Social Icons

Pages

Tuesday, March 17, 2015

JK MGENI RASMI JUKWAA LA VIONGOZI AFRIKA, CHINA

Rais Jakaya Kikwete, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye ufunguzi wa Jukwaa la Viongozi wa Afrika na China litakalofanyika jijini Arusha kuanzia Machi 27 hadi 31, mwaka huu. Kongamano hilo ambalo limeandaliwa na Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), litahudhuriwa na nchi 43 kutoka Afrika na vyama 57 vya siasa, wafanyabiashara 32 kutoka nchi za Afrika, vijana 70 wa nchini na vijana 50 kutoka nchini China.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Sixtus Mapunda, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, alisema lengo la Jukwaa hilo ni kuimarisha mahusiano baina ya Afrika na China kwenye nyanja tofauti za kiuchumi, kijamii na kisiasa.
Alieleza kuwa pia jukwaa hilo litajadili maendeleo ya mahusiano kati ya Afrika na China, ushiriki na uhusiano wa vijana katika maendeleo  na wajibu wa asasi zisizo za kiserikali katika kukuza mahusiano na maendeleo kati ya Afrika na China. “Jukwaa hili ni la tatu kufanyika tangu lilipofanyika kwa mara ya kwanza mwaka 2011 Windhoek, Namibia na kufuatiwa na la pili la mwaka 2012 Beijing, China, hivyo sisi tumepata fursa ya kuliandaa," alisema.
Alisema pia vijana hao watapata fursa ya kubadilishana mawazo na wenzao na kuona namna ya kuzifikia fursa mbalimbali nchini na nje ya nchi. Aidha, alisema Jukwaa hilo linatarajiwa kufungwa na Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe.

CHANZO: NIPASHE

No comments: