Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose Migiro.
Wakati Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ikisema
kukamilika kwa uandikishaji wa wapigakura katika Daftari la Kudumu la
Wapigakura ndiko kutakakotoa mwelekeo wa ama kupigwa kura ya maoni au
la, serikali imesema bado msimamo wake kwamba, kura hiyo itapigwa Aprili
30, mwaka huu.
Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose Migiro (pichani), alisema
hawezi kupiga ramli kujua ya siri kama kura hiyo, ambayo itatoa fursa
kwa wananchi kuamua ama kuikubali au kuikataa katiba inayopendekezwa,
itapigwa tarehe hiyo au la.
Alisema hayo alipokuwa akijibu maswali ya waandishi wa habari baada
ya kukabidhi nakala ya katiba inayopendekezwa kwa wawakilishi wa
serikali, binafsi, kidini na kiraia, jijini Dar es Salaam jana. Alisema chombo chenye majibu ya kama kura hiyo itapigwa katika
tarehe hiyo au la, ni Nec na kwamba, yeye hawezi kufanya kazi ya
kuijibia suala hilo.
“Tume ya Taifa ya Uchaguzi inafanya kazi yake hivi sasa, kwa hiyo
nisingependa kupiga ramli. Tunachojua kura ya maoni itafanyika tarehe 30
Aprili, nisingependa nijibu kwa niaba ya tume,” alisema Dk. Migiro. Awali, akikabidhi nakala ya katiba inayopendekezwa kwa wawakilishi
wa asasi hizo, Dk. Migiro alisema siyo kitabu cha riwaya, bali ni waraka
unaotakiwa kusomwa kwa vikundi.
Alisema jana ilikuwa ni hatua ya pili ya kusambaza katiba hiyo
baada ya kukamilisha hatua ya kwanza katika mikoa yote iliyoko Tanzania
Bara na Zanzibar, huku kila kata zilizoko Tanzania Bara ikipata nakala
300. Dk. Migiro alisema wiki kadhaa zilizopita walikamilisha uchapishaji
na usambazaji wa nakala takriban milioni mbili za katiba hiyo na
kwamba, Tanzania Bara nakala 1,141,300 zilisambazwa chini ya uratibu wa
uongozi wa serikali wilaya na mkoa, huku nakala 658,700 zilizobaki
zikikusudiwa kusambazwa kwa wizara, taasisi za serikali, asasi za
kiraia, kidini na makundi mbalimbali ya kijamii.
Alisema Zanzibar zimepelekwa nakala 200,000, ambazo zitasambazwa mikoa yote chini ya ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais. Waziri Migiro akisema hayo, Mwenyekiti wa Nec, Jaji Damian Lubuva,
alisema kinachoangaliwa na kufanyika kwa ukaribu ni uandikishaji wa
wapigakura.
“Kura ya maoni itategemea uboreshaji wa daftari la wapigakura, kama
tarehe itafika na haujakamilika tutawajulisha umma wa Watanzania.
Uboreshaji wa daftari ndicho cha kwanza halafu mengine yatafuata,”
alisema. Alisema hadi sasa vifaa (BVR kits) vinavyotumika mkoani Njombe ni 250 na vifaa 7,750 vipo njiani na serikali imeshavilipia.
Alipoulizwa vitawasili lini na kiasi cha fedha kilichotolewa hadi
sasa, alisema “Umma ujue kuwa serikali imetoa fedha tumeagiza vifaa vipo
njiani na wakati wowote vitawasili, na tutatoa ratiba ya uandikishaji
nchi nzima,” Kwa mujibu wa taarifa ya Nec iliyotolewa mara kwa mara imeeleza
kuwa baada ya vifaa kuwasili uandikishaji utafanyika nchi nzima
isipokuwa Zanzibar na Dar es Salaam, kutasubiri vifaa vyote na
uandikishaji utakuwa kwa wakati mmoja.
Wakati huo huo, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba, Sheria na
Utawala, imesema imeridhishwa na mwenendo wa uandikishaji wapigakura
unaoendelea mkoani Njombe. Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Jasson Rweikiza, alisema kamati yake
ilitembelea na kuona jinsi mashine zinavyofanya kazi kwa muda wa dakika
tatu, mwananchi anapata kadi ya kupigia kura.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment