Waziri wa ushirikiano wa Afrika Mashariki Dk Mwakyembe.
Wakati Watanzania wakiendelea kufuatilia kwa shauku
kubwa msururu wa makada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wanaojitosa kwenye
mbio za kusaka ridhaa ya chama chao kuteuliwa kugombea kiti cha urais
Oktoba 25, mwaka huu, mitandao ya kijamii imevamiwa na mafundi wa
kutunga na kuumba habari na sasa hata Umoja wa Ulaya na Dk. Harrison
Mwankyembe wamechomekewa mambo dhidi ya Edward Lowassa.
Jana Umoja wa Ulaya (EU) ulikanusha vikali kwamba balozi wake
nchini alifanya mkutano na waandishi wa habari na kumtahadharisha Rais
Jakaya Kikwete kwamba nchi yake inaweza kuingia matatani na EU kama
Lowassa atateuliwa kuwa mgombea urais kupitia CCM.
Akizungumza na NIPASHE kwa njia ya simu jana, Ofisa Habari wa EU,
Susanne Mbise, juu ya taarifa za kuwako kwa kauli ya Balozi wa EU kwenye
mitandao ya kijamii kuhusu Lowassa na nia yake ya kuusaka urais,
alisema wamesikia taarifa hizo, lakini ukweli wa jambo hilo upo kwenye
taarifa waliyoweka kwenye mtandao wa Face Book ya Umoja huo.
Kadhalika, alituma kwa NIPASHE taarifa hiyo kwa njia ya mtandao wa intaneti. Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyosainiwa na Ofisa anayeshughulikia
Siasa na Habari, Luana Reale wa kitengo cha habari, Balozi huyo
hajafanya mkutano wowote na mwandishi yeyote na kwa maana hiyo hajatoa
taarifa yoyote kwa vyombo vya habari.
Reale alisema kuwa tangu Juni mosi mwaka huu Balozi huyo hayuko
nchini kwani alisafiri kwenda makao makuu ya Umoja huo na hajarejea
nchini. Alisema kuwa EU ina uhusiano mzuri wa muda mrefu na Tanzania ambao umejengwa juu ya misingi ya kuheshimiana na kuaminiana.
EU inatoa taarifa hizo baada ya watu wasiojulikana kusambaza
taarifa za uzushi na uongo kwenye mitando ya kijamii wakidai kuwa Rais
Kikwete ameonywa kwamba Lowassa akipitishwa kuwania urais uhusiano wa
Tanzania na EU utaingia shakani na kwamba hawataisaidia katika miradi ya
maendeleo.
Wazushi hao walidai kuwa Lowassa ni mtuhumiwa namba moja wa rushwa
nchini na kutaja kuwa anahusika katika kadhia ya Richmond na NIC. Wakati EU ikijiweka kando na uzushi huo, Dk. Mwakyembe ambaye ni
Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, naye alijiweka kando na
taarifa za uzushi zilizokuwa zinasambazwa kwenye mitandao ya kijamii
zikimnukuu kwamba ametoa taarifa kuhusu Richmond na kumwandama Lowassa.
Akihojiwa na redio moja nchini jana, Dk. Mwakyembe aliwataka
wanasiasa kuacha kujificha mgongoni mwake kwa lengo la kumshambulia
Lowassa. “Taarifa ile haikuwa ya kwangu, ni upuuzi. Mnanijua kwamba huwa
sikurupuki. Mimi ni waziri wa Serikali ambaye naheshimu wadhifa wangu,
hivyo siwezi kuandika mambo kama hayo. Nilipigiwa simu hata na wenzangu
wakiniuliza mbona nimeandika maneno makali,”alisema.
Dk. Mwakyembe alisema kuwa hana sababu ya kuendelea kujadili suala la sakata la Richmond kuhusu Lowassa na kuongeza: “Kama ni suala la kashfa ya Richmond, jamani mbona tulimtanguliza
Mungu? Tulifanya kazi yetu kwa haki na ripoti ya Bunge ipo. Sasa hakuna
haja ya unafiki…unafiki wa watu kutaka kumsema Lowassa halafu
wanajificha mgongoni kwangu.”
Alisema kuwa amekwisha kukamilisha hatua za awali za kutoa taarifa
katika mamlaka zinazohusika ikiwamo Polisi Makao Makuu Kitengo cha
uhalifu wa kimtandao (Cyber Crime), Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania
(TCRA) ili waweze kubaini mtandao huo ambao ulianza harakati zake tangu
Lowassa atangaze nia.
“Siyo uungwana kuchezea majina ya watu wanaokosa ujasiri wa
kuelezea hisia zao hadi watumie majina ya watu wengine, mtandao huo
nauona kuwa ni hatari,” alisema na kuongeza kuwa huenda kwa sababu ya
joto la uchaguzi ndiyo maana suala hilo likapewa msukumo.
Dk. Mwakyembe alisisitiza kuwa amedhamiria kukomesha tabia ya
kuchafuana kupitia mitandao ya kijamiina ndiyo maana amekwenda Polisi
Kitengo cha Cyber Crime (Mkosa ya Jinai ya Mtandao) na TCRA, kulalamikia
mchezo huo mchafu wa kihuni na tayari.
Tangu Mei 30, mwaka huu Lowassa alipotangaza nia ya kuwania urais kupitia CCM, limeibuka wimbi la mashambulizi dhidi yake. Mashambulizi mengine yamekuwa yakitolewa ama moja kwa moja au kwa
kuzunguka (innuendo) na makada wengine wa CCM waliotangaza nia ya kutaka
kuteuliwa na CCM kuwania kiti hicho.
Mbali na Lowassa makada wengine ambao wametangaza nia ni pamoja na
Stephen Wasira, Profesa Mark Mwandosya, Dk. John Magufuli, Frederick
Sumaye, Dk. Titus Kamani, Mwigulu Nchemba, Luhaga Mpina, Samuel Sitta na
Profesa Sospeter Muhongo.
Wengine ni Balozi Amani Karume, Balozi Amina Salum Ali na Amos
Siatemi. Msururu huo unatarajiwa kuongezaka kwani wengine wanatarajiwa
kutangaza nia na kuchukua fomu leo.
CHANZO:
NIPASHE

No comments:
Post a Comment