Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein.
Wahitimu wa Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya
Zanzibar, wametakiwa kuacha tabia ya kupiga chenga wanapopangiwa kufanya
kazi kisiwani Pemba jambo linalosababisha upungufu wa wataalam katika
sekta ya afya kisiwani hapa.
Wito huo umetolewa na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, kwenye Mahafali ya 22 ya Chuo hicho yaliyofanyika Mbweni Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja jana.
Wito huo umetolewa na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, kwenye Mahafali ya 22 ya Chuo hicho yaliyofanyika Mbweni Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja jana.
Akisoma hotuba kwa niamba ya rais, Makamu wa Pili wa Rais wa
Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, alisema kuna wahitimu wa fani ya afya
Zanzibar wamekuwa wakipiga chenga kufanya kazi kisiwani Pemba.
Alisema kwa mujibu wa sheria, watumishi wa umma wanatakiwa kuwa
tayari kufanya kazi sehemu yoyote watakayopangiwa na kuwataka kubadilika
na kuwa tayari kuwatumikia wananchi kokote ili kufanikisha mpango wa
kuimarisha huduma za afya kwa wananchi wa Zanzibar.
“Nimefurahi kusikia kuwa katika orodha ya wahitimu wetu wa fani za
afya chuoni hapa wapo waliotoka Tumbatu, Kojani, Fundo, Mtende na maeneo
mengine ambayo watu wengi huwa wanaona tabu kwenda kufanya kazi
kutokana na mazingira ya kijiografia yaliyopo,“ alisema Balozi Seif.
Katika hotuba yake, Dk. Shein pia aliitaka Wizara ya Afya kufanya
tathmini ya mahitaji ya wataalam wa afya ili kufahamu changamoto zake na
hatua za kuchukua.
Aidha, alisema uwekezaji katika sekta ya afya Zanzibar umeanza
kuleta mafanikio makubwa baada ya wawekezaji wa ndani na nje kujitokeza
na kuanzisha hospitali kubwa visiwani hapa.
Alisema juhudi zinazochukuliwa na serikali katika kuimarisha huduma
za afya kwa kushirikiana na wawekezaji na washirika wa maendeleo,
zimekuwa na mchango mkubwa katika kukuza pia soko la ajira hasa kwa
wahitimu wa chuo hicho.
“Machi mwaka huu nilialikwa kuifungua Hospitali ya Tasakhtaa
inayoendeshwa na Global Hospital ya India katika Mtaa wa Vuga. Hii ni
hospitali ya kisasa yenye uwezo mkubwa wa kutibu maradhi mbalimbali,“
alisema DK. Shein katika hotuba yake.
Hata hivyo, aliwataka wahitimu wa Chuo cha Taaluma za Sayansi za
Afya Zanzibar, kuchangamkia ajira zinazotolewa na serikali na sekta
binafsi wakitambua kuwa hospitali zote zina lengo la kuimarisha huduma
za afya kwa wananchi wa Zanzibar.
Wahitimu 440 walihitimu na kufanikiwa kupata stashahada, hiyo ikiwa
ni karibu mara mbili ikilinganishwa na wahitimu 280 wa mwaka 2014.
Muhitimu Faika Karim Zam, aliuomba uongozi wa chuo hicho kuanzisha
mafunzo ya ngazi ya Shahada na Diploma ili kuwapunguzia gharama za
kusoma ngazi hiyo nje ya Zanzibar.
Mapema Mkuu wa chuo hicho, DK. Haji Mwita Haji, alisema uongozi wa
chuo chao kupitia baraza lake umeamua kuongeza majengo zaidi ili
kuwahudumia vema wanafunzi wanaoamua kujiunga na chuo hicho.
Awali Naibu Waziri wa Afya Zanzibar, Mahmoud Thabit Kombo,
aliwataka wahitimu kufuata maadili ya kazi zao ili kupunguza au
kuondosha malalamiko ya huduma mbovu kutoka kwa wananchi.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment