Social Icons

Pages

Tuesday, May 26, 2015

WABUNGE WAHOJI WIZARA KUPEWA FEDHA KIDUCHU

Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudencia Kabaka akiwasilisha bungeni hotuba ya bajeti ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2015/2016, mjini Dodoma jana.
Mjadala wa Kikao cha 12 cha Bunge la Bajeti jana ulitawaliwa na vilio vya kamati za Bunge na wabunge kuhoji sababu za Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto kupewa fedha kidogo ya maendeleo, huku Wizara ya Kazi na Ajira ikikosa kabisa fungu kutoka Hazina.
Wamesema hali hiyo inasababisha wizara hizo kutokuwa na jipya katika kuiendeleza nchi, ikiwa ni pamoja na kumaliza tatizo la ajira nchini.
Akiwasilisha maoni ya Kamati ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii kuhusu bajeti ya Wizara ya Kazi na Ajira, mjumbe wa kamati hiyo Maua Daftali alisema katika bajeti ya mwaka 2014/15, wizara hiyo haikupewa hata shilingi moja ya fedha za maendeleo. “Bajeti ya wizara hii mwaka 2014/15 ni Sh17 bilioni, kati ya hizo Sh5.8bilioni zilikuwa kwa ajili ya kulipa mishahara, Sh8.9 bilioni kwa ajili ya matumizi mengine na Sh2.9bilioni kwa ajili ya maendeleo,” alisema.
Alifafanua kuwa hadi Aprili mwaka huu, fedha za mishahara zilizotoka ni Sh4.7bilioni, matumizi mengine zilitoka ni Sh2.6 bilioni na hakukuwa na fedha yoyote ya bajeti ya maendeleo iliyotolewa. “Kwa mantiki hii, inaonyesha hakuna kazi yoyote ya maendeleo iliyofanywa na wizara hii. Kukosekana kwa bajeti ya maendeleo maana yake ni kwamba wizara hii haina jipya katika kuindeleza nchi,” alisema Dk Daftari.
Bajeti ya wizara hiyo mwaka 2015/16 ni Sh38.8bilioni, huku Sh20bilioni zikitengwa kwa ajili ya maendeleo.
Akiwasilisha taarifa ya kamati ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii kuhusu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, mjumbe wa kamati hiyo, Agness Hokororo alisema wizara hiyo katika bajeti ya 2014/15 ilitengewa Sh8.9bilioni za maendeleo.
“Hadi Machi mwaka huu, wizara ilikuwa imepokea Sh2 bilioni sawa na asilimia 22 ya bajeti ya maendeleo. Kamati imebaini miradi ya maendeleo haikupewa kipaumbele na hii itaathiri ustawi wa shughuli za kijamii zinazosimamiwa na wizara,” alisema Hokororo.
Akiwasilisha hotuba ya Wizara ya Kazi na Ajira, waziri wake Gaudencia Kabaka alisema katika kipindi cha mwaka 2010 hadi sasa zimezalishwa ajira milioni 1.9 katika sekta ya kilimo, elimu, afya, ujenzi wa miundombinu, nishati na miradi ya kijamii pamoja na ajira milioni moja katika sekta binafsi.

Wabunge wanena
Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), Maulidah Komu alisema Serikali imeshindwa kuwasaidia watoto yatima na wale wa mitaani, badala yake imekuwa na mikakati ya muda mrefu ambayo haiwasaidii walengwa.
“Watoto yatima na mitaani wanapata tabu sana na wanaingiliwa kinyume na maumbile. Mfano kuna nyumba moja ya kuwalea ilikuwa Morogoro walikuwa wanafanyiwa kitu kibaya na Serikali haichukui hatua,” alisema.
Mbunge wa Ukonga (CCM), Eugen Mwaiposa ameitaka Serikali kuanzisha utaratibu kutoa mikopo kwa vijana wanaomaliza darasa la saba ili waweze kupata fursa ya kujiunga na vyuo vya ufundi.
Alisema vijana hao wakikosa nafasi ya kuendelea na masomo huishia vijiweni kwa sababu ya kukosa fedha ya kujiendeleza kielimu.
Kauli ya Mwaiposa iliungwa mkono na Mbunge wa Viti Maalumu (CUF), Riziki Omari Juma ambaye pamoja na mambo mengine, alitilia mkazo zaidi mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino), kuitaka Serikali iweke utaratibu wa kuwalinda badala ya kuendelea kufanya uchunguzi kusaka wauaji.
“Mbona Tembo wanalindwa sana na ikitokea ameuawa mmoja tu wahalifu wanasakwa, lakini albino akiuawa hakuna hatua zinazochukuliwa,” alihoji.
Mbunge wa Mafinga (CCM), Mendrad Kigola alisema tatizo la ajira kwa vijana limeendelea kuwa kubwa na kuitaka Serikali ianze kutoa mikopo ya pikipiki kwa sababu vijana wengi wanamaliza vyuo vikuu na kukosa ajira.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: