Ni janga kwa sababu watu waishio mabondeni hupoteza maisha, hupoteza 
makazi, hupoteza mali na hupoteza biashara zao, ingawa huwachukua muda 
mfupi kurejea kwenye makazi hayo mara tu mvua zinapoisha.
Kwa kawaida mvua ni neema kutokana na faida 
nyingi inazoleta kwa jamii, hasa kwa nchi maskini kama Tanzania ambazo 
hutegemea sana kilimo ambacho hakijaendelezwa sana kiasi cha kuwa cha 
kisasa kwa sehemu kubwa ya nchi.
Kwa maana hiyo, mvua ni baraka kwa kuwa ndio 
tegemeo kubwa la mafanikio katika kilimo endapo wananchi wanaelekezwa 
vyema kuhusu matumizi mazuri ya vipindi vya mvua. Faida nyingine ni kama
 maji kwa ajili ya matumizi ya kawaida, ingawa bado wananchi 
hawajaeleweshwa wala kupewa stadi za kutosha za uvunaji maji.
Pia, kwa Jiji la Dar es salaam, ni sawa kabisa 
wanaposema “watu wa Dar es Salaam wanaogopa mvua kuliko magari” kwa kuwa
 mvua ni janga, hata iwe ya saa chache kama ilivyokuwa Jumatatu.
Ni janga kwa sababu watu waishio mabondeni 
hupoteza maisha, hupoteza makazi, hupoteza mali na hupoteza biashara 
zao, ingawa huwachukua muda mfupi kurejea kwenye makazi hayo mara tu 
mvua zinapoisha.
Ni janga kwa sababu mvua zinaponyesha barabara 
nyingi hazipitiki na hivyo kusababisha foleni kubwa kwenye barabara 
zinazopitika kwa sababu magari yote hukwepa barabara mbovu na kutumia 
chache nzuri.
Lakini ni janga kubwa kwa sababu miundombinu ya 
majitaka, si tu ni mibovu, bali pia hailingani na mabadiliko makubwa 
ambayo jiji limepitia katika miaka michache ya hivi karibuni; kushamiri 
kwa majengo mengi katikati ya mji na majengo ambayo yanazuia mikondo ya 
maji kuelekea baharini isifanye kazi vizuri.
Hili ni tatizo ambalo linaonekana kuwa la kawaida 
sasa na si ajabu viongozi wetu wanaposikia mvua kubwa imenyesha, 
hufahamu kuwa baadhi ya maeneo yamefurika maji kwa sababu, kwanza, njia 
ambayo zingetumiwa na maji hayo kuelekea baharini zimebanwa kutokana na 
ujenzi holela na pili, miundombini ya majitaka inazidiwa na wingi wa 
maji yanayoongezewa na mvua.
Kwa hiyo, ni jambo ambalo linaonekana la kawaida 
kuona vinyesi vikisambaa kwenye mitaa ya katikati ya jiji baada ya mvua 
kidogo kunyesha, picha za magari yaliyokwama kwenye maji katikati ya mji
 na picha za nyumba zinazoonekana paa tu mita chache kutoka katikati ya 
jiji.
Haya huanikwa kila wakati mvua zinaponyesha na 
hatujui wala hatuoni mkakati wowote mkubwa ukichukuliwa kuhakikisha 
miundombinu ya majitaka inapanuliwa ili istahimili ongezeko la majengo 
katikati ya jiji. Haiboreshwi kuhakikisha inadhibiti uwingi wa maji 
yanayosababishwa na mvua zinazoweza kuwa kubwa kama ilivyokuwa juzi.
Hatujui kama viongozi wetu wanaguswa na matatizo 
haya, ambayo ni kero kubwa hasa kwa wananchi wa kawaida au wameshayazoea
 kwa kuwa hutokea kila mwaka na baada ya mvua kuisha husahauliwa?
Hivi hadi lini viongozi wetu wataendelea kuona 
tatizo hili la mvua linahitaji mkakati mkubwa wa kukabiliana nalo? Hivi 
ni lini viongozi wetu wataona kuwa miundombinu ya majitaka haistahimili 
ongezeko la majengo linalosababisha ongezeko la majitaka? Hivi ni lini 
wataona kuwa miundombinu ya majitaka haistahimili ongezeko la maji 
yanayoletwa na mvua?
Hivi itakuwa ni nchi gani ambayo wananchi wake 
wanaandaliwa kuzoea matatizo badala ya viongozi kushughulika kuwatatulia
 kama wanavyoahidi wakati wakitoa jasho kuomba madaraka?
Sisi tunadhani kuwa wakati huu tunajiandaa kuingia mwaka mpya, viongozi wetu waanze kuyachukia matatizo na kufikiria njia za kuwapunguzia wananchi wao kero za kila mwaka ili waanze kuishi kwa matumaini.
CHANZO: MWANANCHI
Sisi tunadhani kuwa wakati huu tunajiandaa kuingia mwaka mpya, viongozi wetu waanze kuyachukia matatizo na kufikiria njia za kuwapunguzia wananchi wao kero za kila mwaka ili waanze kuishi kwa matumaini.
CHANZO: MWANANCHI

No comments:
Post a Comment