Waziri wa Mambo
ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Bernard Membe amepanga kuzishawishi
taasisi zinazohusika na uridhiaji wa Mikataba ya Ushirikiano wa Kiuchumi
na Jumuiya ya Ulaya (Epa), kuangalia masilahi ya nchi kabla ya
kuikubali kwa kuwa inanyonya.
Membe alisema jana katika Mkutano wa Rais mstaafu Benjamin Mkapa na watumishi wa wizara yake.
Alisema atazungumza na wizara na Kamati ya Viwanda
na Biashara kuhusu madhara ya mikataba hiyo kwa mustakabari wa uchumi
wa nchi.
“Tutaenda kuielimisha kamati inayohusika na masuala ya Epa na hatari ilizobeba. Hii mikataba inatunyonya na kutushusha chini na kutuacha palepale. Inabidi tumwambie Spika Anne Makinda wakati suala hili litakapowasilishwa bungeni ni lazima tuangalie mustakabari wa taifa,” alisema Membe.
“Tutaenda kuielimisha kamati inayohusika na masuala ya Epa na hatari ilizobeba. Hii mikataba inatunyonya na kutushusha chini na kutuacha palepale. Inabidi tumwambie Spika Anne Makinda wakati suala hili litakapowasilishwa bungeni ni lazima tuangalie mustakabari wa taifa,” alisema Membe.
Alisema tangu mikataba hiyo iliposainiwa na nchi
wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) Oktoba mwaka jana,
hajawahi kuiona na hajui kilichozungumzwa kwenye mikataba hiyo.
Rais Mkapa alisema licha ya kwamba EAC
ilishasaini, kuna fursa ya kurekebisha vipengele vya kinyonyaji
vilivyopo katika mikataba hiyo.
“Kutiwa saini mikataba hiyo siyo kwamba kila kitu
kimeisha. Kuna mambo yanaweza kufanyika yakiwamo kubainisha maeneo yote
ya kinyonyaji na kutafuta njia stahiki zitakazorekebisha kidogo ili iwe
na masilahi,” alisema Rais Mkapa.
Mkapa aliyewasilisha mada ya namna nchi inavyoweza
kutumia diplomasia kukuza uchumi, alisema vipengele kama kuachiana wazi
masoko na usawa katika biashara baina ya nchi za Ulaya na Afrika,
vitazidi kuzinyonya nchi maskini badala ya kukuza uchumi.
Alisema Nigeria walishakubaliana kuwa hata kama
atapita Rais wa chama tawala au upinzani hawataridhia mikataba hiyo kwa
kuwa wananyonywa katika kodi za uuzaji na uingizaji wa bidhaa.
Iwapo itapitishwa, Rais Mkapa alisema kampuni za
biashara kutoka Ulaya zitazidi kutumia mikataba kufanya biashara kwa
wingi na kuathiri kampuni za ndani ambazo hazina uwezo katika ushindani
wa kimataifa.
Rais Mkapa ambaye amekuwa mkosoaji mkubwa wa Epa
alisema kampuni ya bima ya Tanzania haiwezi kutoa bima kwa kampuni kubwa
zilizopo Ulaya.
Alisema iwapo angevaa viatu vya Serikali basi
angeimarisha mizizi katika umoja wa kikanda hasa Jumuiya ya Maendeleo ya
Kusini mwa Afrika (SADC) na EAC ili kukuza maendeleo ya siasa na uchumi
kuliko kufanya mikataba na mataifa ya Ulaya.
Aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Ubeligiji, Simon Mlay
alifichua siri kuwa mkataba huo umeng’ang’ania kuruhusu masoko na usawa
wa kibiashara ambao hautaongeza uuzaji wa bidhaa za Tanzania nje.
Alisema mkataba huo ni mbovu kwa sababu nchi haikujipanga kwenye majadiliano ya awali.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI

No comments:
Post a Comment