Social Icons

Pages

Monday, December 29, 2014

NYALANDU AJITOSA RASMI MBIO ZA URAIS 2015

WAZIRI wa Maliasili na Utalii na Mbunge wa Jimbo la SingidaK askazini (CCM), Lazaro Samwel Nyalandu, ambaye ametangaza rasmi kugombea nafasi ya urais katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwakani.

Mambo yamezidi kunoga katika kinyang’anyiro cha urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu kutangaza nia ya kuwania nafasi hiyo katika Uchaguzi Mkuu mwakani. Nyalandu ambaye ni Mbunge wa Singida Kaskazini alitangaza nia hiyo jana kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Ilongero, ndani ya jimbo lake la uchaguzi.
Akihitimisha fununu zilizokuwa zikimtaja miongoni mwa wanaCCM wanaotaka kukalia kiti hicho kinachoachwa na Rais Jakaya Kikwete, Nyalandu alisema baada ya kutafakari kwa muda mrefu na kujikagua kwa kina, ameona anao uwezo wa kutosha wa kupokea kijiti kutoka kwa Rais anayemaliza muda wake mwakani kwa mujibu wa Katiba.
“Kujikagua huko ni pamoja na kutafakari jinsi nilivyoweza kutekeleza ilani ya uchaguzi ya CCM katika vipindi vitatu (miaka 15) nikiwa mbunge wa Singida Kaskazini. Katika kipindi hicho cha ubunge, nimetumia zaidi ya Sh2 bilioni kuchangia miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali zikiwamo za afya, maji na barabara,” alisema Nyalandu.
Alisema wakati ukifika, Watanzania kutoka sehemu mbalimbali za nchi wakiongozwa na wakazi wengi wa Jimbo la Singida Kaskazini watamsindikiza kwenda Dodoma kuchukua fomu za kuwania urais.
Katika mkutano huo uliohudhuriwa na mamia ya wananchi wa jimbo hilo ambao ulipambwa na vikundi mbalimbali vya burudani wakiwamo waimbaji mahiri wa nyimbo za injili nchini, Rose Muhando na Christina Shusho, Waziri huyo alitoa changamoto kwa wanasiasa wanaojitokeza kila kukicha kuwania urais kuonyesha walichowafanyia Watanzania. “Watanzania waliokwishaonyesha nia ya kuwania urais mwakani, nawaomba sote tuonyeshe kazi tulizozifanya katika kuwahudumia wananchi ili waweze kutupima vizuri na kujijengea mazingira mazuri ya kuchagua rais atakayewafaa kwa kuwaletea maendeleo,” alisema.
Alikishukuru Chama Cha Mapinduzi kwa maandalizi yake mazuri ya kuhakikisha kinapata mwanachama safi, mwadilifu na mchapakazi atakayepeperusha bendera yake katika kinyang’anyiro hicho mwakani.

Wa nne kutangaza nia
Nyalandu anakuwa mwanaCCM wa nne kutangaza rasmi nia ya kuwania urais baada ya Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba na Mbunge wa Nzega, Dk Hamis Kigwangalla na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliyesema ametangaza nia kimyakimya.
Mbali na hao waliotangaza nia, wapo wanasiasa ambao wamekuwa wakitajwa kuwa miongoni mwa wanaotaka nafasi hiyo ambao ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya.
Wapo pia Mbunge wa Songea Mjini, Dk Emmanuel Nchimbi, Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Dk Mohamed Gharib Bilal na Waziri wa Sheria na Katiba, Dk Asha - Rose Migiro.
Vilevile, lipo kundi la ambao hawajatangaza nia lakini walipewa onyo na CCM kwa kuanza kampeni mapema wakiwamo mawaziri wakuu wa zamani, Edward Lowassa na Frederick Sumaye, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wasira na aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja. Makamba pia alipewa onyo.

Ukawa
Kwa upande wa upinzani, mpango unaofahamika ni Ukawa wa kusimamisha mgombea mmoja na wanaotajwa kuwa na uwezekano wa kuwania nafasi hiyo ni Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa, Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa NCCR- Mageuzi, James Mbatia na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.

Wazazi wazungumza
Baada ya Nyalandu kutangaza nia hiyo, baba yake mzazi, Samwel Nyalandu alisema amepokea kwa mikono miwili kusudio la mtoto wake kuwania nafasi nyeti ya urais kwa kuwa anao uwezo wa kumudu nafasi hiyo.
Alimtaka endapo atafanikiwa kupata nafasi hiyo na kuwa mkazi wa kwanza wa Singida kuwa rais, ahakikishe anafuata nyayo za watangulizi wake.
“Pia namwomba akifanikiwa aje kuwa karibu zaidi na wananchi. Sikio lake liwe jepesi kusikiliza kero mbalimbali zinazowakabili wananchi atakaokuwa akiwaongoza au kuwatumikia.
Mzee Nyalandu alisema mwanaye Lazaro alianza kuonyesha dalili kuwa mbele ya safari ya maisha yake atakuwa kiongozi wa watu kwani alipokuwa mdogo, alikuwa anapenda kukusanya wenzake na kuanza kuwaongoza katika mambo mengi ikiwamo michezo.
Alisema pia alipokuwa anasoma Shule ya Msingi Pohama, alikuwa akiongoza kuanzia darasa la kwanza hadi alipomaliza darasa la saba na kuwa mwanafunzi pekee kufaulu mtihani wa Taifa wa kumaliza elimu ya msingi na kujiunga na shule ya sekondari ya Kibaha ya wanafunzi wenye vipaji maalumu na baadaye Ilboru kidato cha tano na sita. Akimzungumzia waziri huyo, mkulima na mkazi wa Kijiji cha Ilongero, Eliwanja Hango alisema Nyalandu ameonyesha uwezo mkubwa katika kuwatumikia wakazi wa jimbo lake na wakati wote yupo karibu nao. Alisema kutokana na uzoefu alioupata katika kuwatumikia wakazi wa jimbo hilo na uzoefu wake wa kuzunguka dunia nzima, kazi ya urais haitampa shida ataimudu.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: