Social Icons

Pages

Thursday, April 23, 2015

KEBWE: MSIWAKEKETE WATOTO, MNAWAHARIBU

Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Steven Kebwe.
Jamii wilayani Serengeti imetakiwa kuachana na tabia ya kuwakeketa watoto wa kike kwani kufanya hivyo kunawaharibia maumbile yao ya kiasili na kuwapotezea thamani kwenye tendo la ndoa.
Akizungumza katika kituo cha kuwahifadhi wasichana waliotoroka kukeketwa toka kwa wazazi wao, Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Steven Kebwe (pichani), alisema kitendo cha kumkeketa mtoto wa kike huharibu umbile la kiungo chake na kupoteza hamu ya tendo la ndoa.
Alisema kitendo cha baadhi ya wazazi kuwaozesha watoto wa kike wakiwa na umri mdogo, hakiwezi kuvumiliwa na serikali, hivyo kutoa agizo kwa viongozi kuwashughulikia kisheria wale watakaobainika kufanya hivyo.
Wasichana hao kwa sasa wamehifadhiwa katika kituo kilichopo Wilaya ya Serengeti na kusimamiwa na Kanisa  la Anglikana Dayosisi ya Mara.
Dk. Kebwe ambaye pia ni Mbunge wa Serengeti, alisema kitendo cha ukeketaji ni ukatili wa kijinsia ambao hauwezi kuvumiliwa na wakunga wanaoendekeza mila na desturi hiyo potofu, watashughulikiwa.
Alisema suala la kuwaozesha wasichana wadogo ni sehemu ya ukatili kwa sababu hawana viungo vya asili ambavyo havina uwezo wa kuhimili tendo la ndoa ipasavyo hasa anapopata ujauzito. “Serikali haiwezi kuvumilia vitendo hivyo viendelee kwa mtoto wa kike, ni ukatili wa hali ya juu kumkeketa mwanamke kwani unaharibu umbile lake la asili hasa kuwapa shida pale wanapoolewa wakiwa na umri mdogo wanashindwa kufaidi mapenzi zaidi ya kupata maumivu,” alisema.
Kutokana na  kanisa hilo kuwahifadhi wasichana hao waliogoma kukeketwa, Dk. Kebwe alikabidhi baiskeli 48 zenye thamani ya Sh. milioni 7.2 kwa lengo la kuielimisha jamii kuachana na vitendo vya ukeketaji na uozeshaji wasichana walio na umri mdogo. Naye Mratibu wa mpango wa ‘Serengeti tunaweza bila ukatili wa kijinsia na maambukizi ya virusi vya Ukimwi’, Rhobi Samwel, alishukuru kwa msaada huo ambao utasaidia wasichana 34 wanaotunzwa na kituo hicho.

CHANZO: NIPASHE

No comments: