Mtambo wa kienyeji wa kutengenezea gongo.
Kilimanjaro
imekuwa na sifa nzuri ya uchapakazi na kuifanya kuwa na wafanyabiashara
pia wajasiriamali wengi hivyo kuchagiza maendeleo ya eneo hilo hata
Taifa.
Hata hivyo, sifa hiyo nzuri inaporomoka kutokana
na kuingia doa kwa kukumbwa na wimbi la utengenezaji, uuzwaji na unywaji
wa pombe za kienyeji ikiwamo maarufu na haramu ya gongo. Wilayani Rombo sasa kunakadiriwa kuwa na aina 52 za pombe zinazotengenezwa kienyeji bila kuzingatia ubora.
Pombe hizo zimesababisha vijana wengi kujiingiza na kuzama katika ulevi uliopindukia hivyo kupoteza nguvu kazi. Hali hiyo pia imeanza kuibadili sifa iliyokuwapo
ya kukubalika kuwa na watu wachapakazi na wajasiriamali. Mtazamo huo
umebadilika na Rombo kuanza kutazamwa kama eneo la wanywaji pombe wa
kupindukia.
Matokeo ya hivi karibuni ya Ripoti ya Utafiti wa
Ukubwa wa Matumizi ya Pombe nchini, yaliutaja Mkoa wa Kilimanjaro
kuongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya wanywaji huku Wilaya ya Rombo
ikitajwa kuongoza hasa vijana na wanaume.
Mbali na matokeo ya utafiti huo uliofanywa na
Taasisi ya Taifa ya Utafiti Magonjwa ya Binadamu (NIMR) na matokeo yake
kutangazwa Machi, unywaji uliopitiliza wa pombe haramu umeleta
mifarakano ndani ya baadhi ya familia za Wilaya ya Rombo na kuzua
malalamiko kutoka kwa wanandoa hasa kina mama, wanaodai kunyimwa
unyumba.
Hata hivyo, uchunguzi unaonyesha kuwa matumizi ya
pombe hizo yanatokana na wananchi wengi kushindwa kumudu bei ya bia
ambayo ni kati ya Sh2,200 hadi 3,500, hivyo kukimbilia pombe za kienyeji
na pombe kali (spirit). Hali hiyo ya unywaji wa pombe kupita kiasi,
inaelezwa kuwa ilianza takriban miaka 15 iliyopita, ambako pia
uzalishaji wa pombe zisizo na viwango ulianza na kudhoofisha baadhi ya
wanaume, ambao ndiyo wateja wa kubwa.
Ingawa kina mama pia wa wilayani Rombo wamekuwa
wakinywa pombe hizo, lakini hali imekuwa mbaya zaidi kwa baadhi ya
wanaume na vijana.
Mkazi wa Kijiji cha Kikelewa kilichopo Tarakea
wilayani humo, Germana Kimario anasema awali pombe haramu aina ya gongo
ilikuwapo na ilitumiwa na baadhi ya wananume lakini haikuwa na madhara
makubwa kama ilivyo sasa. Anasema tangu kuanza kuzalishwa aina hizo za pombe
katika wilaya hiyo, baadhi ya vijana na wanaume wamekuwa wakidhoofika
siku hadi siku hali inayosababisha wanawake kufanya kazi ambazo
zingefanywa na wanaume kama vile kuchimba mitaro na kubeba zege.
Germana anasema Serikali inawajibika kuangalia namna ya kudhibiti pombe hizo kwa kuwakamata na kuwafilisi wanaozizalisha. Anadokeza kuwa mara kadhaa wazalishaji pombe haramu wamekamatwa lakini waliachiwa na kuendelea na kazi yao.
Anaeleza kwamba vijana wengi katika kijiji hicho
wamegeuza pombe kuwa kama ‘wake zao’, wakisahau mambo mengi ya msingi ya
kifamilia hata yale ya ujenzi wa Taifa.
“Vijana wengi hapa Rombo wakiamka asubuhi kitu
wanachoweza ni ‘kimorali’ au ‘mbundimbundi’, hizo ni baadhi ya pombe
zinazozalishwa hapa, ambazo zimekuwa zikiharibu afya za baadhi ya
vijana.
Hali imekuwa ngumu kwa kuwa wanaume wakishaanza
kunywa pombe hizo hawawezi kufanya kazi nyingine yoyote zaidi ya kuanza
kuuza vitu vya ndani ili aweze kupata fedha za kunywa,” anasimulia mama
huyo.
Anaeleza kwamba katika kijiji hicho wanaume walio
na nguvu, wengi ni Wakenya na kwamba ndiyo wanaofanya kazi kutokana na
mwingiliano wa eneo hilo la mpaka. “Ndiyo hao pia wamekuwa wakitoa huduma ya ‘tendo
la ndoa’ kwa wanawake wa kijiji hiki kutokana na wanaume kushindwa kutoa
huduma hiyo,” anasema Germana.
Mkazi mwingine wa wilaya hiyo, Joyce Shirima
ambaye hivi karibuni amehamia Dar es Salaam anasema: “Tatizo hilo
linakuwa siku hadi siku kutokana na pombe hizo kupikwa karibu kila
nyumba katika Tarafa ya Tarakea na zinazidi kuharibu wanaume na vijana
hapa Rombo.”
Anaongeza: “Hali ilivyo sasa baadhi ya wanaume na
vijana wamekuwa wakishindwa kurudi nyumbani na kuishia kulala kwenye
mitaro kutokana na ulevi.”
Mkazi mwingine, Athanas Kimario, anasema baadhi ya
wanawake kutoka nje ya Rombo sasa hutumia mbinu ya kuolewa na wanaume
wa Rombo ili kupata makazi ya kudumu lakini baadaye hufanya mbinu ya
kupata watoto kutoka kwa mwanaume wa nchi jirani ya Kenya.
“Kuna uwezekano unywaji wa pombe hizo ukasababisha
Tarakea ikawa na watoto wenye baba zao nchi jirani kutokana na unywaji
wa hizi pombe, kwani hata ukinywa, hutamani tendo la ndoa kabisa,”
anasema Kimario na kuongeza:
“Kuna pombe nyingine wanaume wanaokunywa wanavimba
mashavu, nyingine zinaharibu mwili, kuhakikishia hilo mtu aliyekunywa
pombe hizo akikojoa kwenye majani hunyauka, hiyo inaonyesha
wanachokunywa ni sumu.
“Mimi natumia pombe hizo pia hata tendo la ndoa silitamani kwa
kuwa nikishakunywa ‘kimorali’ naishiwa nguvu kwa ulevi na siwezi
kufanya chochote, ninalala tu. Sasa mke wangu ameniacha naishi
mwenyewe.”
Padri wa Kanisa Katoliki, Kigango cha Kikelelwa,
Serafin Kilawe anasema kiwango cha ulevi katika tarafa hiyo ni kikubwa
na kwamba kimeathiri baadhi ya vijana na wanaume.
Anasema hali hiyo imesababisha wanandoa wengi hasa
wanawake kufikisha malalamiko yao kanisani wakiomba kusuluhishwa
kutokana na waume zao kushindwa kuwahudumia katika haki ya ndoa.
“Tumekuwa tukitangaza katika ibada tunazozifanya
kutaka watu waache unywaji pombe kupita kiasi, lakini hali hii imekuwa
inaendelea kuota mizizi siku hadi siku kutokana na baadhi ya viongozi wa
Serikali kugeuza maeneo yanayopika pombe hizo kuwa ‘ATM’ ya kujipatia
fedha,” anasema Padri Kilawe.
Uchunguzi wa gazeti hili unaonyesha kuwa baadhi ya
wasimamizi wa sheria wamekuwa wakiwatafuta wapika pombe na kuunga
urafiki nao hivyo kutowathibiti kutokana na wao kuchukua rushwa hali
inayoruhusu wapikaji kuendelea kutengeneza pombe hizo zinazoua nguvu
kazi ya Rombo.
“Kweli kazi za maendelo sasa zinafanywa na kina
mama kwa kuwa ndiyo wenye nguvu na wanaume kuishia kwenye pombe na
kushindwa kusaidia familia zao,” anasema Padri Kilawe na kuongeza:
“Kuna matajiri katika kijiji hiki kazi yao ni kuua
watu kwa kuwa ndiyo watengenezaji wa pombe ambazo hazina kiwango. Siasa
pia imeingia, viongozi wanaochaguliwa na wananchi hawathubutu kukemea
ulevi kwa kuhofia kutochaguliwa.
Huku Tarakea, baadhi ya viongozi wanafanya
kampeni za kuomba kura kwa kusema endapo wakichaguliwa wataruhusu
uuzwaji wa pombe pamoja na unywaji wa pombe hizo. Hali hiyo
inasikitisha, kiongozi kuongoza wananchi wasio na nguvu na kuruhusu
wanywe sumu?”
Mwenyekiti wa Kijiji cha Kikelelwa, Justine
Shirima anakiri kuwapo kwa tatizo la wanandoa kutopewa haki yao ya
msingi kutokana na ofisi yake kupokea malalamiko mengi hasa kutoka kwa
wanawake.
“Wanawake wengi wanafika ofisini kuwalalamikia
waume zao kutowatimizia tendo la ndoa kutokana na unywaji wa pombe
uliokithiri,” anasema Shirima.
Anasema baadhi ya wanawake wanapata huduma hiyo kutoka kwa wanaume wa nchi jirani kutokana na eneo hilo kuwa mpakani na Kenya.
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama
anaeleza kuwa katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC), mwaka
jana ajenda iliyotawala ilikuwa ni unywaji wa pombe uliokithiri ndani ya
mkoa na kwamba wilaya iliyokithiri ilitajwa kuwa ni Rombo.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment