Wakati Spika wa Bunge, Anne Makinda, akisema hawezi
kumtangaza Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, kuwa siyo mbunge
hadi atakapopata barua ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), Katibu Mkuu
wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibrod Slaa,
amesema bado hawajaandika barua kuiarifu Nec, kwa kuwa hilo siyo jambo
kubwa ambalo chama kinapaswa kuhangaika nalo kwa sasa.
Spika Makinda aliwaambia waandishi wa habari nje ya viwanja vya
Bunge mjini Dodoma jana kuwa ofisi yake haiwezi kufanyia kazi taarifa za
kwenye vyombo vya habari, badala yake inasubiri taarifa za kiofisi
kutoka Nec. “Hatuwezi kutangaza sasa kwa sababu hatujapata barua. Tumesikia
kwenye vyombo vya habari tu. Kwa hiyo hadi hapo tutakapopata barua ya
Nec ndipo tutakapotangaza,” alisema Spika Makinda.
Hata hivyo, alisema kwa mujibu wa sheria, chama kikimvua mbunge uanachama anapoteza ubunge wake.
LISSU: SINA TAARIFA
Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu, alisema hana taarifa
kama barua ya taarifa ya kumvua Zitto uanachama imekwishaandikwa kwa
Nec au la kwa kuwa Ofisi ya Katibu Mkuu wa chama hicho ndiyo inahusika
kuiandika.
DK. SLAA: HATUHANGAIKII ZITTO KWA SASA
Dk. Slaa alipoulizwa na NIPASHE jana, alisema hatua ya kuandika
barua hiyo itafuatia baada ya kikao cha Kamati Kuu ya Chama kuitishwa na
kufanyika. Hata hivyo, alisema suala la kuitisha kikao hicho linahitaji
mchakato na kwamba hivi sasa kuna vitu vikubwa na vyenye athari kubwa
kwa umma na siyo suala la uanachama wa Zitto ndani ya Chadema.
Alitaja vitu ambavyo Chama kinahangaika navyo kwa sasa kuwa ni pamoja na Daftari la Kudumu la Wapigakura. “Sidhani kama waandishi wa habari mnahangaika nalo hilo, kama
mnavyohangaika na suala hilo la uanachama wa Zitto,” alisema Dk. Slaa.
Kitu kingine ambacho alikitaja kuwa ni katika vitu wanavyohangaika
navyo kwa sasa kuwa ni mamilioni ya shilingi ‘yanayoteketea’ kwa ajili
ya kuandaa sherehe za ‘Wiki ya Maji.’ “Hatujaandika hiyo barua, tutaandika ratiba yetu ikituruhusu,” alisema Dk. Slaa.
Zitto alitangazwa kupoteza uanachama katika chama hicho wiki
iliyopita baada ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam
kutupilia mbali kesi yake dhidi ya Chadema iliyokuwa ikihoji uhalali wa
uanachama wake ndani ya chama hicho.
Baada ya hukumu hiyo ya Mahakama, Lissu alitangaza kuvuliwa rasmi uanachama wa Chadema. Lissu alisema Katiba ya Chadema inaeleza wazi kwamba endapo
mwanachama yeyote atakishtaki chama hicho mahakamani na iwapo
atashindwa, atakuwa amejiondoa mwenyewe kwenye Chama.
Hata hivyo, Zitto anasema kuwa yeye bado ni Mbunge na kwamba
ataendelea kufanya kazi za ubunge ikiwamo kutekeleza majukumu ya
Uenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC).
CHANZO:
NIPASHE

No comments:
Post a Comment