Social Icons

Pages

Friday, April 10, 2015

DAR YAONGOZA KUWA NA WAPIGA KURA WENGI

Mkurugenzi Mkuu wa NBS, Dk. Albina Chuwa.
Jiji la Dar es Salaam linaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya wananchi wenye sifa ya kupiga kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, kwa kuwa na watu 2,932,930.
Ripoti ya makadirio ya idadi ya watu na wapiga kura kwa mwaka 2015 iliyowekwa kwenye mtandao wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), iliyoonyesha idadi ya watu watakao kuwa na sifa ya kupiga kura mwaka huu kimajimbo na kitaifa kuwa ni watu 24,253,541.
Taarifa hiyo ilisainiwa na Mkurugenzi Mkuu wa NBS, Dk. Albina Chuwa (pichani), na Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dk. Mohamed Hafidh Rajab. Taarifa hiyo imeeleza majiji yanayofuata ni ya Mbeya lenye watu wenye sifa ya kupiga kura 1,477,365, Mwanza 1,403,743 na Morogoro 1,264,829 huku mikoa mitatu yenye wapiga kura wachache kwa Tanzania Bara ikiwa ni Rukwa 472,796, Njombe 392,634 na Katavi 271,160.
Kwa upande wa Zanzibar mkoa wenye wapiga kura wengi ni Mjini Magharibi wenye watu wenye sifa ya kupiga kura 346,524 na wenye wapiga kura wachache ni Kusini Unguja 63,546. Pia, imeeleza kuwa hadi kufika siku ya uchaguzi mkuu, Tanzania itakuwa na watu wapatao 48,522,228, ikiwa ni watu 47,110,506 wa Tanzania Bara na 1,411,722 wa Zanzibar.
Taarifa hiyo imeainisha kuwa idadi ya wenye sifa ya kupiga kura kati ya hao kwa Tanzania Bara ni 23,533,050 na Zanzibar ni 720,491. Taarifa hiyo imeanisha majimbo ya Tanzania bara ni 189, Zanzibar ikiwa na majimbo 50, huku kwa Tanzania Bara mikoa inayoongoza kwa majimbo mengi na idadi kwenye mabano ni Tanga (11), Mbeya (11), Morogoro (10) na mingine ikiwa na majimbo chini ya kumi, na wenye majimbo machache ni Katavi ambayo ni matatu.
Upande wa Zanzibar mkoa wenye majimbo mengi ni Mjini Magharibi majimbo 19 na Kusini Unguja majimbo matano. Taarifa hiyo imebainisha kuwa makadirio ya idadi ya wapiga kura yametokana na Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012 kwa kutumia mbinu za kidemografia zinazohusisha mabadiliko katika viwango vya uzazi, vifo, uhamaji na uhamiaji katika ngazi ya Taifa, mkoa, wilaya, majimbo ya uchaguzi na kata au Shehia husika.

CHANZO: NIPASHE

No comments: