Social Icons

Pages

Monday, November 09, 2015

TAHARUKI AJALI YA DK. KIJO-BISIMBA


Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk. Hellen Kijo-Bisimba, jana alipata ajali ya gari jijini Dar es Salaam na kukimbiziwa katika Hospitali ya Aga Khan ambako amelazwa.
Awali, taharuki kubwa iliibuka miongoni mwa watu mbalimbali kutokana na taarifa kusambaa kuwa mkurugenzi huyo anayefahamika na wengi kutokana na harakati mbalimbali za kupigania haki za binadamu kupata ajali mbaya, kisha kuonyeshwa picha za gari lililopinduka na kuharibika vibaya, zikielezewa kuwa ndilo alilokuwamo na kupinduka nalo.
Taarifa za awali zilidai kuwa Dk. Bisimba alipata ajali wakati akienda kanisani, chanzo kikitajwa kuwa ni gari lake kugongana na gari jingine. 
Hofu kuhusiana na ajali ya Bisimba iliongezwa na baadhi ya watu waliokuwa wakichangia kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii kwa kumpa pole huku wakikumbushia mkasa mwingine wa kukamatwa kwa wafanyakazi wa kituo chake waliokuwa wakifuatilia mwenendo wa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka kwa ridhaa ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec).   
Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Ilala, Lucas Mkondya, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema ilitokea jana asubuhi katika makutano ya barabara za Bibi Titi Mohamed na Jolly Club. “Kwa sasa nipo katika Hospitali ya Aga Khan. Ni kweli amepata ajali (Kijo Bisimba) na tutatoa taarifa zaidi kuhusu majeruhi wa ajali hiyo,” alisema Kamanda Mkondya.
Mkurugenzi wa Utetezi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu(LHRC), Harold Sungusia, aiiambia Nipashe kuwa ajali hiyo ilitokea saa 5:00 asubuhi. “Nimepata taarifa saa saba mchana na nikaamua kuja moja kwa moja hospitali ya Aga Khan, ili kuzungumza na Mkurugenzi mwenyewe na kufahamu nini kilitokea, kwa sasa naelekea hosptali,” alisema Sungusia.
 
HOSPITALINI AGA KHAN
Nipashe ilifika katika hospitali ya Aga Khan alikolazwa Dk. Bisimba na Mkurugenzi wa Fedha na Utawala wa LHRC, Ezekiel Masanja, alisema taarifa za awali zinaonyesha kuwa Dk. Bisimba amevunjika mguu, ingawa hali yake ilikuwa inaendelea kuimarika.
“Dereva wa Bisimba alikuwa anapatiwa matibabu. Naye amejeruhiwa, lakini taarifa ya awali ya daktari ni kuwa Mkurugenzi (Dk. Bisimba) amevunjika mguu, ingawa uchunguzi zaidi unaendelea,” alisema Masanja.
Alisema taarifa walizo nazo ni kwamba ajali hiyo ilitokea wakati bosi wao akielekea kanisani, baada ya gari lake kugongwa ubavuni na gari jingine lililokuwa likiendeshwa na kijana mdogo ambaye hakutajwa jina.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: