Social Icons

Pages

Wednesday, June 03, 2015

MPINA: RASILIMALI ZA NCHI ZITUMIKE IPASAVYO


Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina (CCM), ametangaza nia ya kugombea urais, akisema akifanikiwa kukamata dola atahakikisha anasimamia vyema rasilimali za nchi zinatumika vyema.
Mpina akihutubia katika uwanja wa shule ya msingi Mwandoya, Meatu, Simiyu, alisema ana uwezo wa kusimamaia na kuhakikisha rasilimali hususani fedha zinatumika ipasavyo. Alisema nchi ina tatizo kubwa la rushwa linalokwamisha jitihada, mikakati na mipango ya maendeleo na ustawi wa wananchi, hivyo atahakikisha wote wanaotumia fedha za umma kwa kuhifadhi benki za nje, wanachukuliwa hatua za kisheria.
“Nia kubwa ya kutaka niwe Rais, lengo ni kuipa kipaumbele serikali na kuhakikisha inakuwa na fedha za kutosha ili kukabiliana na changamoto za mapato,” alisema.
Kuhusu elimu, alisema  atahakikisha anaboresha mambo muhimu yaliyokuwa ndani ya sekta hiyo, huku akisisitiza serikali ya CCM imefanikiwa kutekeleza mikakati yenye lengo la kukuza kiwango cha elimu, hivyo jukumu la serikali yake kama akichaguliwa Rais ataondoa vizingiti vinavyosababisha taaluma hiyo kuonekana havifai.
Kuhusu uchumi, Mpina alisema atahakikisha mikataba mibovu inayosababisha mapato ya nchi kuyumba, inakaa vizuri na kulinufaisha taifa, huku akitangaza kukabiliana na wale wanaotumia mabilioni ya pesa za serikali na kushindwa kulizilipa.
Aidha, alisema atahakikisha sekta ya afya inaimarika na kutoa huduma kwa jamii ipasavyo ikiwamo kuwaweka watumishi wa taaluma katika kufanya kazi wakiwa ndani ya mazingira mazuri ili kusaidia jamii ipate huduma ya afya. “Mambo haya nitayashughulikia muda mfupi nikiingia madarakani,” alisema.
“Zaidi ya asilimia mbili ya fedha zinatoroshwa kwenda nje ya nchi na wanaohusika hawachukuliwi hatua ingawa wanafahamika, natuma salamu kwa watu hao katika serikali yangu wajiandae kuzirejesha hizo fedha walizochukua,” alisema Mpina.
Naye katibu wa CCM wilaya Maswa, Jonathan Mabiya, aliwataka wananchi kufanya uamuzi sahihi kuchagua viongozi bora wakati wa uchaguzi mkuu.

CHANZO: NIPASHE

No comments: