Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara.
Wabunge wameijia juu serikali kuhusu muswada wa
sheria ya Baraza la Vijana wa mwaka 2015, wakipinga vifungu vilivyompa
Waziri wa Vijana mamlaka ya kuteua Mwenyekiti wa Baraza hilo na wajumbe
wa bodi.
Muswada huo ambao uliwasilishwa bungeni jana na Waziri wa Habari,
Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara, vifungu
hivyo vimepingwa pia na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii
na Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni.
Akiwasilisha maoni ya Kamati hiyo jana, Mwenyekiti wake, Said
Mtanda, alisema kamati ilifanya marekebisho katika kifungu cha 4 (3),
kinachozungumzia uanachama wa vijana kwenye baraza hilo utokane na wale
waliojiunga na asasi za kiraia zilizosajiliwa na badala yake kijana
yeyote mwenye umri wa miaka 15 hadi 35, wajiunge kwa hiyari yao.
Pia, Kamati hiyo imepinga kifungu cha 5 (7) (a) kinachompa waziri
mwenye dhamana mamlaka ya kuteua Mwenyekiti wa Baraza la Vijana na
badala yake vijana kupitia Mkutano wake mkuu wamchague mwenyekiti wao. Kadhalika, kamati imependekeza pia kuwa muundo wa baraza hilo uende hadi ngazi ya Kata badala ya kuishia wilayani.
Naye msemaji wa kambi ya upinzani katika wizara hiyo, Joseph
Mbilinyi, alisema kwa mamlaka ya Waziri kutaka kuteua Mwenyekiti na
wajumbe wa bodi, serikali itakuwa inaunda shirika la umma na siyo Baraza
huru la vijana.
Mbilinyi alisema kambi hiyo baada ya kuuchambua kwa kina imebaini
kuwa serikali imeuleta kuwahadaa vijana kwa kuwa ni kipindi cha kuelekea
uchaguzi mkuu. “Kambi Rasmi ya Upinzani baada ya kuuchambua kwa kina muswada huu
tumegundua kuwa umelenga kuanzisha shirika la umma badala ya kuunda
chombo huru cha kuwaunganisha vijana nchi nzima bila ubaguzi wa
kiitikadi, rangi, kabila na tamaduni zao. Muswada huu umempa mamlaka
Waziri ya uteuzi wa viongozi na bodi ya usimamizi, huu ndio mtindo
unaotumika katika uteuzi wa wakurugenzi wakuu na wenyeviti wa mashirika
ya umma,” alisema.
Aliongeza kuwa: “Vijana wa Tanzania hawataki kuwa na shirika la umma, wanataka kuwa na baraza huru.”
Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, alisema muswada huo
haujazingatia maoni ya wadau na kwamba utaunda baraza bovu akieleza kuwa
ni afadhali lisiundwe kuliko mapendekezo ya muswada huo yapite.
Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Esther Bulaya, alipinga mamlaka ya
Waziri kuteua Mwenyekiti na wajumbe wa bodi akieleza kuwa itaondoa uhuru
wa baraza hilo. Vile vile, alitaka vijana wawe huru kujiunga badala ya kulazimishwa
kujiunga kwa kupitia kwenye asasi zilizosajiliwa kwa mujibu wa sheria
na kutaka baraza lifike hadi ngazi ya Kata.
Mbunge wa Kalenga (CCM), Godfrey Mgimwa, alitaka baraza liende hadi
ngazi ya Kata na kwamba elimu iwe ni sifa mojawapo ya mtu kuteuliwa
kuongoza baraza hilo.
Mbunge wa Nzega (CCM), Dk. Hamis Kigwangalah, naye alipinga
madaraka ya Waziri kuteua viongozi wa baraza huku mbunge wa Viti Maalum
(CUF), Kuluthumu Mchuchuli, alitaka vijana wajiunge kwa hiyari na kwa
kadi maalum kwenye baraza hilo na kwamba idadi ya wajumbe kwenye baraza
ngazi ya Mkoa na Wilaya izingatie idadi ya watu, kata na ukubwa wa eneo.
Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Margaret Sitta, alipendekeza kuwa
serikali iandae utaratibu wa kutoa mafunzo ya ufundi mbalimbali na pia
kila Halmashauri ihakikishe inatenga asilimia tano ya fedha za vijana
kila mwaka.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment