Serikali kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara,
imeingilia kati mgogoro wa Kiwanda cha Nguo cha Urafiki kwa
kuwasimamisha kazi Meneja Mkuu wa kiwanda hicho, Nassoro Baraza na Naibu
Meneja Mkuu, Samweli Swai ili kupisha uchunguzi dhidi yao ufanyike na
endapo watabainika kuwa ni chanzo cha mgogoro huo watachukuliwa hatua za
kisheria.
Aidha, serikali imetoa miezi sita kwa kiwanda hicho kiwe kimewalipa
wafanyakazi madai yao mbalimbali sambamba na kuanza kulipa nyongeza ya
mishahara wanayodai kama sehemu muhimu ya kumaliza kabisa mgogoro huo.
Akitoa agizo hilo jana, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Uledy Mussa,
alisema serikali imeona ni vema kufanya maamuzi magumu kwa mtu mmoja au
wawili ili kunusuru uwapo wa nguvu kazi nyingi hasa kwa watu wanaohitaji
kutimiziwa haki zao za msingi.
Uledy pia alikitaka kiwanda hicho kuwalipa wafanyakazi wote kiwango
kipya cha mishahara yao ya Sh. 150,000 ifikapo mwishoni mwa Desemba
mwaka huu, kama wizara ya kazi na ajira inavyosema kupitia mwongozo wa
mishahara ya wafanyakazi nchi.
Licha ya hayo, pia Uledy alisema serikali ipo katika hutua za
mwisho kutafuta muwekazaji mpya katika kiwanda hicho ambaye atahakikisha
analinda maslahi ya wafanyakazi na taifa kwa ujumla.
“Hatua hiyo ni muendelezo aliokuwa akifanya aliyekuwa Waziri wa
Viwanda na Biashara, Marehemu Dk. Abdallah Kigoda,”alisema Uledy.
Pamoja na madai mengine, wafanyakazi hao pia wanahitaji kujua
hatma ya wastaafu kulipwa Sh. 200,000 mara baada ya kustaafu, jambo
ambalo Uledy alihitaji muda tena kabla ya kutoa jibu kamili kwa madai
kwamba hakuwa na uwezo wa kulitolea ufafanuzi kwa wakati huo.
Katika hatua nyingine wafanyakazi wa kiwandani hicho wamemtaka
Katibu wa Chama cha Wafanyakazi (Tuico), Florian Makero, kujihuzulu
wadhifa huo kwa kile kunachodai kuwa ameshindwa kuwatetea katika
kutafuta haki zao kuwa upande wa uongozi.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment