Social Icons

Pages

Wednesday, March 18, 2015

NANI WA KUIWAKILISHA UKAWA URAIS 2015?



Ni takriban miezi minne sasa tangu vyama vinne vya upinzani nchini kupitia ushirikiano wao walioupa jina la Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kusaini makubaliano ya kushirikiana pamoja na kusimamisha mgombea mmoja katika chaguzi zote zijazo.
Umoja huo unaoundwa na vyama CUF, Chadema, NCCR- Mageuzi na NLD, unakabiliwa na kazi moja ngumu ya kufikia mwafaka wa kumpata mgombea urais, kabla filimbi ya uchaguzi kupulizwa. Hata hivyo, wachambuzi wa masuala ya siasa nchini wanasema kabla ya kumpata mgombea mmoja, vyama hivyo vinne, vitalazimika kufanya uamuzi katika sera zao kabla ya kuja na jibu la mgombea kutoka chama kimojawapo atakayekuwa na sifa ya kupeperusha bendera kwa niaba ya umoja huo.
Kufikia hatua hiyo, changamoto kubwa inayoukabili umoja huo ni namna ya kumpata mgombea wa urais atakayetoa upinzani mkubwa zaidi kwa mgombea wa chama tawala.

Historia ya wanaoweza kugombea
Mpaka sasa aliyekuwa mgombea wa urais katika uchaguzi wa mwaka 2010 kupitia Chadema, Dk Willibrod Slaa ndiye anayeonekana kuwa anaweza  kupata mtaji mkubwa wa kura. Matarajio haya yanahanikizwa na  takwimu za uchaguzi wa mwaka huo zinazoonyesha kuwa ndiye aliyepata kura nyingi kulinganisha na wagombea wa vyama vingine vitatu ambavyo mwaka huu vimeamua kujiunga pamoja kupitia Ukawa. Katika uchaguzi wa mwaka 2010, Dk Slaa alipata asilimia 26.34 ya kura zote na kuweka rekodi ya upinzani ikilinganishwa na wagombea wengine miongoni mwa wanaotajwa kuwania nafasi hiyo ya Ukawa waliowawahi kugombea siku za nyuma.
Kwa CUF kuna kila dalili kuwa Profesa Ibrahim Lipumba anaweza kupendekezwa kugombea kiti cha urais kupitia Ukawa. Mgombea huyu si mgeni katika chaguzi, ameshiriki tangu mwaka 1995 bila ya mafanikio.
Katika chaguzi nne zilizopita CUF kupitia Profesa Lipumba kimekuwa katika mtiririko usioridhisha wa kupanda na kushuka katika upataji wa kura za wananchi.
Katika uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi mwaka 1995,  alipata kura 418,973, sawa na  asilimia 6.43 ya kura zote na kushika nafasi ya tatu akiwa nyuma ya Benjamin Mkapa wa CCM na Augustine Mrema aliyegombea kwa tiketi ya  NCCR- Mageuzi.
Profesa Lipumba aliingia tena katika uchaguzi wa mwaka 2000 na kushika nafasi ya pili baada ya kupata kura 1,329,007 (sawa na asilimia 16.26) akiwa nyuma ya Mkapa na uchaguzi uliofuata alipata kura 1,327,125 (sawa na asilimia 11.68) kabla ya kushuka tena mwaka 2010 alipopata kura 695,667 (8.06%).
Kigogo mwingine wa Ukawa ni Mwenyekiti wa NCCR- Mageuzi, James Mbatia. Hata hivyo,  hajaonekana kuleta upinzani kwani hana historia ya kugombea urais, licha ya kuwa chama chake kimepata kusimamisha mgombea wa nafasi  mara tatu.
Ukiachilia mwaka 1995 aliposimama Augustino Mrema na kuibuka na idadi kubwa ya kura pengine kuliko mgombea yeyote wa upinzani, NCCR imewahi kuwasimamisha aliyekuwa kada na nguzo muhimu ya chama,  Marehemu Dk Sengondo Mvungi mwaka 2005 na baadaye  mwaka  2010 kikamsimamisha Hashim Rungwe. Wagombea wote hawa walipogombea urais kupitia NCCR-Mageuzi, hawakuonekana kuleta ushindani wowote wenye kukipa chama hicho mtaji wa kuanzia.
Chama kingine kilichopo kwenye umoja huo na ambacho hakina historia ya ushindani ni NLD chini ya mwenyekiti wake, Dk Emmanuel Makaidi ambaye naye ushiriki wake katika siasa si wa ushindani.
Nani anapewa nafasi Ukawa?
Tayari   wafuasi wengi  wa kambi ya upinzani nchini wanaielekeza kete yao kwa Chadema na mgombea wake aliyejizolea umaarufu  Dk Wilbroad Slaa. Miezi kadhaa iliyopita Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila alianza kumpigia chapuo Dk Slaa kuwa ni mtu anayefaa na kwamba ili kuleta ushindani Ukawa inapaswa kumsimamisha.
Kwa maoni yake, siyo kwamba viongozi au wanachama wa vyama vingine vinavyounda Ukawa hawana sifa za kuwania nafasi hiyo ya juu katika siasa nchini, bali Dk Slaa  ana nafasi kubwa kwa sababu anakubalika zaidi katika jamii na ana sifa ya ziada ya kuwa na mvuto. “Bado namwona Dk Slaa kuwa ana nafasi kubwa kuliko wenzake. Kwa vyovyote itakavyokuwa yeye anawazidi wenzake kwa kukubalika,” anasema Kafulila na kuongeza: ‘’Siyo kama wengine hawawezi, ila si kila mwenye mvuto anaweza kuongoza na wala si kila mwenye sifa anayeweza kuwa na mvuto. Pia si kila anayekubalika anaweza na siyo kila anayeweza anakubalika.’’

Kauli ya Profesa Lipumba
Profesa Lipumba anasema utaratibu wa kumpata mgombea mgombea wa Ukawa bado unaendelea na kuwa lazima atoke kwenye moja kati ya vyama vinne vinavyounda umoja huo.
Anaongeza kuwa endapo makubaliano yatakuja na uamuzi wa kumpitisha mgombea urais kutoka nje ya chama chake, yeye na chama chake watamuunga mkono yoyote atakayeteuliwa. “Tutamuunga mkono yeyote atakayechaguliwa ndani au nje ya CUF, tutafanya hivi kwasababu bila ukawa kuiondoa CCM madarakani itakuwa kazi ni ngumu,” anaeleza.

Michakato yaendelea ndani ya vyama
Wakati vyama vingine vinavyounda Ukawa, vikiendelea na mchakato wa kutafuta jina litakalopendekezwa kugombea kiti cha urais, Mwenyekiti wa Chama cha NLD, Dk Emmanuel Makaidi amesema, tayari chama chake kimeshapendekeza jina lake kuwa miongoni mwa watu watakaoshindanishwa kwenye kinyang’anyiro hicho. Chama cha NCCR-Mageuzi nacho kimeshamtangaza mgombea wake ambaye wanaamini anavyo vigezo stahiki vya kusimama kuwania nafasi hiyo nyeti nchini.
Aliyeteuliwa ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,  Dk George Kahangwa. Huyu ni msomi wa fani ya elimu hususan  katika maeneo ya uongozi, sera na mipango. “Tulikaa kwenye vikao halali vya chama na kuamua kwa pamoja kupitisha jina la Dk George Kahangwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya NCCR-Mageuzi, jambo ambalo limetufanya tuutangazie umma, anasema Mwenyekiti wa vijana wa NCCR-Mageuzi, Deo Meck.

Historia ya nyuma
Uchaguzi Mkuu wa mwakani utakuwa wa Tano chini ya Mfumo wa Vyama vingi uliorejeshwa nchini mwaka 1992. Tayari Chama cha Mapinduzi-CCM kimetoa marais wawili mfululizo baada ya kushinda chaguzi zote nne za 1995, 2000, 2005 na 2010. Wachambuzi wa masuala ya siasa wanatoa nafasi kubwa kwa upinzani kufanya vizuri katika uchaguzi huu endapo utaamua kuunganisha nguvu na kumsimamisha mgombea mmoja mwenye ushawishi na kumpigia debe dhidi ya CCM.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: