Social Icons

Pages

Thursday, April 23, 2015

MAALIM SEIF AWATOA HOFU WALIOJITOKEZA KUGOMBEA CUF


Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, amewataka wanachama walioomba nafasi mbali mbali ndani ya chama hicho kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa Oktoba, mwaka huu  kujenga imani na kamati za uteuzi wa wagombea.
Alisema kamati zote zilizoteuliwa kufanya kazi hiyo zitafanya kazi zake kwa umakini bila ya kujali wadhifa au umaarufu wa mgombea. Maalim Seif alieleza hayo jana katika kikao maalum cha kubadilishana mawazo na wanachama walioomba kugombea nafasi za ubunge, uwakilishi na udiwani upande wa Unguja, kilichofanyika mjini hapa.
Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, alisema kamati zilizochaguliwa zimewekewa vigezo maalum na zitafanya kazi ya kuwateua wanachama wenye moyo wa kujituma na kukitumikia chama ili kipate ushindi. Aliwapongeza wanachama wa chama hicho kwa kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi hizo, hali inayodhihirisha demokrasia ndani ya chama hicho.
Mkurugenzi wa Mipango na Uchaguzi wa CUF, Omar Ali Shehe, alisema wanachama 310 wamejitokeza kugombea uwakilishi na ubunge katika majimbo 32 ya Unguja na Pemba. Alisema hatua inayofuata sasa ni kwa wagombea hao kufanyiwa usaili, kazi inayotarajiwa kufanyika mwishoni mwa wiki hii na kwa upande wa Pemba tayari kazi hiyo imeshafanyika.
Shehe alisema kwa mara ya kwanza kufanyika kwa uchaguzi chini ya mfumo wa vyama vingi wa mwaka 1995, chama hicho kinatarajia kusimamisha wagombea wa udiwani katika wadi zote za Zanzibar, hatua inayoonesha kupevuka kwa chama hicho kisiasa.
Katika hatua nyingine, chama hicho kimesema kinatarajia kufanya mchujo wa wagombea mwezi ujao. Mchujo huo utakuwa na ushindani mkali kutokana na wanachama wengi kujitokeza kutaka kuwania nafasi hizo.
Vigogo wengi wa CUF wamepata wapinzani, ambao wanataka kuwaengua katika nafasi za uwakilishi na ubunge wanazoziwakilisha hivi sasa. Akizungumza na NIPASHE, Ofisa Uchaguzi wa CUF, Mhene Said Rashid, alisema idadi ya wanachama waliojitokeza kuomba kugombea nafasi hizo mwaka huu imeongezeka ikilinganishwa na mwaka 2010.
Alisema wanachama 559 wamejitokeza kugombea nafasi za uwakilishi na ubunge katika visiwa vya Unguja na Pemba, huku wanachama 381 wakiomba kuwania nafasi za diwani.
CHANZO: NIPASHE

No comments: