Tayari Maalim Seif Sharifu Hamadi, ameshachukua fomu ili kuomba ridhaa ya chama chake kimkubalie tena
kukiwakilisha kwa mara ya tano mfululizo kugombea kiti cha urais wa
Zanzibar.
Tafakuri ya Abuu Iddi leo itajikita kwenye uwezekano wa kushinda au kushindwa kwa Maalim Seif katika Uchaguzi Mkuu. Kabla ya kutafakari mazingira yaliyosababisha
Maalim Seif kushindwa au ‘kunyimwa’ ushindi katika chaguzi zilizopita,
kwanza tutafakari kwa pamoja ugumu wake wa kushinda katika Uchaguzi Mkuu
wa mwaka huu.
Kwanza, tukumbuke kwamba kura za wapinzani katika
uchaguzi zitagawanyika, hasa tukizingatia kwamba aliyekuwa miongoni mwa
mihimili mikuu ya CUF, Hamad Rashid atagombea nafasi ya urais wa
Zanzibar kwa tiketi ya chama chake kipya cha ADC. Ni kujidanganya kwamba
eti Hamad Rashid hana wafuasi wa kutosha kumuwezesha kutoa changamoto
kwa wagombea wengine.
Pili, tusisahau kwamba mazingira ya chama cha CUF
kwa mwaka huu katika kuomba kura za Wazanzibar yatapata uzito mkubwa kwa
sababu CUF ni sehemu ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa ya Zanzibar.
Kamwe CUF haitoweza kujinasua na ‘upungufu’
uliojitokeza katika uendeshaji wa serikali hiyo hasa ikizingatiwa kwamba
baadhi ya wizara nyeti zipo chini ya mawaziri kutoka chama hicho.
Tatu, Maalim Seif atakaposimama hadharani kuomba
kura za Wazanzibar kwa mara ya tano, atalazimika kuwaeleza atawafanyia
nini akiwa Rais wa Zanzibar, na yeye kama Makamu wa kwanza wa Rais wa
Zanzibar amewafanyia nini na ameshindwa kuwatekelezea nini akiwa kama
sehemu ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Maalim Seif atakumbana na maswali magumu, kwa
sababu haiwezekani kuipongeza au kuilaumu Serikali ya Zanzibar halafu
yeye pamoja na mawaziri wake kadhaa kutoka CUF wasiwemo.
Lakini tayari pia baadhi ya Wazanzibar wameshapata
wasiwasi hasa baada ya kuona mambo yakiendeshwa kinyume cha matarajio
yao katika baadhi ya zile wizara zilizomo katika mikono ya mawaziri wa
CUF. Maalim Seif asisahau kwamba changamoto hii itampunguzia kura zake.
Maalim Seif asisahau kwamba; unapomuahidi mtu kuwa
ukipata mkate mzima yeye utamgawia nusu yake, halafu ikatokea umepata
nusu yake na huyu uliyemuahidi anajua vyema hilo, matarajio yake ni
kwamba atapata robo ya mkate huo, kwani kama ungepata mzima ungelimpa
nusu.
Ikiwa umepata nusu na yeye hukumpa hata hiyo robo
halafu hali ikawa ni ya kawaida tu, tarajia kwamba ukimya wake unabeba
jambo zito moyoni mwake.
Vilevile Maalim Seif asiisahau changamoto mpya ya
Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu iliyozalishwa na tatizo la baadhi ya
wasiofahamu nguvu za mihimili mitatu ya nchi, kwamba kila mmoja mipaka
yake inakomea wapi.
Wapo baadi ya Wazanzibar wanaoamini kwamba watuhumiwa walioko
mahubusu katika magereza wanaweza kutolewa mara moja tu kwa amri ya
viongozi wa serikali.
Wenye mtazamo huo, walitarajia wamuone Maalim Seif
akilisimamia hilo hasa kwa kuzingatia kwamba baadhi ya madai ya
watuhumiwa wale ni kuidai Zanzibar yenye mamlaka kamili.
Kitendo cha Maalim Seif kukaa kimya na kuendelea
kubakia katika serikali ambayo ni “dhalimu” (kwa mtazamo wao) kinawapa
hasira ya kumsubiri kwenye sanduku la kura wamuwajibishe.
Changamoto nyingine itakayopunguza sana kura za
Maalim Seif ni kitendo cha “kula matapishi yake”. Tayari yeye aliitambua
Serikali halali ya Mapinduzi ya Zanzibar, na ndio maana akakubali kukaa
nayo, wakaendesha vikao vyenye mafanikio makubwa hadi kufikia mwafaka
uliozaa matunda haya ya kihistoria.
Ni vipi leo baada ya mafanikio hayo anakumbushia
tena yale ‘majeraha’ yaliyopita na kutamka hadharani kwamba safari hii
hatokubali tena kuporwa ushindi wake, akimaanisha kwamba hata uchaguzi
uliomfanya yeye kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais aliporwa ushindi.
Aliwezaje kukaa kikao pamoja na Serikali ‘isiyo
halali’ kisha akakubali yaliyoafikiwa katika kikao hicho kwa sababu tu
‘maslahi yake’ yamechungwa?
Changamoto nyingine itakayomfanya Maalim Seif
ashindwe ni ukosefu wa hoja zinazokinaisha juu ya vipi atashinda, kwani
yeye mwenyewe amewahakikishia Wazanzibar kwamba anashinda isipokuwa
anaporwa ushindi.
Wazanzibar wanasubiri awape mchanganuo na maelezo
yanayotosheleza kwamba amejipanga vipi kuzuia huo uporaji kama ni kweli
huwa anaporwa, kwa sababu mfumo wa upigaji kura ni ule ule na mfumo wa
ulinzi wa kura ni ule ule.
Kutokana na haya, ndiyo maana nikaonelea leo tusaidiane katika tafakuri kwamba: Je, Maalim Seif atashinda?
Kwa upande wangu, tafakuri inanipa natija kuwa
hawezi kushinda, kwa sababu yeye mwenyewe anashindwa kubainisha hizo
nguvu zitakazomfanya ashinde. Nihitimishe kwa kumpa nasaha hizi: Akumbuke kwamba kura ni siri tena siri kubwa.
Kwa hiyo anapojenga hoja kwamba amekuwa akishinda
na atashinda tu, aseme na kubakisha, kamwe asimalize maneno, kwani umati
unaojaa kwenye mikutano ya kampeni sio kielelezo halisi cha upigaji wa
kura.
Amkumbuke Augustino Mrema na mikutano yake alipokuwa NCCR –
Mageuzi, na pia mikutano ya kampeni ya CCM kule Pemba ilivyokuwa ikijaza
watu wengi mno, lakini matokeo ya kura baadaye ni tofauti.
Namkumbusha pia juu ya ‘tabia mpya’ ya wapigakura
wa Tanzania pale wanapoamua kumpa kura za kutosha mgombea wa ubunge wa
chama fulani, lakini katika nafasi ya urais wakaamua kumpa kura za
kutosha mgombea wa chama tofauti.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI


No comments:
Post a Comment