusahihisha vitabu vya shule ambavyo vimeshachapishwa na kufanya masahihisho pale yatakapohitajika.
- Kutafsiri kwa Kiswahili vitabu vya kiada na ziada na pale inapowezekana kuandika vitabu vipya vya kiada na ziada.
- Kuandaa vitabu vya shule vya kiada na ziada vitakavyotumika kila mwaka.
Hizi ni baadhi tu ya kazi za kamati hii ya
Kiswahili. Matokeo yake ni kuwapo kwa kamusi zilizotayarishwa na
nyingine kuhaririwa kama:
- A Standard Kiswahili-English Dictionary
- A Standard English- Kiswahili Dictionary
- Kamusi ya Kiswahili –Kiswahili
Kamati hii ilipoanzishwa mwaka 1930, ilipitia vipindi mbalimbali kama vile:
- Mwaka 1930- 1947 ilikuwa chini ya Magavana wa Afrika Mashariki.
- Mwaka 1948 – 1952 ilikuwa chini ya Kamati Kuu ya Afrika Mashariki
- Mwaka 1953 – 1962 ilikuwa chini ya Chuo Kikuu cha Makerere.
- 1962-1964 ilikuwa chini ya Chuo Kikuu Kishiriki cha DSM katika Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (TUKI).
Taasisi nyingine iliyoanzishwa wakati wa ukoloni
wa Kiingereza ilikuwa ni East African Literature Bureau. Kazi kubwa ya
taasisi hii ni kuwatia moyo waandishi chipukizi kuhusu masuala ya
uandishi. Kazi nyingine ni kupitia miswada ya vitabu vya Kiswahili na
kuthibitisha ubora wake. Muhuri wa Ithibati ulisimamiwa na taasisi hii.
Pamoja na lawama nyingi tunazotoa za kukiboronga
Kiswahili, inatubidi tukiri kuwa Waingereza wamechangia sana katika
ukuzaji wa Kiswahili na kutufikisha hapa tulipo sasa.
Kiswahili wakati wa kupigania uhuru
Wakati wa kipindi cha kupigania uhuru wa
nchi za Tanganyika na kwa kiasi kikubwa Kenya, Kiswahili ndiyo
lugha iliyotumika kuwaunganisha wananchi wa nchi hizi. Kwa upande wa
Tanganyika wakati harakati za siasa zilipoanza kupamba moto hasa kipindi cha harakati za chama cha
Tanganyika African Association (TAA), mbinu za chinichini zilizokuwa
zikifanywa zilitumia Kiswahili. Hata Chama cha Tanganyika African
National Union (TANU) kilipoanzishwa rasmi 1954, viongozi wake walikuwa
wakisafiri mikoani na wilayani wakitumia Kiswahili kuwashawishi wananchi
kujiunga na harakati za ukombozi. Nyimbo zilikuwa zinatungwa na kuimbwa
nchi nzima. Mwalimu J.K. Nyerere akiwa Mwenyekiti wa TANU alitembea
nchi nzima akifuatana na wenzake na lugha mahususi iliyotumika ilikuwa
ni Kiswahili. Ni sehemu chache sana ambapo lugha za kikabila zilitumika
na kuhitaji mkalimani wa Kiswahili. Kwa maana hiyo, Kiswahili kilikuwa
ni alama ya umoja, uzalendo na uhuru.
Huko Kenya wakati wa utawala wa Uingereza,
Kiswahili kilitumika kwa baadhi ya shule za msingi hasa maeneo ya pwani.
Kiswahili kilitumika sana wakati wa harakati za kupigania uhuru.
Wakoloni wa Uingereza walipobaini kuwa Kiswahili kinatumika kama nguzo
ya umoja wa Wakenya, wakaanza kukipiga vita na kushauri lugha za
makabila zitumike kama lugha za kufundishia katika shule za msingi kwa
lengo la kuvunja umoja wa Wakenya.Viongozi wa KANU na hasa Hayati Mzee
Jomo Kenyetta alitumia sana Kiswahili wakati wa harakati za kupigania
uhuru wa Kenya.
Kwa upande wa Uganda, Kiswahili kilipigwa vita na
Wamisionari na pia Watawala wa Baganda wakidai kuwa Kiswahili
kilichotumiwa sana na wafanyabiashara hasa Waarabu na kuhusishwa na dini
ya Kiislamu na biashara ya watumwa. Pamoja na pingamizi zilizokuwapo,
Kiswahili kiliendelea kutumika katika majeshi (ya ulinzi na polisi).
Kiswahili baada ya Uhuru
Baada ya nchi za Afrika Mashariki kupata uhuru
(Tanganyika 1961, Uganda 1962, Kenya 1963 na Zanzibar 1964 baada ya
Mapinduzi, kila nchi ikawa na kipaumbele chake katika sera ya lugha.
