Social Icons

Pages

Monday, March 30, 2015

MSIMBANI KUFUNGWA KUPISHA UJENZI MFUMO WA MABASI YA KASI

Mamlaka ya Usimamizi wa Usafiri wa Ardhini na Majini (SUMATRA)
Mtaa wa Msimbazi, jijini Dar es Salaam, utafungwa kuanzia Jumatano wiki hii ili kupisha ujenzi wa mfumo wa mabasi yaendayo haraka. 
Taarifa kutoka wakala unaosimamia mradi huo, Dart ilisema ujenzi wa sehemu hiyo utaanza Aprili Mosi, mwaka huu na mkandarasi   mkuu,   Strabag   Internation.
Kipande hicho kinachoanzia eneo la ‘Fire’, kina umbali wa kilomita moja lakini ni moja ya maeneo muhimu kwa mfumo huo wa usafiri wa mabasi yaendayo haraka. Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyotolewa mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam, njia nyingi zinazokutana na mtaa wa Msimbazi zitafungwa moja kwa moja isipokuwa mitaa ya Lindi, Uhuru, Mafia na Swahili ambapo taa za kuongozea magari zitawekwa katika makutano ili kurahisisha upitaji wa magari.
Kutokana na ujenzi huo Wakala wa Dart kwa kukubaliana na Mamlaka ya Usimamizi wa Usafiri wa Ardhini na Majini (Sumatra) na wamiliki wa mabasi ya daladala, wamekubaliana kuwa mabasi ya abiria kutoka barabara ya Morogoro yatavuka kona ya mtaa wa Msimbazi na kukata kulia yatakapofika mtaa wa Lumumba.
Patakuwa na kituo kipya cha daladala katika mtaa wa Lumumba kabla ya makutano na mtaa ya Uhuru. Daladala zitakata kushoto katika mtaa wa Uhuru na kushoto tena barabara ya Bibi Titi na hatimaye kushoto tena  Barabara  ya  Morogoro.
Pia daladala kutoka barabara ya Kilwa zitakata kulia kuelekea barabara ya Nyerere, kisha kushoto kuelekea mtaa wa Uhuru na kisha kushoto tena kuelekea Lumumba.  Baada ya hapo mabasi hayo yatatakiwa kukata tena kulia barabara ya Nyerere na hatimaye kushoto barabara ya Gerezani.
Mabasi ya abiria kutoka Chang’ombe na Buguruni yatatokea barabara ya Uhuru na kukata kushoto mtaa wa Shaurimoyo ambapo yatakata kulia kuelekea mtaa wa Lindi na kugeuzia katika eneo la muda lililojengwa karibu na kituo cha baadaye cha mabasi yaendayo haraka cha Kariakoo. “Wakala wa Dart unaomba radhi kwa usumbufu utakaotokea kutokana na mabadiliko haya ya njia,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, wakala unategemea kuanza kutoa huduma ya mabasi kwa kipindi cha mpito kutokea Mbezi Louis kuelekea Kimara hadi Kivukoni na mabasi 76 Julai, mwaka huu. Huduma kamili inatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwaka 2016. Kwa ujumla kazi ya mfumo huo kwa awamu ya kwanza umeshakamilika kwa asilimia 90. Awamu hiyo inatarajiwa kukamilika Novemba, mwaka huu.

CHANZO: NIPASHE

No comments: