Social Icons

Pages

Wednesday, March 18, 2015

WABUNGE SASA WAHOJI KUHUSU DAWA ZA KULEVYA

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Ummy Mwalimu.
Wakati Tanzania ikitajwa kuwa kichochoro cha kupitishia dawa za kulevya, wabunge wamehoji dawa hizo zinazokamatwa kama ushahidi zimekuwa zikipelekwa wapi kwa kuwa haionyeshi kama zimekuwa zikichomwa moto au la hali inayotia shaka udhibiti wa biashara hiyo.
Mbunge wa Viti Maalum, Rukia Ahmed, akiuliza swali la nyongeza jana bungeni, alisema kumekuwa na ucheleweshaji wa kesi za dawa za kulevya licha ya mtuhumiwa kukutwa na dawa hizo tumboni na pia zilizokamatwa haionyeshi zinapelekwa wapi.
Alisema kesi nyingi za mauaji na dawa za kulevya zinachukua muda mrefu kumalizika mahakamani na kusababisha watuhumiwa kukaa zaidi ya miaka saba rumande na kuhoji kwa nini muda wanaokaa rumande usijumuishwe kama sehemu ya hukumu wanapotiwa hatiani. Mbunge wa Karagwe (CCM), Gosbert Blandess, alihoji lini serikali itaanzisha mahakama maalum kwa ajili ya kushughulikia kesi za dawa za kulevya na rushwa kama njia ya kudhibiti tatizo hilo.
Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Ummy Mwalimu , alisema mahakama inaendeshwa kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za nchi, hivyo suala la hukumu pamoja na kipindi cha mshtakiwa kutumikia kifungo chake hufanyika kulingana na sheria inavyotamka kuhusu adhabu ya kosa husika.
Kuhusu zinapopelekwa dawa za kulevya zinazokamatwa, alisema kiutaratibu vidhibiti havirudishwi na hukumu ikishatolewa vinateketezwa.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: