Social Icons

Pages

Thursday, June 04, 2015

WATANGAZA NIA CCM WANATUTENGENEZEA NJIA-UKAWA

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika akitoa maoni yake juu ya Bajeti Kuu iliyosomwa Bungeni mjini Dodoma juzi.
Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), umesema vita ya kurushiana maneno miongoni mwa makada wa CCM wanaotaka kugombea urais ni faraja kwao, kwani inawasafishia njia ya kuingia Ikulu .
Katibu Mwenza wa umoja huo, John Mnyika alisema hayo jana alipokuwa akichambua hotuba za makada wa CCM waliotia nia kwa nyakati tofauti ya kuwania nafasi ya Urais.
Alisema wagombea wote ndani ya CCM wanapaswa kujua kuwa hawawezi kushinda uchaguzi ujao kwa kuwa tayari Watanzania wamekichoka chama hicho.
“Nimesikia ahadi zao za kuomba kura, lakini wajue serikali ijayo itakuwa ni ya Ukawa na sisi ndio tutaunda Serikali ya Umoja ya Kitaifa kupitia Ukawa,” alisema.
Mnyika alisema kitendo cha makada hao wa CCM kutangaza nia huku wakipigana vijembe vya chinichini, ni faraja kwa Ukawa kwani ‘vita ya panzi ni neema ya kunguru.’ “Waendelee na migogoro yao tu na kutangaza nia kwenye luninga, lakini wajuwe wananchi tayari wamewakataa kutokana na kusaliti maoni yao waliyotoa juu ya Katiba,” alisema.
Mnyika alisema Chama Cha Mapinduzi hakiwezi tena kuaminika machoni pa Watanzania, kwani ukifika wakati wa kula rushwa, kutetea mafisadi wapo pamoja na hivyo chama hicho kimegeuka cha mafisadi. “Wamewasaliti wananchi na kutetea wala rushwa mkaguzi na mdhibiti wa hesabu za serikali anawataja wezi lakini hawachukuliwi hatua” alisema.
Mnyika alisema ukawa haimuogopi mgombea yoyote wa CCM na wakati ukifika watamtangaza mgombea wao na ndiye atakuwa Rais.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: