Social Icons

Pages

Thursday, June 04, 2015

WAMACHINGA WAMLILIA JK KUUZWA MACHINGA COMPLEX

Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Dk. Didas Masaburi.
Umoja wa wafanyabiashara Soko la Machinga Complex, jijini Dar es Salaam, umeeleza kusikitishwa na tetesi za kuuzwa kwa jengo hilo kwa mwekezaji kutoka China hivyo kumwomba Rais Kikwete, kuingilia kati kabla hajaondoka madarakani.Tetesi hizo zilibainishwa jana na Makamu Mwenyekiti wa umoja huo, Gerald Mpangama, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maendeleo ya soko hilo na kupinga taarifa aliyodai kutolewa na Meya wa jiji hilo, Dk. Didas Masaburi, kwamba hatambui upangaji wa shule ya Lamoon kwenye jengo hilo.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti huyo, suala la uuzwaji wa jengo hilo lililojengwa kwa mkopo na Shirika la Hifadhi la Jamii (NSSF), kwa Sh.bilioni 12, lilijadiliwa katika kikao chake cha bodi hivi karibuni. Alisema wafanyabiashara hawako tayari kuona jengo hilo, ambalo lilijengwa na serikali kwa ajili ya kupunguza changamoto ya maeneo ya kufanyia biashara kwa wafanyabiashara ndogondogo ‘machinga’, likiuzwa.
“Sisi wafanyabiashara wa Machinga Complex, tunasema msimamo wetu utakuwa palepale kwamba jengo hili lilijengwa na serikali kwa ajili ya kutatua au kupunguza suala zima la maeneo ya kufanyia biashara kwa wafanyabiashara wadogowadogo nchini,” alisema na kuongeza:
“Tunaomba serikali kupitia Rais wetu, ambaye kwa nia na dhamira yake nzuri kwetu sisi na wafanyabiashara wadogo wa Machinga Complex, tunamuomba alizungumzie suala hili la uuzwaji wa jengo letu la Machinga Complex na kulitolea ufafanuzi katika moja ya hotuba zake za mwezi kabla hajaondoka kwenye kiti chake cha urais.”
Kwa mujibu wa Mwenyekiti huyo, hawajashirikishwa wala hawajui mauzo yake yataanza lini japokuwa tayari wameshabaini mwekezaji kutoka China akija  kupiga picha jengo hilo kwa madai ya mauzo ya takribani Sh. bilioni 38.
Kuhusu kupangishwa kwa shule hiyo katika jengo hilo, Mpangama alisema anayehusika kutia sahihi ya mkataba huo ni halmashauri ya jiji, ambao ndio wenye jengo na wala hakuna mahali popote katika nyaraka zake panapomruhusu meya wa jiji kuweka sahihi.
Akijibu malalamiko hayo, Mkurugenzi wa jiji hilo, Wilson Kabwe, alisema hana taarifa yoyote ya kuuzwa kwa jengo hilo, lakini wapo katika mazungumzo na NSSF kuhusu urejeshwaji wa deni hilo ambalo kwa sasa limefikia Sh. bilioni  34 kutoka Sh. bilioni 12.
Kwa upande wake, Masaburi alipotafutwa kuzungumzia suala hilo, simu yake haikuwa hewani na alipotumiwa ujumbe wa maandishi haukujibiwa. 

CHANZO: NIPASHE

No comments: