Social Icons

Pages

Friday, March 13, 2015

NCHI ZA AFRIKA ZAHIMIZWA KURIDHIA MKATABA

Rais wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu, Jaji Agustino Ramadhani ameziomba asasi na taasisi za kisheria na haki za binadamu kuzihimiza nchi wanachama wa Umoja wa Afrika (AU), kuridhia mkataba wa kuanzishwa kwa mahakama hiyo.
Akifungua mkutano wa jukwaa la wanasheria na wadau wa haki za binadamu barani Afrika jijini Arusha jana, Jaji Ramadhani alisema hadi sasa ni nchi 28 pekee kati ya 54 wanachama wa AU ndizo zimeridhia mkataba huo.
“Kati ya hizo, ni mataifa saba pekee yametoa azimio la kuruhusu raia wake na asasi zisizo za kiserikali kuwasilisha maombi yao mbele ya Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu,” alisema Jaji Ramadhani na kuhoji:
“Iwaje nchi 35 ziridhie Mkataba wa Rome ulioanzisha Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu, lakini zinashindwa kuridhia mkataba wa kuanzishwa kwa Mahakama yao wenyewe?
“Kama raia wa nchi za Afrika hawana fursa ya kufikisha madai yao mbele ya mahakama yao kwa sababu mataifa yao hayajaridhia mkataba wa kuwa na mahakama yao wenyewe, ni sawa na kutoa haki kwa kutumia mkono mmoja na kuichukua kwa mkono mwingine,” alisisitiza Jaji Ramadhani.
Katibu mtendaji wa jukwaa la wanasheria na wadau wa haki za binadamu, Wedi Djamba alisema jukwaa hilo litaendelea kupigania na kutetea misingi ya utawala unaojali na kulinda haki za binadamu barani Afrika.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: