Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na 
Maendeleo (Chadema) Tanzania Bara, John Mnyika, amewataka 
wanachama wa chama hicho wilayani Tarime kuachana na makundi 
yanayosababisha kukigawa Chama.
Akihutubia katika mkutano wa hadhara uliofanyika uwanja wa Sabasaba
 mjini Tarime na kuhudhuriwa na umati wa wananchi, Mnyika alisema kuwapo
 makundi kunasababisha Chama kugawanyika hivyo kudhoofisha nguvu zake.
Aidha, aliwapongeza wananchi wa wilaya hiyo kwa kufanikisha chama 
hicho kunyakua viti vingi katika uchaguzi wa serikali za mitaa 
uliofanyika Desemba 14, mwaka jana katika nafasi za uenyekiti wa mitaa, 
vijiji na vitongoji pamoja na wajumbe.
“Pamoja na kuwapongeza huko, lakini nawaomba wananchi mjitokeze kwa
 wingi kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapigakura muda 
utakapowadia,” alisema Mnyika.
Naye Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec), John Heche, aliwaasa
 wana-Tarime wawe na mshikamano wa kushirikiana kuleta maendeleo kwa 
kupiga vita maadui watatu ambao ni umaskini, ujinga na maradhi huku 
akichukua nafasi hiyo kujitangaza kuwania nafasi ya ubunge Jimbo la 
Tarime.
     CHANZO:
     NIPASHE
    

No comments:
Post a Comment