Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kiluteri Tanzania 
(KKKT) Dayosisi ya Kusini, Isaya Mengele, amesema iwapo rasimu ya Katiba
 nayopendekezwa haitasambazwa na kuwafikia wananchi kote nchini mapema, 
atatangaza kuwahamasisha  wasiipigie kura ya maoni.
Kura ya maoni ya wananchi kuamua ama kuikubali au kuikataa rasimu 
ya katiba hiyo inatarajiwa kupigwa Aprili, mwaka huu, lakini hadi 
kufikia jana, ilikuwa haijaanza kusambazwa kwa wananchi. Askofu Mengele alisema hayo katika hafla ya kukabidhi Shule ya 
Sekondari ya Ruhuji iliyokuwa chini ya Balozi mstaafu wa Tanzania nchini
 Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Gidion Ngilangwa.
Alisema amezunguka sehemu nyingi nchini, lakini hajaona mahali ambako wananchi wanakosema kuwa wanaifahamu katiba hiyo. Askofu Mengele alisema wananchi wanatakiwa kuisoma na kuielewa ili 
wapige kura kukifanyia maamuzi kile walichokisoma na kukielewa. “Sisi kama kanisa hatutakubali kuwaruhusu wananchi kupigia kura 
katiba inayopendekezwa kama haitafikishwa kwa wananchi, kwani wanatakiwa
 kuisoma na kuielewa kabla ya kuipigia kura,” alisema Askofu Mengele.
Aliongeza: “Endapo itafika tarehe 30 mwezi wa nne, tutawaambia wananchi wasiipigie kura na wasubiri waisome kwanza.” Alisema kanisa linajiuliza itakapofika Aprili 30, mwaka huu 
wananchi watapigia kura ya ndiyo au hapana juu ya nini wakati hawajui 
kilichopo ndani ya katiba hiyo.
Kwa mujibu wa Askofu Mengele, kamwe hawawezi kukubaliana na kitu 
hicho na kwamba, watatangaza kwa umma ulimwenguni kote wajue, ikiwa ni 
pamoja na kuwakataza kupiga kura. Hata hivyo, alisema wataungana na Watanzania wote kuhakikisha 
kunakuwapo na amani wakati wote wa mchakato wa katiba na uchaguzi mkuu 
wa mwaka huu.
“Sasa mwezi Januari karibu unaisha. Uandikishaji wapigakura 
haujaanza. Muda uliopo ni mfupi kweli. Rais alikutana na maaskofu 
tukamshauri kuwa apitishe mchakato huo mpaka uchaguzi upite, lakini 
alishawishiwa na Bunge la Maalumu la Katiba na kutangaza kufanyika 
upigaji wa kura ya maoni kabla ya uchaguzi mkuu,” alisema Askofu 
Mengele.
Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Sarah Dumba, ambaye ni 
Ofisa Tarafa ya Njombe, Lilian Kembele, alisema serikali ina mpango 
mkakati wa kuhakikisha inasambaza Katiba inayopendekezwa kwa wananchi 
kabla ya muda wa kuipigia kura haujafika. Aliwataka wanasiasa kuwa makini katika kipindi hiki cha kuelekea 
kwenye mchakato wa kura ya maoni ya Katiba inayopendekezwa ili kuepuka 
kuiingiza nchi katika machafuko.
Alisema serikali haitakuwa na jinsi kama viongozi wa dini 
watawazuia wananchi kuipigia kura katiba hiyo, kwani ile ya zamani ipo. Kauli hiyo ya Askofu Mengele, imetolewa siku chache baada ya 
aliyekuwa Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji 
Joseph Warioba, kutamka kwamba hakuna uwezekano wa kura ya maoni kabla 
ya uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
Jaji Warioba alisema ameona taarifa inayoeleza kuwa kura ya maoni 
inatarajiwa kufanyika Machi, mwakani na kusema kama kuna umakini, kura 
hiyo haitawezekana kufanyika. Naye Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, amewasilisha taarifa 
kwa Katibu wa Bunge akitaka Bunge lijadili udhaifu wa katiba 
inayopendekezwa na kupitisha azimio la kuahirishwa kufanyika kwa kura ya
 maoni ya wananchi kuamua ama kuikubali au kuikataa katiba hiyo.
Pia amemtaka Rais Jakaya Kikwete kutangaza kufuta tangazo la 
serikali la kufanyika kwa kura hiyo mwishoni mwa Aprili, mwaka huu, hadi
 uchaguzi mkuu utakapofanyika. Mnyika alisema kama ambavyo Rais Kikwete alitumia sheria kutangaza 
upigaji kura hiyo, ni vema pia akafanya hivyo kuutengua kwa kuwa kuna 
udhaifu katika mchakato mzima. Alisema zimebaki siku chache kufanyika mchakato huo, lakini hadi sasa elimu kuhusiana na suala hilo haijatolewa kwa wananchi.
     CHANZO:
     NIPASHE
    

No comments:
Post a Comment