Mgombea urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Wananchi
(CUF) Maalim Seif Sharif Hamad, amesema kuwa hana wasiwasi
kuhusu ushindi wake kutokana na idadi kubwa ya kura alizopata dhidi ya
mpizani wake, Dk. Ali Mohammed Shein, katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika
Oktoba 25, mwaka huu.
Amesema kwa sasa anajihesabu kama Rais anayesubiri kuitwa na
kuapishwa na sasa yupo katika matayarisho ya kuunda serikali ili
akiapishwa asipoteze tena muda wa kufikiria kuunda serikali hiyo.
Maalim Seif aliyasema hayo wakati akizungumza na wajumbe wa mkutano
mkuu ngazi za wilaya na majimbo katika ukumbi wa Majid Kiembesamaki,
nje kidogo ya mji wa Zanzibar.
Alisema tayari dunia nzima wanamfahamu Rais aliyechaguliwa na
wananchi wa Zanzibar katika Uchaguzi Mkuu uliopita na kuwataka wanachama
wa chama hicho kuacha kusikiliza kile alichokiita propaganda za Chama
Cha Mapinduzi (CCM) zinazoeleza kurejewa kwa uchaguzi.
Alisisitiza msimamo wake kuwa hakuna sababu za kurejewa kwa
uchaguzi huo kwani ulishakamilika katika ngazi zote na washindi wa
uwakilishi na udiwani kutangazwa bila ya kuwapo malalamiko yoyote na
kwamba kinachosubiriwa hivi sasa ni kukamilika kwa kazi ya uhakiki wa
kura za urais kwa majimbo yaliyobakia na hatimaye mshindi wa uchaguzi
huo atatangazwa.
“Niwaambie wafuasi na wapenzi wa CUF tembeeni kifua mbele kutokana
na ushindi mkubwa nilioupata katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 25
mwezi uliopita,” alisema.
Maalim Seif alisema ushindi huo umeleta matumaini mapya kwa
Wazanzibari ambao wameitumia vyema haki yao ya kupiga kura na kuwachagua
viongozi wanaowataka.
Alisema hakuna namna yoyote ya kupindua maamuzi ya wananchi waliyoyafanya kupitia masanduku ya kura.
Alisema wanachokifanya Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (Zec) hivi sasa
ni kuchelewesha kukamilisha uhakiki wa kura kwa majimbo 14 yaliyobakia
na kumtangaza mshindi wa urais na hivyo kuishauri Zec kukamilisha kiazi
hiyo ili serikali mpya ianze kufanya kazi ya kuwatumikia wananchi.
Akizungumzia madai ya ongezeko la kura katika kisiwa cha Pemba,
Maalim Seif alisema hayana ukweli kwani hakuna hata kituo kimoja
kilichozidishwa wapiga kura 350 kilichopangiwa na kwamba vituo vingi
vilikuwa na wapigakura chini ya idadi hiyo.
Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi wa Mipango na Chaguzi wa
CUF, Omar Ali Sheikh, alisema licha ya ushindi wa urais, chama hicho
pia kimepata ushindi mkubwa kwa nafasi za uwakilishi na udiwani.
Sheikh alisema katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, CUF ilipata
Wawakilishi wanne na madiwani saba kwa upande wa Unguja ambapo uchaguzi
wa 2015, imefanikiwa kupata Wawakilishi tisa na madiwani 15.
Aidha alisema CCM imepoteza wodi zote tatu za udiwani katika kisiwa
cha Pemba na kuifanya ishindwe kupata mjumbe yeyote wa Baraza la
Wawakilishi, Ubunge na Udiwani.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment