Social Icons

Pages

Tuesday, June 02, 2015

WAKULIMA BARIADI KUACHANA NA PAMBA KUJARIBU ALIZETI, CHOROKO

Waziri wa kilimo, Chakula na Ushirika Steven Wasira.
Kutokana na matatizo mengi katika kilimo cha pamba ikiwamo kutotabirika kwa bei, baadhi ya wakulima wa zao hilo Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu wameonyesha mwelekeo wa kutaka kuhamia kilimo cha mazao ya alizeti na choroko.
Uamuzi huo unafikiwa na wakulima hao kutokana na bei iliyopangwa kwa ajili ya kununulia zao hilo kuwa ndogo ukilinganisha na gharama wanayotumia kufanyia maandalizi hadi kuvuna. Wakizungumza na NIPASHE juzi, baadhi ya wakulima wa vijiji vya Gambosi na Nyamswa wilayani humo, walisema hakuna matumaini ya bei nzuri ya pamba kutokana na kukatishwa tamaa.
“Tatizo ni bei ya pamba sisi wakulima tunapewa bei ndogo sana ndiyo maana tunaona tuhamie mazao mengine ya kibiashara kutokana na kutumia gharama kubwa lakini tunapouza tunapewa bei ndogo, hivyo kupoteza muda na kupata hasara na suala hili ndilo litakaloua zao hili,” alisema Masule Sigola, mkazi wa kijiji cha Gambosi.
Naye Katibu Mkuu Chama cha Wakulima wa Pamba Tanzania (Tacoga), George Mapanduji, alisema ushindani wa ununuzi kwa wakulima na mawakala kutaka kuwa na kilo nyingi za pamba, umechangia kutozingatiwa kwa madaraja ya pamba, hivyo kushusha ubora wa zao hilo la kimataifa na kuwa ya chini.
Alisema zamani mkulima alikuwa akichambua pamba yake na kuitenganisha safi na mafifi, kila moja inakuwa na bei yake, lakini kwa sasa hali hiyo haipo tena isipokuwa inatangazwa bei moja tu hivyo kushusha ubora wa pamba katika soko la kimataifa.

CHANZO: NIPASHE

No comments: