Social Icons

Pages

Wednesday, March 18, 2015

JIFUNZE KISWAHI UWAFUNZE NA WENGINE


NINGEPENDA kuwauliza wasomaji wangu  kwa nini waandishi hawazingatii maelekezo na maoni kuhusu uandishi bora yanayotoilewa  mara kwa mara kupitia gazeti hili?
Inawezekana kuwa waandishi   wanaosoma makala zangu ama hawaelewi au hawapendi kubadilika. Hata hivyo, hatutakata tamaa kwani taaluma ya saikolojia inadai kuwa wako  watu wenye vichwa vigumu kuelewa jambo na wako wepesi kukubali mabadiliko. Makala ya leo ni mwendelezo wa azma yetu ya  kuendelea kurekebisha makosa yaliyo katika magazeti kwa faida ya waandishi na wasomaji  kwa jumla.
Kwa mfano imeandikwa:
Ukiachilia mbali sakata hilo, mechi ya maafande hao  ilifana.” Katika maelezo hayo hapo juu, maneno ‘ukiachilia mbali’ yanatumika katika mazungumzo na ni mara chache tunayatumia katika uandishi . Katika Kiswahili fasaha, maneno ‘ukiachili mbali’ hayafai kutumika na badala yake tunatumia “Mbali ya sakata hilo, mechi ya maafande hao ilifana.”
“ Tulisaini kujiunga na mchakato huu mwaka 2004 wakati huo Benjamin Mkapa akiwa Rais na Jakaya Mrisho Rais wa sasa akiwa Waziri wa Mambo ya Nje.” Kwa kawaida jina la mtu linatakiwa kuwa na maneno matatu ili kumtofautisha na mtu mwingine. Jina la Rais wa Awamu ya Tatu ni Benjamin William Mkapa na Rais wa sasa ni Jakaya Mrisho Kikwete. Jambo la pili ni kuwa kwa kuwa Rais wa sasa anafahamika hatumtaji na kuanza kumwelezea yeye ni nani. Kwa hiyo maneno ‘Rais wa sasa’ hayahitajiki. Ingetakiwa kuandikwa,
“Tulisaini kujiunga na mchakato huu mwaka 2004 wakati huo Benjamin William Mkapa akiwa rais na Jakaya Mrisho Kikwete akiwa Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje.” “Wanahukumiwa kwa jinai dhidi ya binadamukatika matukio yaliyojiri baada ya Uchaguzi Mkuu wa mawaka 2007”.
Dhana inayopatikana hapa ni kwamba mwandishi alikuwa akifikiri kwa kutumia dhana  za kigeni. Kwa msomaji wa kawaida hataweza kuelewa mantiki ya sentensi hii. Katika kuandika Kiswahili fasaha, tunatumia neno jinai likifuatiwa na neno makosa. Kwa hiyo  iwe ’makosa ya jinai’ na hivyo sentensi isomeke:   “wanatuhumiwa kwa makosa ya jinai dhidi ya binadamu katika matukio yaliyojiri baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2007.” ‘Lakini nje ya hiyo ni kwamba timu bora imepoteza mchezo.”
Waandishi wengi wanadhani kuwa kuandika maneno mengi ni kuipamba lugha. Hii siyo  sahihi. Ukweli ni kuwa tunatakiwa kuandika kwa ufupi na kwa ufasaha.   Maneno  yasiyo  ya lazima yaachwe kuandikwa kwani katika  utaratibu wa uandishi bora  tunazingatia matumizi ya maneno machache inavyowezekana. Kwa hiyo kuandika, Maneno  ’Lakini nje ya hiyo ni kwamba’ hayahitajiki. Tukiandika ‘Timu bora imepoteza mchezo’ msomaji ataelewa.
“Watu wawili walikufa mkoani katika matukio mawili tofauti kufuatia kunywa pombe haramu ya gongo.” Kosa moja linaloonekana wazi ni kutokuutaja mkoa husika. Msomaji atapata shida kuufahamu mkoa husika na hivyo kupoteza lengo lako.  Pamoja na hayo kosa jingine ambalo linajitokeza sana na limeshaingia katika fikra za waandishi wengi ni ‘kufuatia’. Nilipoandika mara ya kwanza niliwafahamisha wasomaji wangu kuwa ‘kufuatia’ ni utohozi wa neno kufuata. Maana ya kufuata ni kwenda nyuma, kuandamana, ambatana, n.k. Tunasema kufuata nyayo, kuifuata sheria. Kwa hiyo kufuatia ni kwenda nyuma ya mtu au kitu. Kwa hyo siyo sahihi kusema matukio yalifuatia kunywa pombe. Badala yake tunasema ‘kutokana na  kunywa pombe.’
“Sasa katika makundi yetu, baada ya muda mchache tulifanikiwa kupata usafiri wa kutupeleka bandarini.”
Katika suala la muda, ni bora mhusika akatumia muda mfupi au muda mrefu badala ya muda mchache au muda mwingi. Kutumia neno ‘chache’ ambalo ni kielezi tunamaanisha  kidogo, adimu, pungufu, kutokea mara moja moja. "Nimewiwa kuandika makala hii kueleza mambo ya kifamilia.”
 Maana ya ‘wia’ ni kutaka kilicho chako kutoka kwa mtu mwigine au kudai. Mwandishi anasema ‘amewiwa’ kwa maana ya kusema kuwa anajihisi kama anadaiwa na wanafamilia kuandika makala. Huu ni msemo mgumu kueleweka kwa wasomaji wa kawaida ambao wengi wao ni wenye kisomo cha kawaida.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: