Social Icons

Pages

Tuesday, March 17, 2015

MUSWADA WA MAHAKAMA YA KADHI NJIAPANDA

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju.
Wakati Mkutano wa 19 wa Bunge la 10 ukitarajiwa kuanza kesho mjini Dodoma, hadi sasa Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala, haijauona Muswada wa Mahakama ya Kadhi. 
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Jasson Rweikiza, akizungumza na NIPASHE kwa njia ya simu jana, alisema kamati yake haijauona muswada huo bali Katibu wa kamati alipigiwa simu na kuelezwa kuwa kuna muswada utapelekwa.
“Kama ujuavyo tunafanya kazi kwa maandishi na siyo kwa simu, kama kungekuwa na muswada huo Spika angeniandikia Mwenyekiti wa Kamati. Hadi ninavyoongea sasa sijauona na sitegemei kama kwa sasa utaletwa na kuufanyia kazi,” alisema.
Kauli ya Mwenyekiti huyo inakuja huku kukiwa na ahadi ya serikali kwa muswada huo kuwasilishwa bungeni, huku Jukwaa la Wakristo Tanzania, likipinga kwa kuwa hauhusiani na masuala ya kiserikali.
Makundi ya dini za Kiislamu na Kikristo kwa nyakati tofauti yametoa kauli za kudai kuhamasisha waumini wao kutoipigia kura Katiba pendekezwa iwapo suala hilo halitakwenda kwa jinsi pande zinavyotaka.
 
KAULI YA MWANASHERIA MKUU 
Mwezi uliopita Mwanasheria Mkuu wa serikali, George Masaju, alivieleza vyombo vya habari kuwa Mahakama ya Kadhi haitakuwa na athari yoyote hasi nchini. Alisema tatizo lililopo ni kwamba serikali haijachukua hatua madhubuti kuwaelimisha wananchi namna ambavyo mahakama hiyo itakuwa inaendesha kazi zake.
“Suala la Mahakama ya Kadhi limekuwapo tangu zamani na ilikuwa ahadi za Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, serikali hatuoni kwa nini suala hili lisifanikiwe,” alisema.
Masaju alisema Watanzania lazima watambue kuwa Mahakama ya Kadhi itahusu mambo ya Waislamu wenyewe ambayo ni mirathi, ndoa na talaka na haihusiani kabisa na mambo mengine au watu wa dini jingine ikiwamo makosa ya jinai.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: