Wanawake 47 Zanzibar, wamepewa talaka na waume zao
kutokana na kushiriki kwao kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika
Oktoba 25, mwaka huu.
Wanawake hao walipewa talaka baada ya kutotii amri za waume zao
ambao waliwataka kutokwenda kupiga kura kutokana na kutofautiana kwa
itikadi za vyama.
Akizungumza na waandishi wa habari visiwani hapa mwishoni mwa wiki,
Mratibu wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (Tamwa),
Ofisi ya Zanzibar, Mzuri Issa, alisema katika uchaguzi huo ambao
ulifutwa na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (Zec), wanawake
wengi walikumbwa na udhalilishaji wa kulazimishwa kupigia kura chama
fulani kinyume na ridhaa yao.
Alisema Unguja na Pemba wanawake 47 walikatazwa kupiga kura na
walipoamua kwenda, waume zao waliwapa talaka na ndoa zao kuvunjika. Aisha Mzuri alisema wanawake wengine 24 walitishiwa kupewa talaka
ikiwa watahudhuria mikutano ya kampeni ama watapiga kura na matokeo yake
hawakwenda kupiga kura.
“Wanawake wanne waliambiwa wasipige kura na walipiga kura, lakini
hawakuachwa, mmoja kati ya hao katelekezwa baada ya kukataa amri ya
kuhudhuria mkutano wa kampeni,” alisema Mzuri. Aidha, alisema baadhi ya
kauli za viongozi pia ziliwadhalilisha baadhi ya wanawake ikiwamo
kiongozi mmoja wa juu wa chama fulani alipokuwa akihutubia mkutano wa
hadhara wa kufunga kampeni za uchaguzi huko Gombani Pemba alitoa kauli
ya kumdhalilisha mwanamke. Hata hivyo, alisema Tamwa kwa kushirikiana na
wadau mbalimbali ikiwamo kitengo cha wanawake katika Shirika la Umoja
wa Mataifa (UN Women), imetoa mafunzo kwa wanawake na wanaume 355 kutoka
vyama 20 vya siasa. Alisema wanawake 30 wamegombea nafasi za uwakilishi
majimboni na 87 udiwani.
“Ni muhimu kufahamu kuwa kati ya hao wanawake 10 nafasi za
uwakilishi sawa na asilimia 33.3 na 20 wa udiwani sawa na asilimia 22.9,
wamefaidika moja kwa moja na mafunzo yaliyotolewa,” alisema.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment