Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta, amekuwa kada wa
tisa kutangaza nia ya kuomba Chama Cha Mapinduzi, kumpa ridhaa ya
kupeperusha bendera yake katika kinyang’anyiro cha uchaguzi mkuu,
Oktoba, mwaka huu.
Sitta alitangaza nia jana katika kijiji cha Itetemia mkoani Tabora,
makao makuu ya mashujaa wa Unyanyembe, walikotawala watemi Isike na
Kiyungi walioendesha harakati dhidi ya dhuluma na unyanyasaji wa
wakoloni.
Alisema iwapo atapewa nafasi ya kupeperusha bendera ya chama hicho,
atahakikisha anatenganisha masuala ya siasa na biashara kwa sababu
‘ishu’ hizo mbili ni chanzo kikubwa cha kuwapo rushwa kubwa na kusainiwa
mikataba mibovu. “Nina ari, uwezo na utayari wa kuimarisha nchi katika kipindi cha miaka mitano ijayo,” alisema.
RUSHWA
Waziri Sitta aliainisha baadhi ya vipaumbele atakavyosimamia kuwa
ni pamoja na kupambana kwa nguvu zote na rushwa kwa kutenganishe siasa
na biashara. Alisema rushwa kubwa zimekuwa na athari mbaya kwa uchumi wa nchi na
kusababisha kuwapo na mikataba mibovu ya huduma na mauzo, manunuzi
hewa, manunuzi yaliyojaa unyonyaji, uteuzi wa wazabuni kwa rushwa na
rushwa katika ajira ambavyo vimesababisha hasara ya trilioni za fedha
kwa taifa.
"Uchumi unakosa afya kutokana na kubanwa na rushwa ambayo sasa
imeenea mijini na vijijini...hatua ya kwanza hatuna budi kutenganisha
biashara na uongozi, hivyo mtu achague kushiriki kwenye biashara ama
siasa,” alibainisha Sitta.
Aliongeza kuwa kwa sasa baadhi ya wanasiasa na watumishi waandamizi
serikalini wanatumia nafasi zao kujitajirisha kwa kujipendelea, jambo
ambalo ni hatari wanasababisha kuchochea rushwa na usumbufu kwa
wananchi, kupunguza ari ya wafanyabiashara wa dhati na kudumaza
uwekezaji.
Alitaja hatua nyingine katika kukabiliana na rushwa ni kutunga
sheria mpya zilizo kali na zitakazokuwa na matokeo ya kumzuia mtu
asitamani kusaka rushwa, mali za viongozi zitamkwe kwa uwazi, mali
isiyolingana na kipato na kukosa maelezo ya kutosheleza kutaifishwa,
kesi za rushwa ziwe na utaratibu wenye uwazi na tume inayoshughulikia
maadili ya viongozi ipewe nguvu kubwa za uchunguzi na ufatiliaji wa mali
za viongozi bila kuzuiwa na mamlaka yoyote.
"Sambamba na kupiga vita rushwa, hatuna budi kuchukua hatua kali
dhidi ya hujuma za uporaji wa maliasili za nchi na rasilimali
zake…madini, misitu, vyanzo vya maji, bahari, maziwa na mito ni
rasilimali zisipotunzwa zitatishia uendelevu wa uchumi kwa vizazi
vijavyo, hivyo uhalifu dhidi ya maliasili na rasilimali za nchi itabidi
iwekwe sheria na taratibu kali," alisema.
MUUNGANO
Sitta ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, alisema
atahakikisha anaimairisha Mungano kutokana na kuonekana kuna mwelekeo wa
mifarakano, mshikamano hafifu kuwapo na chokochoko za siasa za
ushindani, udini na kupanuka kwa tofauti ya kipato na vijana wengi wasio
na ajira.
Kutokana na hali hiyo, Sitta ambaye alikuwa Spika wa Bunge la tisa,
alisema atatumia mchanganyiko wa uzoefu wa uongozi kutanzua changamoto
hizo zikiwamo za Muungano. Alisema kwa sasa zinajitokeza kauli na vitendo ambavyo vinaashiria
kutaka nchi mbili zilizoungana zitengane, wapo wanaodai Zanzibar
itanufaika iwapo itabaki huru bila muungano, na Bara nao wanawatazama
Wazanzibar ni wakorofi wasioridhika na chochote kinachofanywa na
serikali ya Muungano.
Alisema ili kuziweka nchi hizo mbili ni kudumisha Muungano na
kuuokoa hivyo kiongozi anayeweza kuzileta pamoja kambi hizi na kuuokoa
muungano pekee. “Ushiriki wangu katika serikali yetu tangu awamu ya kwanza ya
uongozi wa nchi yetu, unaniweka katika nafasi nzuri ya kuongoza mchakato
utakaowezesha kuzijadili na kuzipatia ufumbuzi changamoto za Muungano,”
alisema.
KATIBA
Kingine ni Katiba na kwamba licha ya muafaka kamili kuhusu Katiba
mpya kutofikiwa, lakini ile iliyopendekezwa ina maeneo mengi ya msingi
ambayo yanaweza kuleta ukaribu ikiwa ni hatua ya awali inayowezesha
kusonga mbele kwa amani.
"Naamini pande zinazosigana kuhusu Katiba zina wazalendo ambao
wanaweza kukubaliana kuwa na kipindi cha mpito cha utulivu na maelewano
kitakachotuwezesha kama taifa kusonga mbele, viongozi wa kisiasa na wa
jamii washawishike kukubali hoja mbili, hakuna mshindi wala mshindwa
katika kufikia kukubalika kwa Katiba ya taifa letu na katiba yoyote ni
waraka unaoenda unabadilika kulingana na mahitaji ya wakati husika,”
alisema.
UCHUMI
Sitta alisema jambo jingine ambalo atalipa kipaumbele ni kujenga
mfumo wenye motisha kwa wote, ili kuchochea uchumi endelevu na wa
viwanda ili kukuza uchumi wa nchi kwa kasi inayopunguza umaskini kwa
haraka.
"Tukijenga uwezo mkubwa zaidi wa bajeti ya serikali kutosheleza
ubora wa huduma za jamii kama vile afya, elimu na maji, hatuna budi
kufanya jitihada za makusudi za kuubadili mfumo wa uendeshaji nchi uwe
ni wa motisha kwa wazalishamali, mifumo ya nchi zilizopiga hatua kubwa
za maendeleo duniani ni ile iliyoweka mazingira chanya ya kuaminiana
baina ya serikali na sekta binafsi lakini kwetu haijatimia,” alisema.
Aliongeza kuwa wafanyabiashara wakubwa wa ndani hawawekezi vya
kutosha ndani ya nchi ili kuleta maendeleo ya haraka ya huduma, viwanda,
kilimo na biashara na baadhi yao baada ya kuchuma pesa wanazihamishia
nje ya nchi huku watendaji serikalini wakiwatazama wafanyabiashara ambao
hawana uzalendo na wakwepa kodi.
CHANZO:
NIPASHE

No comments:
Post a Comment