Nchini Tanganyika na Kenya, Kiswahili kilitumika kujenga umoja na
kilifanywa kuwa ni lugha ya taifa kwa nchi hizi mbili.
Kwa upande wa Tanganyika, Kiswahili kilifanywa
kuwa ni lugha ya kufundishia masomo yote katika shule za msingi na pia
kama somo kuanzia darasa la kwanza hadi la nane/saba. Kwa upande wa
sekondari, Kiswahili kinatumika kama somo kuanzia kidato cha kwanza hadi
cha nne na kwa kidato cha tano na sita ilikuwa ni somo la upendeleo na
si la lazima. Hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Tanganyika katika kukiendeleza na kukikuza Kiswahili ni kwa kuanzisha asasi kadhaa kama :
- Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (TUKI) katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
- Idara ya Kiswahili kwa ajili ya kufundisha fasihi na isimu baada ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuundwa kwa Sheria ya Bunge, 1970.
- Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima 1975
- Baraza la Kiswahili la Taifa (Bakita) 1976
- Taasisi ya Kiswahili na Lugha za Kigeni (TAKILUKI), Zanzibar kwa ajili ya kufundisha, kukuza na kuendeleza Kiswahili na pia lugha za kigeni kama Kiarabu, Kifaransa, Kireno, Kijerumani na Kiingereza.
- Baraza la Kiswahili Zanzibar (Bakiza)
Nchini Kenya
Kiswahili kilipata msukumo mkubwa baada ya Rais
wa Kenya Mzee Jomo Kenyetta kutoa kauli kuwa Kiswahili kinafaa kuwa
lugha rasmi kwa nchi ya Kenya na kuwa hapo baadaye kingekuwa ni lugha ya
mawasiliano katika Bunge. Mwaka 1975 Kiswahili kilianza kutumika katika
Bunge la Kenya. Ili kufanikisha azma hii, Ofisi ya Bunge la Kenya
ilimtuma mtaalamu wake kuja Tanzania kuonana na viongozi wa Bakita ili
kushauriana kuhusu istilahi zilizosanifiwa na kukubaliwa kuwa ni
istilahi rasmi za Bakita na kulinganisha orodha hiyo na ya Kenya.
Inafahamika kuwa vyuo vikuu vyote vya serikali
nchini Kenya vilivyoanzishwa miaka ya 1980 vinafundisha somo la
Kiswahili kwa kutumia Kiswahili. Mifano hai ni Chuo Kikuu cha Nairobi,
baadaye Chuo Kikuu cha Kenyatta na cha Moi. Kwa utaratibu huu idadi ya
wahitimu wa Kiswahili wa kiwango cha digrii ya kwanza nchini Kenya ni
kubwa ikilinganishwa na idadi ya wahitimu wa Kiswahili kutoka Tanzania.
Kiko chama nchini Kenya kinachojulikana kama
Kenya Kiswahili Association ambacho wanachama wake ni walimu pamoja na
wakuza mitalaa wa Kiswahili katika shule za sekondari. Pia wako
wanafunzi wa Kiswahili walioungana na wenzao wa Tanzania na kuanzisha
chama cha kukuza Kiswahili kinachojulikana kama CHAWAKAMA. Chama hiki
kinawaunganisha wanafunzi wote wa Kiswahili wanaosoma katika vyuo vikuu
vya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Huandaa semina na warsha za Kiswahili
kila mwaka na hukutana kwa nchi wanachama kwa mzunguko.
Suala linalotokana na mfumo wa elimu ya Kenya wa 8-4-4
unawalazimisha wanafunzi wa shule za msingi na sekondari kuchukua somo
la Kiswahili kama somo la lazima. Hatua hii itawafanya wanafunzi wa
shule za msingi na sekondari nchini Kenya kuona umuhimu wa lugha ya
Kiswahili.
Kiswahili kwa Wananchi wa Afrika Mashariki
Lugha ya Kiswahili ni lugha muhimu katika masuala
ya siasa, elimu, uchumi, biashara na utamaduni. Kwa maana hiyo,Kiswahili
kina nafasi kubwa kwa maendeleo ya Afrika Mashariki. Tumeona kuwa
lugha ya Kiswahili inawaunganisha watu na kuwaletea umoja. Hakuna lugha
nyingine ambayo imeenea sehemu kubwa ya Afrika Mashariki kama Kiswahili.
Kwa mfumo huu ndiyo lugha inayoweza kuleta maelewano katika masuala ya
kisiasa kwa wananchi wote.
Katika masuala ya kiuchumi, Kiswahili kinatumika
kama lugha ya mawasilano kwa upande wa biashara. Wakenya wanaweza kwenda
sehemu yoyote ya vijijini nchini Tanzania na kufanya biashara bila
shida. Sehemu nyingine wanazoweza kutumia Kiswahili katika biashara ni
Mashariki mwa Kongo na kwa kiasi fulani Rwanda na Burundi.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment