Kasi ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Rais Dk. John
Magufuli, katika kukabiliana na ukwepaji kodi na ufisadi wa fedha za
umma imechukua sura mpya baada ya kuwasimamisha vigogo kadhaa wa Mamlaka
ya Bandari (TPA) wakiwamo wateule wa waliokuwa Mawaziri wa Uchukuzi kwa
nyakati tofauti, Dk. Harrison Mwakyembe na Samuel Sitta.
Mkurugenzi Mkuu wa Bandari aliyeteuliwa na aliyekuwa Waziri wa
Uchukuzi katika ngwe ya mwisho ya Serikali ya Awamu ya Nne iliyomaliza
muda wake, Sitta, ni miongoni mwa watu waliosimamishwa kazi kwa amri ya
Rais Dk. Magufuli.
Kadhalika, Rais Magufuli alitangaza kuivunja Bodi ya Wakurugenzi ya
Mamlaka ya Bandari iliyokuwa imeteuliwa na Sitta huku ikiongozwa na
Professa Joseph Msambichaka aliyekuwa ameteuliwa kushika nafasi hiyo kwa
nyakati tofauti na Dk. Mwakyembe aliyewahi pia kuiongoza Wizara ya
Uchukuzi kabla ya kuhamishiwa Wizara ya Afrika Mashariki na pia Sitta.
Akitangaza uamuzi wa Rais Maguguli jana, Waziri Mkuu Kassim
Majaliwa, alisema vile vile kuwa ameamuru kukamatwa na kuchunguzwa kwa
baadhi ya vigogo wa mamlaka hiyo na taasisi nyingine za umma waliohusika
kufanikisha ukwepaji kodi wa makontena 2,431 ulioikosesha Serikali
mabilioni ya fedha.
Majaliwa alisema Rais Dk. Magufuli amefikia uamuzi wa kutengua
nafasi ya Massawe kutokana na utendaji mbovu wa TPA kwa muda mrefu na
pia kwa kitendo chake cha kutochukua hatua kwenye vyanzo sahihi vya
upotevu wa mapato.
“Mheshimiwa Rais Dk. Magufuli amevunja Bodi yote ya Bandari na
kutengua uteuzi wa Mwenyekiti wa Bodi ya Bandari na Mkurugenzi Mkuu wa
Bandari,” alieleza.
Alisema uamuzi huo umefikiwa baada ya ziara za kushtukiza Novemba 27, 2015 na Desemba 4, mwaka huu.
Wiki iliyopita, Majaliwa alifanya ziara ya ghafla bandarini na
kubaini kuwapo kwa makontena 349 yaliyopitishwa bila kulipiwa kodi
katika Bandari ya Dar es Salaam na kuikosesha Serikali takriban Sh.
bilioni 80, na hivyo kwa mlinganisho huo, makontena 2,431 yakadiriwa
kuikosesha Serikali mapato ya Sh. milioni 557 (takriban Sh. bilioni
560).
Majaliwa aliongeza kuwa (yeye) amewasimamisha kazi viongozi watano
wa taasisi mbalimbali za Serikali waliohusika katika kuidhinisha utoaji
wa makontena 2,387 bila kulipiwa kodi na pia watumishi nane waliokuwa
wakishughulikia makontena kwenye Bandari Kavu (ICD’s) mbalimbali jijini
Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Majaliwa, wahusika hao (wote) waliosimamishwa kazi
kwa kuhusishwa na ukwepaji kodi wa makontena 2,387 wanapaswa kukamatwa
mara moja, kuhojiwa na mwishowe waisaidie Bandari kujua kontena
zisizolipiwa kodi zilipaswa kutozwa kiasi gani.
Alisema ripoti za ukaguzi wa ndani TPA kwa kipindi kinachoishia
Julai 30, mwaka huu, zimebainisha ukwepaji kodi mkubwa ulioisababishia
serikali hasara ya mabilioni ya fedha kutokana na kontena hizo (2,387)
kuondoshwa bandarini bila kulipiwa kodi.
“Viongozi hawa hawakuwamo kwenye ripoti ya ukaguzi lakini ni
wahusika wakuu. Hawa ndiyo waliotoa ruhusa ili makontena yaende kwenye
ICDs,” alisema Majaliwa wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Majaliwa aliwataja viongozi hao kuwa ni Meneja Mapato ambaye kwa
sasa amehamishiwa Makao Makuu kitengo cha Fedha, Shaban Mngazija;
aliyekuwa Mkurugenzi wa Fedha na Mkuu wa Bandari Kavu (ICD) – ambaye
sasa amehamishiwa Makao Makuu kwa Naibu Mkurugenzi, Rajab Mdoe; Kaimu
Mkurugenzi wa Fedha, Ibin Masoud; na Meneja Bandari Msaidizi ( Fedha),
Apolonia Mosha.
Kadhalika, Waziri Mkuu aliwataja wasimamizi nane waliosimamishwa
kazi kuwa ni Happygod Naftari, Juma Zaar, Steven Naftari Mtui, Titi
Ligalwike, Lydia Prosper Kimaro, Mkango Alli, John Elisante na James
Kimwomwa ambaye alihamishiwa Mwanza lakini kuanzia sasa anasimamishwa
kazi akiwa kwenye mkoa huo.
“Bila wao kuidhinisha hakuna Kontena linaweza kutoka au kwenda
kokote. Watumishi wote hao wawe chini ya ulinzi na waisaidie polisi
kupata taarifa ya hayo makontena (2,387) ni ya nani na yana thamani
gani,” alisema Majaliwa.
Waziri Mkuu Majaliwa aliwaeleza waandishi wa habari kwamba Desemba
3, mwaka huu aliamua kurudi tena bandarini kufuatilia na kuangalia hatua
ya udhibiti wa upitishaji wa bidhaa mbalimbali kinyume cha utaratibu.
“Ziara yangu ilinipa nafasi ya kupitia hatua zote za upitishaji
mizigo ambazo pia, kwa mujibu wa taarifa ya Ukaguzi wa Ndani ya tarehe
30 Julai 2015, Mamlaka ya Bandari iligundulika kuwapo kwa mianya mingi
ya ukwepaji kodi ikiwamo makontena 2,387 yaliyopitishwa kati ya Machi –
Septemba 2014 kinyume cha utaratibu,” alisema Majaliwa.
“Vitendo hivi vinaonyesha kuwa bandari yetu hupitisha makontena
mengi bila ya kulipiwa kodi na hakuna hatua yoyote inayochukuliwa.
Serikali haitavumilia kuona watu wachache au kikundi chochote
kilichojipanga kuhujumu mifumo au kuiibia Serikali kwa namna yoyote ile
kwa manufaa ya wachache kikifanikiwa kwani bandari ni eneo muhimu ambalo
likisimamiwa vizuri, linaweza kukusanya fedha nyingi na kuchangia pato
la taifa,” alisema.
NYAYO ZA MWAKYEMBE, SITTA
Bodi iliyovunjwa na Rais Magufuli jana iliingia madarakani kufuatia
uteuzi uliofanywa Juni 2, mwaka huu na Sitta, ikiongozwa na Mwenyekiti
Profesa Joseph Msambichaka huku wajumbe wakiwa ni pamoja na aliyekuwa
Mhadhiri wa Sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Tulia Ackson
(sasa Naibu Spika wa Bunge); Mhandisi wa Ujenzi, Musa Ally Nyamsingwa;
Mtaalamu wa Manunuzi na Mjumbe wa Bodi ya Posta, Donata Mugassa na
Mkurugenzi Mkuu mstaafu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji
(Ewura), Haruna Masebu.
Wengine ni Mhandisi wa Bodi ya Wahandisi Tanzania, Gema Modu;
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Dar es Salaam, Francis Michael;
Mkurugenzi wa Mipango NSSF, Crescentius Magori na aliyekuwa Mkurugenzi
wa Masoko wa TPA, Flavian Kinunda.
Kabla ya uteuzi huo, Sitta aliivunja Bodi ya Wakurugenzi iliyokuwa
imeteuliwa na Mwakyembe Novemba 6, 2012, ikiongozwa pia na Profesa
Msambachaka huku wajumbe wake wakiwa Dk. Jabir Kuwe Bakari, John Ulanga,
Caroline Temu, Jaffer Machano, Dk. Hildebrand Shayo, Said Salum Sauko,
Mhandisi Julius Mamiro na Asha Nasoro.
Bodi hiyo ilidumu kwa miaka mitatu kabla ya kukumbana na ‘rungu’ la
Sitta, aliyeingia baada ya Mwakyembe kuteuliwa kuwa Waziri wa Afrika
Mashariki.
Awali, alipotua Wizara ya Uchukuzi, Mwakyembe aliwahamisha vituo
vya kazi watumishi 27 wa idara mbalimbali bandarini kwa tuhuma za wizi,
rushwa na utendaji mbovu na kumteua Madeni Kipande kuwa Kaimu Mkurugenzi
wa TPA, kushika nafasi ya Ephraim Mgawe, ambaye pia aliondolewa kwa
tuhuma mbalimbali na sasa anakabiliwa na kesi mahakamani.
Hata hivyo, Kipande (aliyeteuliwa na Mwakyembe), naye hakudumu kwa
muda mrefu kwani ujio wa Sitta katika Wizara ya Uchukuzi ulihusisha
mabadiliko kadhaa yaliyomuweka kando na nafasi yake kutwaliwa na Awadh
Massawe
KATIBU MKUU UCHUKUZI ATEMWA
Katika hatua nyingine, Rais Magufuli ametengua uteuzi wa Katibu
Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Shabani
Mwinjaka. Majaliwa alisema uamuzi wa rais wa kutengua uteuzi wa Katibu Mkuu Mwinjaka umeanza jana na atapangiwa kazi nyingine.
Alisema uamuzi huo ulitokana na ziara yake (Majaliwa) ya Desemba 3,
mwaka huu katika Shirika la Reli Tanzania (TRL) ambayo iligundua
matumizi mabaya ya fedha Sh. bilioni 13 nje ya utaratibu na kwamba
uchunguzi unakamilishwa.
Alisema Katibu Mkuu amesimamishwa kazi kwa sababu ya kutosimamia
kwa makini mashirika mawili ya Bandari na Reli ambayo yako chini ya
wizara yake.
“Tarehe 3 Desemba, mwaka huu, nilifanya ziara ya kushtukiza pale
TRL… nikakuta wametumia visivyo Sh. bilioni 13.5 walizopewa na Serikali.
Pia nilikuta wamekopa Sh. bilioni 3 kutoka Benki ya TIB lakini nazo
wamezitumia nje ya utaratibu. Fedha hizi zilikuwa ni za kusaidia
kuboresha miradi ya shirika lakini wao wamezitumia visivyo uchunguzi
bado unaendelea,” alisema Waziri Mkuu.
MATUKIO BANDARI DAR
Desemba 3, mwaka huu, Waziri Mkuu alimpa saa tatu Kaimu Meneja wa
Bandari, Hebel Mhanga amletee ofisini majina ya watumishi wote
waliohusika na ukwepaji kodi huo.
Pia, alimpa Meneja huyo wiki moja kuhakikisha kuwa mamlaka hiyo
inabadilisha mfumo wa utozaji malipo kutoka kwenye utumiaji wa kujaza
karatasi kwa mkono na badala yake kuweka mfumo wa malipo wa
kielektroniki (e-payment) hadi Desemba 11, 2015.
Ziara ya Majaliwa ya kwanza ilifukuzisha kazi watumishi 12 ambao
walifikishwa mahakamani kwa makosa ya uhujumu uchumi na rais alitengua
uteuzi wa Kamishana wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Rished Bade,
kwa kushindwa kuchukua hatua kwenye ukwepaji kodi katika kontena 329.
Hata hivyo, Rais alitoa muda wa siku saba kwa kampuni 43
zilizohusika na ukwepaji kodi kulipa haraka kabla hatua za kisheria
hazijachukuliwa na kampuni tatu zimelipa zaidi ya Sh. bilioni 5.
Pia, ziara ya pili ilisimamisha kazi watumishi 34 na kufanya jumla ya waliofukuzwa kazi kuwa 47.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment