Tanzania imebahatika kuwa na aina nyingi ya madini ya vito vya thamani kama vile dhahabu, almasi na Tanzanite.
Wingi wa rasilimali hizo za thamani duniani
umekuwa ukiwafanya baadhi ya watu kuamini kuwa nchi ni tajiri lakini
unapoingia kwenye uhalisia, utajiri huo haulisukumi taifa kumea vizuri
kiuchumi.
Je, tatizo ni nini? Kuna mipango gani ya
kukabiliana na hali hiyo? Haya ni maswali ambayo yamekuwa yakiulizwa na
wengi na makala hii inakusudia kuyajibu.
Arusha na moja ya mikoa nchini ambao kuna
uchimbaji wa aina nyingi za madini. Moja ya madini yanayoupa sifa kubwa
mkoa huu ni madini ya Tanzanite ambayo hayapatikani eneo jingine popote
duniani.
Biashara kubwa ya madini hayo ipo katika Jiji la
Arusha na kuna mitaa, ambayo ni kawaida kukuta vijana, wakiwa wamekaa
kando ya barabara wakichonga madini na kuuza. Mitaa hiyo ipo katikati ya
Jiji la Arusha kama vile Barabara ya Pangani, jengo la Chama cha
Wafanyakazi Arusha (Ottu) na Mtaa wa St Thomas.
Katika mitaa hii, utakuta vijana wengi wakiwa na
viti na meza ndogo wakichonga madini na wengine wakiuza. Mbali na
Tanzanite, pia kuna aina nyingine madini kama vile saphire, spinel,
tourmaline, sperssatite na aquamarine. Miongoni mwa madini hayo yapo
yanayochimbwa mikoa ya jirani.
Kuuzwa holela kwa madini kunatajwa ndiyo
kunasababisha madini mengi kutoroshwa na kuvuka mipaka kuingia nchi
mbalimbali ambazo huziuza kwenye soko la dunia. Aina hii ya biashara
hulikosesha taifa mapato na isitoshe hata wachimbaji na wafanyabiashara
hiyo hapa nchini hupata faida kidogo tofauti na ingekuwa wangepeleka
wenyewe kwenye soko la dunia.
Kwa mfano ripoti ya mwaka 2013 inaonyesha kuwa
uuzaji wa madini ya Tanzanite uliingizia Tanzania Dola 38 tu za Marekani
huku nchi zinazopata madini hayo kwa njia ya panya, zikijipatia mapato
makubwa. Kulingana na ripoti hiyo, katika mwaka huo, Tanzanite
iliingizia Kenya Dola 100 milioni na India Dola 300 milioni.
Tanzania yazinduka
Kwa kutambua namna inavyopoteza mapato na nchi
kutofaidika kikamilifu na madini yake, Serikali imeamua kuweka mkakati
ambao utaziba mianya ya utoroshaji wa madini nchini. Ili kuifanya
biashara ya madini ya vito, kutambulika kisheria na kuinufaisha Serikali
katika kukusanya kodi mipango imeanza kujengwa kituo cha kukata,
kusanifu na kuuza madini Arusha.
Kituo hiki, kinakuwa cha kimataifa, ambacho
kitakusanya wafanyabiashara wa madini ya Tanzanite wa ndani na nje ya
nchi kukaa pamoja kufanya biashara halali.
Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene
anasema kituo hiki, kitajengwa na Serikali kwa kushirikiana na Kituo cha
Mikutano cha Arusha (AICC). “Katika kituo hiki, kutakuwa na maduka ya kununua na kuuza
madini, ofisi za mamlaka ya kodi (TRA), ofisi za madini na eneo la
kukata na kusanifu madini,” anasema.
Wadau wanasemaje?
Lengo la Serikali kuja na mpango huo, ni
kuhakikisha madini yanayopatikana nchini, yanalinufaisha Taifa pia
kunakuwapo masoko ya uhakika. “Hatutaki biashara ya utoroshaji wa madini
pia kuuzwa nje yakiwa ghafi,” anasema.
Wakati Serikali ikiweka mikakati hiyo, Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA) nao unaweka udhibiti kwenye viwanja vya ndege kuhakikisha hakuna madini yanayotoroshwa nje ya nchi kimagendo.
Wakati Serikali ikiweka mikakati hiyo, Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA) nao unaweka udhibiti kwenye viwanja vya ndege kuhakikisha hakuna madini yanayotoroshwa nje ya nchi kimagendo.
Mkurugenzi wa Fedha na Utawala wa TMAA, Bruno
Mteta anasema: “Kwa kipindi cha kuanzia Januari mpaka Desemba mwaka
jana, wakala umeweza kukamata watoroshaji wa madini ya aina mbalimbali
katika matukio 27 tofauti.”
Kamishna wa madini nchini, Paul Masanja anasema
mipango ya Serikali na wadau kwa sasa ni kuhakikisha Tanzania hasa
Arusha inakuwa kitovu cha biashara ya madini ya vito barani Afrika.
“Madini ya vito tuliyonayo nchini, hayapatikani
katika mataifa mengi Afrika hivyo tunataka kulifanya Jiji la Arusha kuwa
kitovu cha biashara ya madini ya vito barani Afrika,” anasema.
Anasema kituo cha kisasa cha kukata na kuuza
madini, kikikamilika wafanyabiashara wakubwa duniani wa madini ya vito
watakuja nchini kununua madini.
Hata hivyo, anatoa wito kwa wachimbaji na wanunuzi
wa madini ya Tanzanite nchini, kuacha tabia ya utoroshaji wa madini
hayo nje na kuuza madini hayo yakiwa ghafi.
Wadau wanasemaje?
Mwenyekiti wa chama cha wachimbaji wa madini Mkoa
wa Manyara, Sadiki Mnenei, Wakurugenzi wa kampuni ya Tanzanite One,
Faisal Juma Shabhai na Hussein Gonga na Ofisa wa Kampuni ya Kuuza Madini
ya Crown Lapidary Limited, Lucas Mdemu wanasema kituo hicho kikijengwa
ni faraja na mkombozi kwa wachimbaji na wafanyabiashara hiyo.
Mnenei anasema kwa miaka mingi wachimbaji wadogo
wa madini ya vito wamekuwa hawana masoko ya ndani ya uhakika ili wauze
madini yao. “Wachimbaji wamekuwa wakipeleka madini yao nchi
Ulaya, Marekani, India na Kenya na baadhi yao wamekuwa wakitapeliwa na
wanunuzi sasa kituo cha kimataifa kikiwa Arusha ni ukombozi kwao na
hawatakuwa na sababu ya kupeleka madini nje ya nchi kwani wanunuzi
watakuja Arusha,” anasema.
Shabhai anasema kituo kitawafanya wafanyabiashara ya madini nchini
kumiliki biashara hiyo kimataifa. Mdemu anasema, biashara ya Tanzanite
itakuwa bora kama, wanunuzi wa madini hayo watanunua sehemu ambazo
zinatambulika kisheria. Serikali kuja na mpango wa kujenga kituo hiki ni
ukombozi wa wafanyabiashara, wataokoa mapato yanayopotea na nchi
itafaidika na rasilimali zake.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment