Social Icons

Pages

Friday, March 13, 2015

WABUNGE WAILAUMU SERIKALI MGOGORO EFD

Naibu Waziri wa Fedha, Adam Malima.
Wabunge wameilaumu serikali wakisema ndio inayofuga mgogoro kati ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na wafanyabiashara kuhusu matumizi ya mashine za kodi zinazotumia mfumo wa kisasa wa kielektroniki (EFD).
Lawama hizo zilitolewa kutokana na kushindwa kuitisha kikao cha kamati ya majadiliano ya kushughulikia kero zote za kodi wanazotozwa wafanyabiashara kupitia EDF kwa zaidi ya miezi sita tangu iundwe na Waziri wa Fedha Saada Salum Mkuya.
Pia wamelalamika namna mapato ya serikali yanavyopotea kwa kuhoji kampuni ya Home Shopping Center (HSP) inakopata nguvu za kulazimisha wafanyabiashara kutumia wakala zake pekee kuingiza kontena, ambazo hutozwa kodi ndogo tofauti na thamani halisi ya mzigo na bila kupewa stakabadhi.
Walitoa malalamiko hayo katika kikao kati ya Kamati ya Bunge ya Uchumi, Viwanda na Biashara, uongozi wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania, watendaji wa TRA na wa wizara hiyo, walioongozwa na Naibu Waziri wa Fedha, Adam Malima (uchumi na fedha).
Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Luhaga Mpina, alimweleza Kamishna Mkuu wa TRA, Rished Bade, kwamba hakuna mtu mwingine anayepaswa kulalamikiwa kuhusu kuendelea kwa mgogoro huo kutokana na kuchelewesha kuitishwa kwa kikao cha kamati hiyo tangu iundwe Oktoba, mwaka jana, isipokuwa TRA.
Akijibu hoja hiyo, Bade alikiri kasoro hiyo na Malima akaahidi kuwa kikao hicho sasa kitafanyika ndani ya siku 14 kuanzia sasa. Kamishna wa Mapato wa Wizara hiyo, Shogholo Msangi, alisema Februari 18, mwaka huu, walikutana na wasambazaji wa mashine hizo, ambao walitumia fursa hiyo kueleza matatizo yaliyopo, ikiwamo ubovu wa mitandao na karatasi zinazotumika.
Mbali na Mpina, ambaye ni Mbunge wa Kisesa, wabunge wengine walioilalamikia serikali kuhusiana na kuendelea kwa mgogoro huo na mfumo mbovu wa ukusanyaji wa kodi, ni Khatib Haji (Konde), Josephine Genzabuke (Viti Maalumu) na Juma Ngwali (Ziwani).

CHANZO: NIPASHE

No comments: