Wifi wa aliyekuwa Mbunge wa Ukonga marehemu, Eugen Mwaiposa , Sauda
Mwaiposa, akilia baada ya kupata taarifa za msiba nyumbani Ukonga, Dar
es Salaam jana.
Mbunge wa Ukonga
(CCM), Eugen Mwaiposa amefariki dunia usiku wa kuamkia jana nyumbani
kwake eneo la Chadulu mjini Dodoma saa chache baada ya kutoka katika
kikao cha 19 cha mkutano wa 20 wa Bunge la 10.
Mbunge huyo alikuwa bungeni juzi wakati wa mjadala
wa Bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi na alimweleza Waziri
wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), Jenista Mhagama
kuwa ataiwekea ‘ngumu’ bajeti hiyo kama asingepatiwa majibu ya
kuridhisha.
Kifo cha mbunge huyo kinafanya idadi ya wabunge
waliofariki dunia tangu Januari mwaka hu kufikia wawili baada ya kifo
cha Kapteni John Komba aliyekuwa mbunge wa Mbinga Magharibi.
Taarifa za kifo cha Mwaiposa zilitangazwa jana saa
6:58 mchana na Naibu Spika, Job Ndugai na kusababisha wabunge kuanza
kuangua vilio, huku wakieleza jinsi walivyozungumza na marehemu juzi
jioni.
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto
Sofia Simba alisema mpaka wanaachana na marehemu alikuwa akisisitiza
zaidi suala la maendeleo ya wananchi wa jimbo lake na hakuonekana
anaumwa.
Kikao cha jana kilikuwa kikiongozwa mwenyekiti
wake Lediana Mng’ong’o na ilipofika saa 6:55 mchana alimpisha Ndugai
ambaye alitangaza taarifa za kifo hicho na kusitisha shughuli za Bunge
hadi kesho.
Akitangaza kifo hicho Ndugai alisema Mwaiposa alifariki dunia akiwa usingizini usiku wa kuamkia jana.
“Marehemu alikuwa akisumbuliwa na tatizo la
shinikizo la damu kwa muda mrefu. Hakika Bunge limepata msiba mzito.
Mwili wa marehemu umepelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti katika
hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma,” alisema.
“Taarifa zaidi tutazisambaza kupitia simu za
mkononi mara baada ya familia ya marehemu kufika. Kamati ya Uongozi
tukutane mara moja ili kujadili suala hili. Msiba uko nyumbani kwake
Chadulu,” alisema Ndugai.
Alisema shughuli za kuaga mwili wa marehemu zitafanyika leo nyumbani kwake Chadulu.
Nyumbani kwake Dar
Nyumbani kwa marehemu Kipunguni jijini Dar es
Salaam jamaa, majirani na watoto walikuwa kwenye hali ya majonzi, huku
ndugu wakishindwa hata kuzungumza. Katibu wa Siasa na Uenezi (CCM), Wilaya ya Ilala, Said Sidde
aliyekuwa nyumbani hapo, alisema juzi usiku walikuwa wakiwasiliana na
alihisi kuwa anaumwa lakini alipomuuliza mbunge huyo alijibu hana tatizo
lolote.
Wabunge wamlilia
Taarifa zaidi
Wasifu wa marehemu
CHANZO: MWANANCHI
Wabunge wamlilia
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera,
Uratibu na Bunge), Jenesta Mhagama alisema, “Jana (juzi) Mwaiposa
alinifuata na kuniambia kuwa muda wa kupitisha vifungu vya bajeti ya
wizara ya elimu atashikilia shilingi kwa ajili ya kujijenga jimboni
kwake. Mhagama alisema kilichomuuma zaidi ni tukio la
Mwaiposa kumpungia mkono wakati akiondoka bungeni juzi jioni, kitendo
alichotafsiri kuwa alikuwa akimuaga.
Simba alisema, “Jana (juzi) nilizungumza naye
kuhusu jimbo lake la Ukonga. Tulizungumza masuala ya kugawanywa kwa
majimbo na nilimpa moyo kuwa kama jimbo hilo likigawanywa atakuwa na
nafasi nzuri ya kushinda. “Aliniambia hana wasiwasi katika suala hilo kwa
sababu wananchi wa Ukonga wanampenda. Alinihakikishia hali yake ya
kisiasa katika jimbo hilo ni nzuri,” alisema Simba.
Aliongeza, “Hakuniambia anauwa ila kuna baadhi ya
watu aliwaeleza kuwa alikuwa anaumwa, aliwaambia kuwa alikuwa akiumwa
akiumwa na mishipa ya shingo.”
Kwa upande wa Mbatia alisema, “Nakumbuka jana
(juzi) nilipomaliza kuchangia bajeti ya elimu nilizungumza naye,
aliniuliza kuhusu jinsi ya kutatua foleni za Dar es Salaam.”
Taarifa zaidi
Taarifa zilizolifia gazeti hili zinaeleza kuwa
dereva wa mbunge huyo alikwenda nyumbani kwa bosi wake jana asubuhi
kumchukua kwenda bungeni, alipofika eneo analoishi aligonga mlango
lakini hakujibiwa.
Baada ya kuona hali hiyo alimpigia simu mume wa
marehemu ambaye aliwasiliana na mbunge mmoja ambaye aliondoka bungeni
akiambatana na polisi kwenda nyumbani kwake ambako walivunja mlango na
kukuta amekwishafariki.
Wasifu wa marehemu
Mwaiposa alizaliwa Novemba 23, 1960 wilayani Hai mkoani Kilimanjaro ambapo mpaka anakutwa na mauti alikuwa na umri wa miaka 55. Alipata elimu yake ya msingi katika Shule ya
Msingi Nkweseto mwaka 1967 hadi 1974 na kujiunga na shule ya sekondari
Masama mwaka 1976 hadi 1980 ambapo baadaye alipata elimu ya juu ya
sekondari katika shule ya biashara ya Shinyanga (Shycom) mwaka 1981 hadi
1983, baadaye alipata shahada mbili za uzamili, moja akiipatika katika
Chuo Kikuu cha Strathclyde kilichoko Glasgow, Scotland.
CHANZO: MWANANCHI

No comments:
Post a Comment