Mtemi Msagata Fundikira akiwa amemshika Margareth Sitta ambaye ni
mke wa Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta (kushoto) kwa ajili ya kuwapa
baraka ya na kuwapandisha cheo kuwa Mjukuu wa Mkubwa wa Unyanyembe,
kabla ya Waziri huyo kutangaza nia ya kugombea Urais, kwenye viwanja ya
Ikulu ya Itetemya Tabora jana.
Waziri wa Uchukuzi,
Samuel Sitta ametangaza nia ya kugombea urais kwa tiketi ya CCM,
akieleza kuwa anataka kulifanyia Taifa mambo matano, ikiwa ni pamoja na
kutenganisha biashara na siasa na kusimamia maadili ya viongozi wa umma.
Alitaja mambo mengine kuwa ni kusimamia Muungano,
kukamilisha mchakato wa kuandika Katiba Mpya, kuweka mfumo wenye motisha
kwa wote ili kuchochea uchumi endelevu na wa viwanda, vita dhidi ya
rushwa na kukiimarisha Chama cha Mapinduzi (CCM) kiuchumi.
Sitta alitangaza nia hiyo jana kwenye Ikulu ya Wanyanyembe iliyopo Itetemia, takriban kilomita saba kutoka mjini Tabora. “Ili kukomesha tatizo hilo (la rushwa), hatuna
budi kutunga sheria itakayotenganisha biashara na uongozi,” Sitta
alisema akiungana na Rais Jakaya Kikwete ambaye pia aliwahi kuahidi
kutenganisha siasa na biashara lakini hadi sasa bado hajatunga sheria
hiyo.
“Mtu achague moja, biashara au uongozi wa siasa.
Ikiwa mfanyabiashara atataka kuingia katika uongozi wa siasa itabidi
akabidhi mali na biashara zake kwa mdhamini atakayeziendesha wakati
mhusika anatumikia umma,” alisema Spika huyo wa Bunge la Tisa.
Alisema mikataba mibovu ya huduma na mauzo,
ununuzi hewa, ununuzi uliojaa unyonyaji, uteuzi wa wazabuni kwa rushwa
na hasa rushwa katika ajira, imelisababisha Taifa hasara kubwa.
Alisema hatua ya pili ya kupambana na rushwa ni
kutunga sheria mpya zilizo kali na ambazo zitakuwa na matokeo ya kumzuia
mtu asitamani kusaka rushwa. “Katika hilo tutahakikisha mali za viongozi
zinatajwa kwa uwazi. Mali isiyolingana na kipato na kukosa maelezo ya
kutosheleza itaifishwe, kesi za rushwa ziwe na utaratibu wenye uwazi,”
alisema mbunge huyo wa Urambo Mashariki.
“Tume inayoshughulikia maadili ya viongozi ipewe
nguvu kubwa za uchunguzi na ufuatiliaji wa mali za viongozi bila
kuzuiliwa na mamlaka yoyote. Pia Tume ifanye kazi zake kwa kuyaweka
mambo wazi kuhusu watuhumiwa, tuhuma zao, majibu yao na hatua
zinazofuatia. Vikao vya tume vya kusikiliza mashauri ya maadili viwe vya
wazi kwa wananchi.”
Alisema adhabu ya utoaji na wapokeaji rushwa
itakuwa kali na iambatane na mali zitakazothibitika kupatikana kwa
rushwa, zitataifishwa.
“Ikumbukwe kwamba, kiongozi tutakayemuamini
kupambana na rushwa hana budi awe na historia ya uadilifu wa muda mrefu
kama nilivyo,” alisema Sitta.
Sambamba na kupiga vita rushwa, alisema watachukua
hatua kali dhidi ya hujuma za uporaji wa maliasili za nchi na
rasilimali zake. “Madini, misitu, vyanzo vya maji, bahari, maziwa na mito ni
rasilimali ambazo zisipotunzwa zitatishia uendelevu wa uchumi kwa vizazi
vijavyo. Kwa hivyo uhalifu dhidi ya maliasili na rasilimali za nchi
itabidi uwekewe sheria na taratibu kali,” alisisitiza Sitta.
Mambo anayosimamia
Alisema mazingira ya rushwa pia yataangaliwa
pamoja na kuimarisha utawala bora. Tabia za watendaji serikalini
kusimamia taratibu zenye usumbufu kwa wananchi inazifanya huduma za
jamii zipatikane kwa tabu kubwa. “Tabia za njoo kesho na wananchi kuzungushwa
zungushwa wanapofuatilia haki zao itabidi zikomeshwe, zikemewe na ziwe
kigezo cha kuwapima watumishi,”alisema.
Akizungumzia uamuzi wake wa kutangaza kugombea
urais, Sitta alisema: “Kugombea nafasi ya urais wa nchi yetu si jambo
jepesi. Linahitaji fikra ya kina ukizingatia kuwa nafasi hiyo ya uongozi
inabeba matumaini ya Watanzania milioni 47. “Naamini kuwa kipindi cha uongozi cha 2015-2020 ni
kipindi chenye changamoto nzito za kitaifa ambazo zinahitaji aina ya
uongozi wenye uimara, uadilifu, uzalendo na maarifa thabiti ili kuivusha
nchi kwa usalama. alisema.
Sitta, ambaye anajulikana kama ‘Mzee wa Viwango’
kutokana na kaulimbiu aliyoitumia wakati akiongoza Bunge la Tisa ya
“Kasi na Viwango”, alisema mgombea yeyote makini wa nafasi ya urais,
hana budi kuyapima mazingira ya Taifa katika miaka mitano ijayo na
kuzielewa changamoto zitakazokuwapo katika kipindi cha uongozi
anachokusudia kuongoza.
“Kipindi cha miaka mitano ijayo kina mwelekeo wa
mifarakano katika masuala ya Muungano wetu, kutetereka kwa mshikamano
wetu kunakotokana na chokochoko za siasa za ushindani, udini na kupanuka
kwa tofauti ya kipato, ongezeko la kundi kubwa hususan la vijana mijini
lisilo na uhakika wa ajira na haya yote yanaashiria ongezeko la
uhalifu,” alisema.
Sitta, ambaye alianza kuteuliwa kuwa waziri miaka
ya sabini, alisema anaamini ana mchanganyiko wa uzoefu wa uongozi
unaomuwezesha kukusanya nguvu chanya za Watanzania ili kuyatatua
matatizo hayo. Ninaweza kufanya hayo yote kwa kuwa nimeitumikia Serikali
katika nafasi mbalimbali za uongozi kwa zaidi ya miaka 30. “Kwa kifupi ninao uelewa na uzoefu unaolingana na
changamoto za kipindi kigumu cha miaka mitano ijayo yenye mwelekeo wa
kutikisa misingi ya utawala wa nchi yetu… kwa uimara wangu wa uongozi,
nitajumuisha nguvu na maarifa ya wananchi ili tuvuke salama na pia
tutekeleze kazi za maendeleo kwa ufanisi na tija zaidi,” alisema Sitta.
Mambo anayosimamia
Sitta alisema katika vipaumbele vyake
atakavyosimamia akipitishwa na CCM na baadaye kushinda kwenye Uchaguzi
Mkuu, atahakikisha Muungano unaimarishwa licha ya kuwa na viashiria vya
kutaka uvunjwe.
“Pande zote mbili za Muungano zinatoa kauli na
vitendo ambavyo vinaashiria kutaka nchi zetu mbili zilizoungana
zitengane. Zanzibar, tunashuhudia wanasiasa wanaodai kuwa nchi hiyo
itanufaika zaidi ikirejea kuwa na uhuru kamili bila kuwa sehemu ya
Muungano,” alisema na kuongeza:
Aufagilia mchakato wa Katiba
Uchumi endelevu
“Baadhi ya watu wa Tanzania Bara wanawaona ndugu zao wa Zanzibar
kuwa ni wakorofi na wasioridhika na chochote kitakachofanywa na
Muungano, wanahisi kuwa mfumo wa huu unapendelea upande mmoja.”
Alisema hakuna shaka kwamba pande mbili za Muungano zikitengana kutazuka uhasama na matokeo yake ni kuvunjika kwa amani.
Alisema ushiriki wake katika Serikali tangu awamu
ya kwanza ya uongozi, unamuweka katika nafasi nzuri ya kuongoza mchakato
utakaowezesha kuzijadili na kuzipatia ufumbuzi changamoto za Muungano.
Aufagilia mchakato wa Katiba
Sitta, ambaye alikuwa mwenyekiti wa Bunge Maalumu
la Katiba, alisema pamoja na kuwa muafaka kamili kuhusu Katiba Mpya
haujapatikana, Katiba Inayopendekezwa ina maeneo mengi ya msingi ambayo
yanaweza kuwaleta karibu Watanzania.
“Hakuna mshindi wala mshindwa katika kufikia
muafaka wa kukubalika kwa Katiba ya Taifa letu. Katiba yoyote ni waraka
unaobadilika kulingana na mahitaji ya wakati husika,” alisema na
kubainisha kuwa hakuna Katiba duniani ya kumridhisha kila mmoja lakini
kadri muda unavyokwenda, inaweza kuboreshwa kwa kuzingatia maoni ya
wengi.
Uchumi endelevu
Sitta, ambaye pia amewahi kuwa mkurugenzi mtendaji
wa Kituo cha Uwekezaji kwa miaka tisa, alisema ili kukuza uchumi wa
nchi, lazima jitihada za makusudi zifanyike kuubadili mfumo wa
uendeshaji nchi, ili uwe na motisha kwa wazalishaji.
Alisema mfumo huo utasaidia kujenga uwezo mkubwa
zaidi wa bajeti ya Serikali, utakaotosheleza katika utoaji wa huduma
bora kwa jamii kama vile afya, elimu na maji.
“Mifumo ya nchi zilizopiga hatua kubwa za
maendeleo duniani ni ile iliyoweka mazingira chanya ya kuaminiana baina
ya Serikali na sekta binafsi. Hali hii haijatimia hapa kwetu,” alisema
Sitta.
Aliishukuru Serikali ya Awamu ya Nne ya Rais
Jakaya Kikwete akieleza kuwa imefanya kazi kubwa ya kutandaza
miundombinu, hususan barabara, mawasiliano na nishati.
“Sasa wakati umefika wa ushirikiano na kuaminiana
baina ya sekta binafsi na Serikali ili kuzifungua rasilimali za nchi
zirutubishe uchumi kwa faida ya wote,” alisema.
Kuimarisha CCM kiuchumi
Kwa nini alitangazia Ikulu ya Wanyanyembe?
“Mazingira ya Serikali na sekta binafsi kufanya kazi kama timu
moja yatafungua fursa nyingi za uchumi na hivyo kupunguza tatizo la
ajira kwa vijana.”
Kuimarisha CCM kiuchumi
Sitta ambaye amewahi Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya
Taifa (NEC) na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM 2005-2010, alisema: “Chama
tawala madhubuti ni nyenzo muhimu sana katika kuhakikisha kuwa wananchi
wanapata kwa ufanisi, huduma zote zilizoahidiwa kwenye ilani.
“Katika hili, ni wajibu wa mwenyekiti wa chama
kuhakikisha kwamba vitengo na vitegauchumi vya chama vinakuwa na tija
inayokiwezesha kuendesha shughuli zake kwa kujitegemea.
“Chama tawala kilicho imara kiuchumi kitakuwa na
watendaji wanaofanya kazi zao kwa kujiamini na hivyo kuisimamia Serikali
yake itimize wajibu wake kwa wananchi.
“Chama imara kiuchumi kitakuwa na ufanisi zaidi
katika kuendesha shughuli zake bila kujidhalilisha kwa kuomba misaada
kutoka kwa matajiri. Mfumo mzima wa chama unaozingatia nyenzo kamili na
masilahi endelevu kwa watumishi wake ni msingi bora wa kuendesha masuala
ya nchi kwa uadilifu.
“Nikibahatika kuchaguliwa katika nafasi ya rais na
kukiongoza chama, nitatumia uzoefu wangu wa miaka tisa na nusu katika
kukiongoza Kituo cha Uwekezaji Tanzania kuziunganisha shughuli za uchumi
za chama na wawekezaji makini ili kupunguza utegemezi wa chama kwa
ruzuku ya Serikali na pia utegemezi hatari zaidi kwa matajiri wachache,”
alisema.
Kwa nini alitangazia Ikulu ya Wanyanyembe?
Sitta alisema Ikulu ya Wanyanyembe ndiyo sehemu
iliyokuwa makao makuu ya mashujaa wa Unyanyembe kama Isike na Kiyungi
walioendesha harakati dhidi ya dhuluma na unyanyasaji wa wakoloni.
Alieleza asili ya neno Ikulu kuwa ni la Kinyamwezi
lenye maana ya Itetemia ambalo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere
mwaka 1961 alilitumia kumaanisha ‘State House’. “Neno hili maana yake
ni makazi ya mkuu wa nchi ambayo hapa Tanzania yako jijini Dar es Salaam
na mimi nimeamua kuanza safari yangu ya kuelekea Ikulu hapa.”
Alisema kitendo chake cha kutangazia nia ya
kugombea urais akiwa Ikulu ya Wanyanyembe kinaamnisha kuienzi sehemu
hiyo ambayo ina historia yenye kutukuka ya Itetemia.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI

No comments:
Post a Comment