Social Icons

Pages

Wednesday, March 18, 2015

JAJI MKUU KUONGOZA JOPO LA UCHUNGUZI LA UN

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mohamed Chande Othman.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Ban Ki- Moon, amemteua Jaji Mkuu wa Tanzania, Mohamed Chande Othman, kuongoza jopo la kujitegemea la  wataalam kuchunguza, na kutathmini uhalisi wa thamani ya habari mpya, zinazohusiana na kifo cha kutisha, wa marehemu Katibu Mkuu wa zamani, Dag Hammarskjold na wanachama wengine aliokuwa ameambatana nao.Uteuzi huo umefanywa na Ki- Moon juzi jijini New York, Marekani, kufuatia azimio namba 69/246 lililopitishwa na Mkutano Mkuu wa UN, uliofanyika Desemba 29, mwaka 2014. Azimio hilo lililomtaka Ki-Moon, ateue jopo la wataalamu ili kuchunguza kuibuka kwa habari mpya zinazohusiana na kifo cha katibu mkuu huyo wa zamani, kilichotokea mwaka 1961.
Wengine walioteuliwa kuwa wajumbe, ni pamoja na Kerryn Macaulay wa Australia, na Henrik Larsen wa Denmark. Jopo litafanya kazi ya kupitia na kutathmini thamani ya uhalisi wa habari zilizotolewa kwa katibu mkuu, na tume ya Hammmarskjold,  na rekodi zingine zinazohusiana, au habari zilizotolewa na nchi wanachama, au vyanzo vingine.
Jopo hilo huru la wataalamu linatarajiwa kuanza kazi yake Machi 30, na kuwakilisha ripoti yake kwa katibu mkuu, si zaidi ya Juni 30, 2015. Aidha , Azimio hilo lilizihimiza nchi wanachama kutoa rekodi zozote zilizo chini yao, zinazohusiana na tukio hilo, na kumpatia katibu mkuu habari zozote juu ya kifo cha katibu mkuu huyo wa zamani.

CHANZO: NIPASHE

No comments: