Social Icons

Pages

Monday, December 07, 2015

MIL 675/- ZANUFAISHA KAYA 17,162 SENEREMA

Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).
Jumla ya Sh. 675,436,159 zimetumika kwa ajili ya kuzilipa kaya 17,162 zilizopo wilayani Sengerema katika mkoa wa Mwanza kwa ajili ya kuzikwamua kuondokana na wimbi la umaskini.
Mratibu wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf) wilayani humu, Rehema Simeon, akizungumza wakati wa kuzikabidhi kaya maskini za vijiji tisa wilayani humu, alisema lengo la mfuko huo ni kuwaondolea umaskini wananchi hao.
“Tuna vijiji 106 kati ya 153 ambavyo wananchi wake wapo katika malengo ya kuondolewa umaskini na Tasaf, leo tunamalizia kaya za vijiji tisa kwa awamu ya tatu baada ya kuanza Julai, mwaka huu na kukamilika Desemba, mwaka huu,” alisema Simeon.
Alivitaja vijiji ambavyo baadhi ya kaya zilikabidhiwa pesa kwa ajili ya kujikwamua na umaskini ni Mnadani, Mtakuja, Kizugwangoma, Kanyamwanza, Butonga road, Sima, Isungang’holo, Ishinshangholo na Ilyamchele.
Alisema walengwa waliondolewa umaskini kwa kupatiwa fedha za mtaji wamekuwa wakipatiwa kati ya Sh. 20,000 hadi 78,000 kwa kila kaya hususani zikiwalenga akinamama ambao ni wasimamizi wakuu wa familia.
Hata hivyo, alisema changamoto wanayokabiliana nayo ni pale wanapokuta kaya imehama ama kufariki dunia na wenyeviti kudai kutaka kuachiwa fedha hizo kwa makusudi ya kuzipatia familia ya kaya husika.
Naye Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya mji Sengerema, Vincent Bushaija, aliwataka walengwa wa kaya zilizopata fedha hizo, kujiwekea malengo ya kuzitumia na kupata mabadiliko ya kimaisha.
“Tunataka tuone watoto wanaenda shule wakiwa na sare na madaftari, akinamama waende kliniki kupeleka watoto wao na familia katika kaya kupata milo mitatu kwa siku badala ya miwili,” alisema Bushaija.
Bushaija alisema kutolewa kwa fedha hizo ni mpango wa serikali kuboresha afya, watoto wapelekwe kliniki pamoja na shule wakiwa nadhifu kwa kuvaa sare za shule.
Stephania Msabaha, ambaye ni mlengwa wa mfuko huo, alisema mpango huo wa Tasaf kuwaondolea umaskini ni mzuri, hivyo kiasi alichopata kitamsaidia kuendesha shughuli za ufugaji wa kuku wa kienyeji na kutunza wajukuu zake watatu.
Mkaguzi wa ndani wa Halmashauri na Tasaf, Theopasta Nyabange, alisema amekuwa wakifuatilia na kukagua iwapo kama mlengwa amelipwa kinachostahili ama la.
Nyabange alitoa wito kwa kuwataka wasimamizi walipe kwa utaratibu uliopo ili kuepukana kuingia katika matatizo.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: