Mwenyekiti wa Taifa wa Tanzania Labour Party 
(TLP), Augustine Mrema, amesema hata kama vyama vinavyounda Umoja wa 
Katiba ya Wananchi (Ukawa) vimefanikiwa kumwangusha kwenye 
kinyang’anyiro cha ubunge katika Jimbo la Vunjo mkoani Kilimanjaro, bado
 ana nguvu ya kuendelea kuwania nafasi mbalimbali za kisiasa na wala 
hajakata tamaa ya kukisuka upya chama chake.Mrema aliangushwa katika kiti hicho na hasimu wake kisiasa, James 
Mbatia, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha NCCR-Mageuzi, 
aliyevunja rekodi ya kupata kura nyingi kwa upande wa wabunge wa 
upinzani, baada ya kuibuka na ushindi mnono wa  kura 60,187 dhidi ya 
6,416 alizoambulia Mrema (TLP) aliyekuwa akishikilia jimbo hilo huku 
mgombea wa CCM, Innocent Shirima, akipata kura 16,097.
Alikuwa akihojiwa jana na kituo kimoja cha redio mkoani Kilimanjaro
 kuhusu majaliwa yake kisiasa, baada ya yeye na chama chake kukosa 
uwakilishi kwenye Bunge na Halmashauri za Wilaya. Mbali ya kupoteza kiti
 cha ubunge, TLP haikuambulia   hata kiti kimoja cha udiwani. 
“Chama changu hakifi na wala sijakata tamaa, tutaanza moja na 
ninawaomba wanachama wa TLP watulie…Nitashirikiana na Rais ajaye 
aliyetangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), na tutakijenga chama 
chetu…Hata Dk. John Magufuli, anajua mimi ni mchapakazi na alinipigia 
debe na wananchi wakapuuza,” alisema Mrema.
Katika Mkoa wa Kilimanjaro wenye majimbo tisa ya uchaguzi, viti 
saba vya ubunge vimenyakuliwa na baadhi ya vyama vinavyounda Ukawa vya 
Chadema na NCCR-Mageuzi, huku majimbo mawili ya Mwanga na Same 
Magharibi, yakiangukia CCM.
Kwa mujibu wa matokeo hayo, Chadema iliyovuna wabunge sita na 
NCCR-Mageuzi yenye mbunge moja mkoani  Kilimanjaro, sasa zitaunda 
halmashauri tano za wilaya ambazo ni Moshi Mjini, Hai, Siha, Rombo, 
Moshi Vijijini na Vunjo; wakati CCM ikiwa imeambulia Halmashauri mbili 
za Mwanga na Same.
Majimbo hayo na idadi ya kata ambazo Chadema na NCCR-Mageuzi zitaunda halmashauri zake ni kama ifuatavyo; Moshi Mjini, Chadema imeshinda Kata 19 kati ya 21 na CCM imepata 
Kata mbili za Bondeni na Kilimanjaro, wakati Jimbo la Hai, Chadema 
imeshinda kata 16 kati ya 17, ambapo Kata moja ya Bomang’ombe ndio pekee
 haijafanya uchaguzi kutokana na mgombea wa CCM kufariki dunia wakati wa
 kampeni za uchaguzi mkuu. 
Aidha, Chadema iliyoshinda kata 27 kati ya 28 za Wilaya ya Rombo, 
ndiyo itakayounda halmashauri ya wilaya hiyo, huku NCCR-Mageuzi 
iliyoshinda kata nane, kati ya 16 na Chadema iliyoshinda viti 15 vya 
udiwani katika Jimbo la Moshi Vijijini, sasa zitaunda Halmashauri moja 
ya Wilaya ya Moshi. 
Katika Jimbo la Moshi Vijijini, CCM imeshinda kata moja tu. 
CHANZO:
     NIPASHE
    

No comments:
Post a Comment