Social Icons

Pages

Friday, June 05, 2015

SIYANTEMI AJA NA MBINU MPYA KUZUIA UHALIFU

Kada wa CCM, Amos Siyantemi akipongezwa na wafuasi wake baada ya kuchukua fomu za kuomba kugombea kiti cha Urais wa Jamhuri ya Muungano kupitia chama hicho makao makuu ya chama hicho mjini Dodoma jana.
Mtumishi wa CCM katika Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, Amos Siyantemi, amesema idadi kubwa ya Watanzania wameanza kupoteza imani kwa Serikali na kuendelea kuamini kuwa chama hicho hakijali wanyonge.
Akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Halmashauri ya CCM mjini hapa jana baada ya kuchukua fomu ya kuomba ridhaa ya chama chake kuwania urais, Siyantemi alisema kaulimbiu yake ni Sura Mpya, Fikra Mpya.
Alisema endapo atateuliwa na chama chake na kuchaguliwa na wananchi kuwa rais, miongoni mwa mambo atakayozingatia ni kudumisha amani kwa kurejesha mfumo wa nyumba kumikumi akisema kutakuwa na daftari la wakazi litakaloorodhesha watu wote wanaoishi katika eneo husika na shughuli zinazofanyika.
Siyantemi ambaye alitumia nafasi hiyo kuzindua kitabu chake cha CCM na mapambano ya uongozi, alisema hali ya usalama nchini imeanza kulegalega kutokana na kukithiri kwa matukio ya uvamizi wa vituo vya polisi, mauaji ya askari, wizi wa silaha, mauaji ya albino, uhalifu wa kutumia silaha na aina nyingine. Kuhusu rushwa alisema endapo atafanikiwa kupata nafasi hiyo ya juu, atahakikisha kuwa watakaokamatwa na rushwa watafilisiwa mali zote.Mengine ambayo atayazingatia ni umoja na mshikamano wa Taifa, kuimarisha usalama wa nchi, kurejesha imani na matumaini ya wananchi kwa Serikali ya CCM. “Rushwa imeendelea kuwa ugonjwa mbaya kabisa unaoiangamiza jamii. Kwa sasa jamii yetu imegubikwa na matatizo makubwa kama vile kushamiri kwa tabia ya kuabudu mali na fedha hali iliyokuza ubinafsi miongoni mwa watu nchini,” alisema. Siyantemi alisema tofauti hiyo imesababisha kupanuka kwa tabaka dogo la walionacho dhidi ya idadi kubwa ya wasionacho wanaoishi katika lindi la umasikini, ujinga na maradhi.

Kupoteza imani na CCM
“Idadi kubwa ya Watanzania wameanza kupoteza imani kwa Serikali na kuendelea kuamini kuwa CCM kwa sasa ni chama kisichojali wanyonge na kwamba kimeachana na misingi yake ya ujamaa na kujitegemea,” alisema. Alisema machoni mwa Watanzania, CCM inaonekana kuwa chama kinachokumbatia matajiri na wafanyabiashara na si chama cha wakulima na wafanyakazi kama ilivyokuwa enzi za Mwalimu Julius Nyerere.
Siyantemi alisema atahakikisha anaongeza juhudi za pamoja za kupiga vita ujinga, umaskini, maradhi pamoja na kulipatia ufumbuzi tatizo la ukosefu wa ajira kwa kuchochea mapinduzi katika sekta mbalimbali ikiwamo kilimo na ufugaji. Aliahidi kufanya uwekezaji mkubwa wa maendeleo ya sayansi na teknolojia katika maeneo yote muhimu ikiwamo sekta ya elimu, sekta ya utoaji huduma na sekta ya uzalishaji mali, kuendeleza juhudi za pamoja za kuyapatia makundi mbalimbali fursa sawa kisiasa, kijamii, kiuchumi na kuutazama upya mfumo wa elimu. Alisema baadhi ya mikakati ya kufanikisha mapinduzi hayo ni pamoja na kufufua viwanda vya zamani, kujenga viwanda mama, viwanda vya kati, viwanda vidogo pamoja na viwanda vya kuongeza thamani ya bidhaa.
“Mikakati mingine ni kukuza sekta binafsi na kupanua fursa za uwekezaji, kuhimiza ari ya kufanya kazi kwa bidii na fikra za kimaendeleo miongoni mwa vijana, kuwahimiza Watanzania wakiwamo vijana kujiunga katika vikundi vya ushirika wa kuweka na kukopa pamoja na vikundi vya uzalishaji mali,” alisema.
Aliahidi kuwaboreshea maslahi ya watumishi wa CCM endapo atafanikiwa kuchaguliwa kuwa rais. Kwa mujibu wa utaratibu wa chama hicho, Rais wa nchi ndiye anayekuwa mwenyekiti wake.

Alivyochukua fomu
Siyantemi alifika kuchukua fomu akisindikizwa na watumishi wa makao makuu ya chama hicho wengi wao wakiwa wamevaa sare za CCM. Watumishi hao walionekana kushangilia karibu kipindi chote alichokuwa akizungumza na waandishi wa habari.
Baada ya kumaliza mazungumzo hayo, baadhi ya watumishi hao walikwenda kumkumbatia wakimpongeza.

Amos Siyantemi ni nani?
Amos Siyantemi alizaliwa Aprili 29, 1975 wilayani Magu mkoani Mwanza. Alipata elimu yake ya msingi katika Shule ya Nyambitilwa (1983-89), kabla ya kujiunga na elimu ya sekondari katika Shule ya Kinango kati ya mwaka 1994 na 1997.
Mwaka 1999 -2001 alikuwa Shule ya Sekondari Makongo akisoma kidato cha tano na cha sita, kabla ya kujiunga na Chuo kikuu cha Dar es Salaam alikohitimu Shahada ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa kati ya mwaka 2002-2005.
Mwaka 2007 hadi 2012 alikuwa katika Chuo cha Diplomasia Dar es Salaam alipohitimu Shahada ya Uzamili katika masuala siasa na uhusiano wa kimataifa.
Ajira yake ya kwanza ilikuwa ni katika ofisi ndogo za makao makuu ya CCM akiwa katibu msaidizi kwenye Idara ya Itikadi na Uenezi.
Mwaka 2006 alipata uhamisho kwenda Geita, ikiwa ni utaratibu wa CCM wa kuwaandaa watendaji wake kuyafahamu mazingira ya uongozi kwenye wilaya mbalimbali. Huko alihudumu cheo cha katibu msaidizi na mhasibu wa wilaya.
Mwaka 2008 alihamishiwa Kilwa mkoani Lindi akihudumu kwa nafasi hiyohiyo, mwaka 2009 aliteuliwa kuwa mjumbe wa Baraza la Umoja wa vijana CCM mkoani humo.
Mwaka 2010, alirudishwa tena makao makuu na kuwa katibu msaidizi mwandamizi kwenye Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa.
Mwa 2012, yalipofanyika mabadiliko na Dk Asha Rose Migiro, akachukua nafasi ya January Makamba na kuwa Mkuu wa idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa. Hapo ndipo alipopata nafasi ya kupandishwa daraja na kuwa katibu msaidizi mkuu, anayeratibu uhusiano kati ya CCM na vyama vya ukombozi nafasi anayoifanyia kazi hadi sasa.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: