Social Icons

Pages

Friday, June 05, 2015

MATIBABU YA MACHO KUTOA MACHOZI


Ni kawaida kabisa kwa mtu kutoa machozi kwa wingi katika kipindi cha muda mfupi hususan unapokua unapitia mambo fulani ya kihisia, mfano misiba au masikitiko pamoja na matukio ya kawaida ya mwili kama kucheka au kupiga miayo.
Zaidi ya sababu za kawaida kama nilizotaja hapo juu sababu zisizo za kawaida zinazoweza sababisha mtu akatokwa na machozi kuliko kawaida. Sababu zinazoweza kuchangia hayo ukavu wa macho. Hii ndiyo sababu kubwa zaidi ya tatizo la kutokwa machozi kwa wingi.
Macho yakiwa makavu sana mfumo wa utengenezaji wa machozi huanza kutengeneza machozi kwa wingi.
Utengenezaji huu wa machozi kwa wingi na kwa haraka mara nyingi huishia kuzalisha machozi yenye upungufu hivyo kusababisha uratibu wa namna ambavyo machozi haya yatakaa kwenye macho kuvurugika. Hii husababisha mzunguko usioisha wa utengenezaji wa machozi kwa wingi na uondoaji wa machozi haya haraka zaidi.
Mambo yanayochochea uzalishaji wa machozi ni hali ya hewa kama vile upepo mkali au jua kali, macho kufanya kazi sana kwa mfano kuangalia kitu kwa muda mrefu kama vile runinga au kompyuta na kuziba kwa matundu maalum ya kuondoa machozi kunakoweza kutokana na kujaa uchafu kwa kuumia.
Mambo mengine ni macho kuangalia kwenye mwanga mkali, kupulizwa na upepo mkali, kuumwa mafua, mzio, maradhi yanayosababisha macho kuvimba na tatizo ya maumbile kwenye kope.
Mambo mengine pia ni matatizo ya maumbile kwenye nyusi, kuumwa kwa macho, kitu kikiingia machoni kama vile chafu au mchanga, maatumizi ya dawa zenye madhara na matibabu ya maradhi ya saratani.
Mara nyingi hali hii hutokea kwa muda mfupi na baadaye huisha yenyewe hususan pale ambapo sababu ya tatizo inafahamika na inakwepeka.
Kama ikitokea hali ya kutokwa na machozi isipoisha katika kipindi cha muda mfupi au mwenye tatizo akishindwa kugundua sababu hasa iliyopelekea akapata tatizo hilo basi inabidi aende hospitali na aonwe na daktari mtaalamu wa macho.
Daktari wa macho atafanya vipimo na baada ya hapo atajua atoe matibabu gani.
Mara nyingi sana vyanzo vya tatizo huwa vinatambulika hivyo hata matibabu ya tatizo huwa sio magumu sana. Matibabu yanaweza kuhusisha mpaka usafishaji wa macho kwa maji safi.
Matibabu mengine huhusisha matumizi ya dawa zinazowekwa kwenye macho kama matone au hata za kumeza kama vilezile za kuua vimelea vya maradhi kama antibiotiki.
Kwa wale ambao tatizo huwa limesababishwa na kuziba kwa matundu ya kuondolea machozi kutoka kwenye macho basi wao hufanyiwa taratibu za kuweza kuzibua matundu hayo.
Namna ya kuepuka tatizo hili kwanza ni vyema kutambua kuwa macho ni muhimu na yanadhurika kwa urahisi sana. Kinachotakiwa kufanyika ni kuhakikisha unalinda macho yako dhidi ya vitu vitakavyoweza kuyadhuru.
Unaweza kufanya hivi kwa kuvaa miwani maalumu itakayokinga vitu visiweze kugusa macho. Pia, unaweza kuepuka matatizo makubwa ya macho kwa kuhakikisha unaenda hospitali haraka baada ya kuona kuna tatizo au hali isiyo ya kawaida imetokea kwenye macho yako.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: