Social Icons

Pages

Tuesday, November 18, 2014

BUNGE LARIDHIA SERIKALI KUFUTA DENI


Bunge limeridhia azimio la kufuta na kusamehe madai au hasara itokanayo na upotevu wa fedha na vifaa vya Serikali vya zaidi ya Sh10 bilioni za kipindi kilichoishia Juni 30, 2011.
Katika fedha hizo, kiasi cha Sh4.9 bilioni kilitokana na hasara ya kuharibika kwa dawa zilizoingizwa nchini kwa ajili ya kurefusha maisha ya watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi.
Hasara nyingine ni Sh4.9 bilioni iliyotokana na kuungua kwa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, hivyo kufanya hasara kubwa ya kiasi kilichoombwa kufutwa kutokana na mambo hayo mawili.
Fedha nyingine zilitokana na kupotea kwa vitabu katika shule mbalimbali nchini, ambavyo vimeshindwa kurudishwa na wanafunzi, kuharibika kwa gari moja aina ya Toyota Land Cruiser VX kutokana na kuingia maji katika lita 6,000 za mafuta ya dizeli.
Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba alisema jana kuwa Bunge limefanya uamuzi sahihi kufuta fedha hizo kwenye vitabu vya Serikali kwa kuwa hazilipiki.
“Asilimia 90 ya fedha zote tulizoomba zifutwe, inatokana na dawa zilizokwisha muda pamoja na kuungua kwa ofisi ya mkuu wa mkoa. Hii ni hasara ambayo ingeendelea kutuharibia vitabu,” alisema Nchemba.
Alisema fedha hizo hazikufanyiwa wizi bali kilichotokea ni hasara baada ya mali mbalimbali za Serikali kuharibika.
Akihitimisha hoja hiyo, Waziri wa Fedha, Saada Mkuya alisema Serikali itaangalia utaratibu mpya wa kuagiza dawa ili kuondokana na adha ya kuharibika na kuiingizia hasara Serikali.
“Pia tutaweka bima kwa mali za Serikali kupitia Shirika la Bima la Taifa (NIC),” alisema.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: