Social Icons

Pages

Tuesday, March 17, 2015

UVCCM: HATUMBEBI MTU YEYOTE URAIS 2015

Katibu Mkuu wa UVCCM, Sixtus Mapunda.
Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umesema haumbebi mtu yeyote anayetaka kugombea urais miongoni mwa wanaotajwa kutaka kuwania nafasi hiyo ndani ya chama hicho katika uchaguzi mkuu ujao.
Katibu Mkuu wa UVCCM, Sixtus Mapunda, akizungumza na NIPASHE jana, alisema kwa sasa hakuna mtu yeyote, ambaye ameshachukua fomu ya kuwania nafasi hiyo, hivyo umoja huo hauna mgombea wanayemuunga mkono zaidi ya yule, ambaye atapitishwa na chama muda utakapofika.

“Mgombea yupi? Hawa unaosikia wanatangaza nia tuna uhakika gani kama watagombea? Na wakija kusema walikuwa wanatania? Chama hakijapitisha yeyote kugombea nafasi ya urais. Hivyo, sisi hatuna mgombea zaidi ya atakayeteuliwa na chama,” alisema Mapunda.
Kuhusu baadhi ya vijana wa vyuo vikuu na walioanza kueleza msimamo wao juu ya viongozi na makada waliojitangaza, Mapunda alisema hawezi kuelezea msimamo wa mtu mmoja mmoja, kwani sheria na kanuni za chama hicho zitawabana. Alisema kila kijana ana uhuru wa kumpigia kura kiongozi anayemuhitaji, lakini kama UVCCM wana wajibu wa kusimamia msimamo wa chama juu ya kiongozi atakayesimamishwa.
“Hatuwezi kumzuia mtu kusema, lakini tuna uhakika gani hao viongozi wa vyuo walioeleza msimamo wao kama ni wa UVCCM? Hata kama watakuwa wamesema, kanuni na taratibu za chama ziko wazi na msimamo wetu uko wazi. Tuna wajibu wa kumsimamia kiongozi aliyepitishwa na chama,” alisema Mapunda.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: