Wakati Taifa
likijiandaa kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, yamebainika mambo
matatu mazito ambayo yanaliweka njiapanda , hali inayosababisha viongozi
na hata wananchi kubaki na maswali lukuki wakihoji hatma ya nchi yao.Mambo hayo ambayo hadi sasa hayajulikani hatma
yake ni Katiba Inayopendekezwa, Mahakama ya Kadhi na uboreshaji wa
Daftari la Wapigakura kwa vifaa vya kielektroniki vya Biometric Voter
Registration (BVR).
Mambo hayo yamekuwa mjadala wa kitaifa kwa muda
sasa, hoja kubwa ikiwa ni endapo matukio makubwa ya kitaifa – upigaji wa
kura ya maoni kupitisha Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu wa Oktoba
yatafanyika kwa mafanikio au yanaweza kukwama na kusababisha
sintofahamu.
Uandikishaji BVR
Hoja kubwa katika eneo hili imekuwa ni iwapo kura
ya maoni ya kupitisha Katiba itafanyika Aprili 30, mwaka huu kama
ilivyopangwa, lakini Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi (NEC), Jaji Damian
Lubuva mara kadhaa amesimamia msimamo wa Serikali kuwa uandikishaji
unaendelea bila matatizo katika Mkoa wa Njombe kama ilivyopangwa.
Ukiacha upungufu unaosababisha shughuli hiyo
kuchukua muda mrefu, Jaji Lubuva amekuwa akikwepa kuzungumzia madai kuwa
Serikali haikutoa fedha za kutosha kufanikisha shughuli hiyo, lakini
juzi alikiri kuwa Tume yake ilijaribu hata kuazima vifaa hivyo Kenya na
Nigeria bila mafanikio.
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba
amekaririwa na gazeti hili jana akisema hata bajeti ya mchakato huo ya
Sh297 bilioni iliyopangwa haipo kwa kuwa katika kasma ya tume zilikutwa
Sh7.01 bilioni na fedha za maendeleo na fedha za tume hazikuonekana.
Profesa Lipumba alisema pia hata Sh144 bilioni za
kura ya maoni zilizoelezwa na Tume hazikuonekana kwenye vitabu vya
bajeti na kuwa BVR 250 zilizopo badala ya 8,000 zilizokusudiwa haziwezi
kufua dafu.
Kuhusu muda uliosalia wa siku 42 kabla ya kura ya
maoni, umeelezwa na wachambuzi kuwa hautoishi, ukilinganishwa na Kenya
iliyokuwa na BVR 15,000 na ikaandikisha wapiga kura milioni 14 kwa siku
kati ya 45 hadi 60. Kutokana na hali hiyo, kinachosubiriwa na wananchi
ni ama kuelezwa ni muujiza gani utafanyika hadi shughuli hiyo
kukamilika na kura ya maoni kupigwa bila matatizo au kuahirisha kura
hiyo hadi wakati au baada ya uchaguzi mkuu.
Mahakama ya Kadhi
Saula jipya kabisa katika mjadala wa uanzishwaji
wa Mahakama ya Kadhi inayotambuliwa na Serikali ni kesi iliyofunguliwa
Mahakama Kuu na Mwenyekiti wa DP, Mchungaji Christopher Mtikila akitaka
mahakama itamke kuwa Mahakama ya Kadhi na masuala ya Jumuiya ya Kiislamu
(OIC) ni haramu na itamke kuwa ulinzi na uhai na utu wa binadamu nchini
hauwezi kubaguliwa na Uislamu.
Kesi hiyo iliyofunguliwa siku moja kabla ya Bunge kuanza mkutano
wake wa 19 jana ambao pamoja na mambo mengine umepanga kujadili muswada
wa marekebisho ya sheria mbalimbali, unaokusudia Mahakama ya Kadhi
itambuliwe katika mfumo wa mahakama nchini, hali ambayo inaweza kubadili
upepo katika chombo hicho cha kutunga sheria.
Hata hivyo, Mkurugenzi wa Shughuli za Bunge, John
Joel alisema hadi jana chombo hicho hakikuwa na taarifa yoyote kutoka
mahakama kuhusu kesi ya Mahakama ya Kadhi. Kwa siku za karibu suala la Mahakama ya Kadhi
limeingia katika mjadala kutokana na ahadi ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda
aliyoitoa bungeni kuwa Serikali ingeleta muswada huo ili kuitambua
lakini isingewekwa katika Katiba Inayopendekezwa.
Katiba Inayopendekezwa
Katiba Inayopendekezwa ilipita katika misukosuko
mingi na imeendelea kupingwa na baadhi ya makundi ya jamii, vyama vya
siasa huku ikiungwa mkono na chama tawala na Serikali yake. Huku ikiendelea kupigiwa chapuo kupitia vyombo vya
habari, mikutano ya kisiasa ya chama tawala na baadhi ya makundi, vile
vile imeendelea kupingwa na makundi mengine, jambo ambalo ni dhahiri
limeacha mgawanyiko kitaifa.
Vyama vya upinzani chini ya umoja wao wa Katiba ya
Wananchi (Ukawa) wameweka msimamo wa kuendelea kuipinga na kujiweka
kando katika mchakato wake, huku baadhi ya viongozi wa dini wakitoa
matamko yanayoeleza msimamo wa kuipigia kura ya hapana Katiba hiyo.
Tamko la karibuni kabisa ni lile la Jukwaa la
Wakristo lililotolewa na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Baraza la
Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) na Baraza la Makanisa ya Kipentekoste
Tanzania (CPCT) lililoelekeza waumini kupiga kura ya Hapana kwa Katiba
Inayopendekezwa.
Siku chache baada ya tamko hilo, Askofu Mkuu wa
Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo aliibuka
na kupingana na tamko hilo akisema waumini waachwe waamue wenyewe aina
ya kura wanayoitaka, hivyo akaagiza tamko hilo lisambazwe na kusomwa
makanisani ili waumini waamue wenyewe cha kufanya. Hata hivyo, Ushirika wa Wachungaji wa Kipentekoste
Tanzania (PPFT), umetoa kauli yake ukionya taasisi za kidini
zinazotumia mwavuli wa dini kwa maslahi binafsi kuacha kuwaburuza katika
suala la Katiba mpya. Matamko hayo ya viongozi wa dini yameliweka Taifa
kwenye kona na kuwaacha waumini wao na hata wananchi wengine wasijue
washike lipi na waache lipi.
Kauli ya Serikali
Hata hivyo, akizungumzia matamko hayo, Kaimu Kiongozi wa
Shughuli za Serikali bungeni jana, Samuel Sitta alisema mvutano uliopo
kati ya Jukwaa la Wakristo Tanzania na Pengo kuhusu kuipigia kura ya
“Hapana” Katiba Inayopendekezwa hauwezi kubadili msimamo wa Serikali
kuhusu upigaji wa kura hiyo.
Sitta, ambaye pia ni Waziri wa Uchukuzi na
aliyekuwa mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, alisema waumini waachwe
wachague aina ya kura watakayopiga, kama viongozi hao wa dini
wamegawanyika hamna namna ya kuwafanya wawe na kauli moja.
Maoni ya wadau
Kutokana na hoja hizo zinazolibana Taifa, waziri
wa zamani wa mambo ya nje na mwanasiasa mkongwe nchini, Ibrahim Kaduma
alisema: “Sikuwa natarajia kama ipo siku viongozi wetu watawadhihaki
wananchi, kwani haiwezekani uwaambie kuwa kura ya maoni itafanyika
Aprili 30, wakati uandikishaji unavyokwenda hauridhishi, hii ni
kuwadhihaki tu.”
“Tumefanya makosa, turudi nyuma na tutumie
uandikishaji kwa daftari letu, kisha tufanye uchaguzi na Kura ya Maoni,
kwa kutumia BVR inahitaji mwaka mmoja au miwili zaidi kuhakikisha
tunaandikisha watu wote.”
Alisema, “Tatizo Serikali haipo tayari kusikiliza
ushauri kwani tulishasema huwezi kuandikisha watu wote kwa kipindi hiki
kilichobaki, lakini haikusikia, hizo mashine zikimaliza kuandikisha
zibaki hapo kwa ajili ya kuwaingiza watu wanaofikisha umri wa
kuandikishwa na mchakato huu uwe endelevu, jambo ambalo sidhani kama
litafanyika.”
Spika Mstaafu wa Bunge, Pius Msekwa alisema,
“Kutojua ukweli ni adui mkubwa, wanazungumza Katiba
hawajaisoma kuzungumzia jambo ambalo hujui ukweli wake ni tatizo,
tusizungumze jambo kama hulijui undani wake.” Akizungumzia tamko la maaskofu alisema, “Kama
Mkristo limenikwaza, sana lakini nilipata faraja na tamko la Kardinali
Pengo. Kwanini umnyime uhuru kupiga kura aipendayo, imenikwaza sana
hii.”
“Usiwaelekeze jinsi ya kupiga kura kwani
inajulikana na wanachotakiwa kukifanya ni kuwaelekeza kilichomo ndani ya
Katiba hiyo na siyo kuwaeleza kwamba kapigeni kura ya hapana, hii siyo
sahihi kwani ni watu wazima wanaweza kuamua wao wenyewe,” alisema
Msekwa.
Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi
Tanzania (Tucta), Gration Mukoba alisema nchi inapoelekea inahitajika
mtabiri wa hali ya juu atakayetabiri Tanzania ya mwaka 2016 itakuwaje. “BVR na vitambulisho vinavyotolewa na Mamlaka ya
Vitambulisho vya Taifa (Nida) havina tofauti, lakini hawa Nida wana
zaidi ya mwaka sasa na wakazi wa Dar es Salaam hawajapata wote, sasa
kweli NEC watamaliza uandikishaji kabla ya Aprili 30, hii ni ndoto.”
Akizungumzia Mahakama ya Kadhi alisema, “Hivi leo
tukiipitisha Mahakama ya Kadhi, kesho wanga nao watataka mahakama yao na
makundi mengine yatajitokeza yakitaka mahakama yao nchi iko katika
wingu zito sana,” alisema Mkoba ambaye pia ni rais wa Chama cha Walimu
Tanzania (CWT).
CHANZO: MWANANCHI
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Dk Ernest Mwasalwiba
alisema, “Mahakama ya Kadhi ina mkanganyiko kwani elimu haijatolewa vya
kutosha, mfano mtu asiyehusika nayo atafaidika nayo vipi, lakini kuna
makundi yanapingana, nani atakayeiongoza, itatoa wapi fedha za
kujiongoza haya yote yalitakiwa kutolewa ufafanuzi.”
Kuhusu BVR Dk Mwasalwiba alisema, “Muda uliobaki
ndiyo unaolalamikiwa. Suala la kupiga kura ya maoni ni la wananchi,
kwamba wapige au wasipige hilo lipo mikononi mwao.” Aliongeza, “Haya matamko nisingeungana sana nayo
kuwa upige kura ya hivi, lakini walichopaswa au wanachopaswa kukifanya
viongozi wa dini na Serikali ni kutoa elimu ya kutosha kwa wananchi
kuhusu mchakato huu.”
Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), Dk
Billy Haonga alisema, “Uwezekano wa kura ya maoni kufanyika Aprili 30 ni
mgumu kwani kama Njombe mpaka sasa hawajamaliza itakuwaje nchi nzima
kumaliza kwa kipindi hicho.” “Kinachotakiwa kufanyika sasa ni mawazo ya busara
kutumika kura ya maoni iahirishwe na uandikishaji uendelee kwa umakini
na inawezekana kabisa ukafanyika pamoja na uchaguzi mkuu siku hiyo hivyo
kwani inawezekana kabisa.”
CHANZO: MWANANCHI

No comments:
Post a Comment