Profesa Abdallah Safari
WASIFU
Umri: Miaka 64
Elimu: Shahada ya Uzamivu (PhD) katika Sheria, Chuo Kikuu cha Sussex, Uingereza.
Kazi: Wakili wa Kujitegemea na Makamu Mwenyekiti wa Chadema (Bara).
Historia yake
Profesa Abdallah Safari ni Makamu Mwenyekiti wa
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na wakili wa kujitegemea
Tanzania. Alizaliwa Juni 3, 1951, katika Kata ya Ngamiani, Tanga
(anatimiza miaka 64 Juni).
Baba yake mzazi alikuwa mfanyakazi na mwendeshaji
wa mashine kubwa za kazi viwandani na barabarani katika Shamba la Mkonge
Mwera. Kwa ujumla, Safari amekulia Mwera japokuwa asili yake ni
Nyanguge, Mwanza (Baba yake mzazi ni Msukuma kwa asili). Safari alianza
elimu katika Shule ya Msingi Pangani mwaka 1958 – 1966 na kuhitimu
darasa la nane, mwaka 1966 – 1967 akaendelea na elimu ya kidato cha
kwanza na cha pili katika Shule ya Sekondari Lushoto (siku hizi ni Chuo
Kikuu cha Sebastian Kolowa) kisha akahamia shule ya sekondari Karimjee
(sasa hivi inaitwa Shule ya Sekondari Usagara) ambako alihitimu kidato
cha nne mwaka 1972.
Safari amesoma kidato cha tano na sita akiwa
mtahiniwa binafsi (private candidate) na akapata cheti cha kuhitimu
masomo ya juu ya sekondari mwaka 1972 katika Shule ya Sekondari Azania
kisha akajiunga Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), baada ya miaka
michache akisomea sheria na kuhitimu shahada hiyo mwaka 1979.
Profesa Safari alifanya Shahada ya Uzamili ya
Sheria hapohapo UDSM na kuhitimu mwaka 1985 na mwaka 1987 akafuzu na
kusajiliwa kuwa Wakili wa Mahakama Kuu ya Tanzania kabla ya kuendelea na
masomo ya juu kabisa kwa maana ya Shahada ya Uzamivu aliyosomea katika
Chuo Kikuu cha Sussex Uingereza na kuhitimu mwana 1995.
Safari ana historia ndefu ya kufanya kazi nchini.
Mwaka 1972 – 1975 alifanya kazi UDSM katika
Taasisi ya Utafiti wa Kiswahili akiwa mtafiti msaidizi, mwaka 1974 –
1976 alifanya kazi katika Shirika la Uchapishaji Tanzania akiwa mhariri,
mwaka 1979 – 1986 alifanya kazi katika Wizara ya Sheria akiwa wakili wa
Serikali, mwaka 1987 aliajiriwa na Chuo cha Diplomasia (Centre for
Foreign Relations – CFR) akiwa ofisa wa uchapishaji na utafiti, mwaka
1988 – 1991 baadaye akapanda na kuwa mhadhiri wa sheria na mwaka 1991 –
1995 kisha mhadhiri mwandamizi.
Kuanzia mwaka 1996 hadi 2001, Safari alipanda na
kuwa Mkurugenzi wa Masomo na Programu chuoni hapo na mwaka 2000 alipanda
ngazi kitaaluma na kuwa Profesa Mshiriki wa Sheria katika kituo
hichohicho.
Lakini pia, Profesa Safari amewahi kushika
nyadhifa nyingine ambazo hazikuwa ajira ya moja kwa moja. Kwa mfano,
mwaka 1978 – 1979 alikuwa Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria wa Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam, mwaka 1983 – 1986 aliongoza kitengo cha mafunzo
kwa vitendo ya wanasheria katika Wizara ya Sheria, mwaka 1996 – 2000
alikuwa Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Vitabu Tanzania (Uwavita),
mwaka 1999 – 2000 akawa Katibu Mkuu wa Kituo cha Usuluhishi wa Migogoro
cha Tanzania.
Msomi huyu ameandika vitabu zaidi ya saba vya
kisheria na vingine vinaendelea kuchapishwa, huku pia akiwa mdau mkubwa
wa lugha ya Kiswahili akiwa ameandika riwaya na vitabu vya kawaida kwa
lugha za Kiingereza na Kiswahili na vingi vinauzwa madukani. Ameoa na
ana watoto wawili.
Mbio za ubunge
Profesa Safari hakuwahi kuombea ubunge au kuwa
mbunge. Amekuwa mpenzi wa siasa, mfuatiliaji na mwenye kiu kubwa ya
kushiriki katika masuala ya kisiasa moja kwa moja tangu alipokuwa UDSM.
Mbio za urais
Nguvu yake
Akiwa Mlimani, ndiye aliyekuwa mhariri wa kijarida cha
kimapinduzi kilichokuwa kikitolewa hapo kikiwa na picha ya mwenge na
kilitokea kupendwa sana. Ameniambia kwamba huo ndiyo wakati ambao
alizidi kuipenda siasa, japokuwa aliwahi kuvutiwa na baba yake ambaye
alikuwa anashiriki katika harakati za kisiasa.
Alipotoka Uingereza kwa masomo ya shahada ya
uzamivu, alikuta joto la mabadiliko limepamba moto Tanzania. Kwa sababu
alikuwa anafahamiana vizuri na Profesa Ibrahim Lipumba, aliamua kujiunga
na Chama cha Wananchi (CUF), amenisisitiza kuwa hakufuatwa wala
kuombwa, aliamua mwenyewe. Tangu wakati huo alikuwa mshauri wa viongozi
wa chama akisaidia masuala muhimu ya kisheria.
Mwaka 2009 aliamua kujitosa kwenye kinyang’anyiro
cha kugombea uenyekiti wa CUF akipambana na Profesa Lipumba lakini
hakufanikiwa kuchaguliwa. Baadaye alisikika akisema kuwa hakutendewa
haki katika uchaguzi huo, akaamua kujiondoa na miaka miwili baadaye
akahamia Chadema na kuwa mjumbe wa Kamati Kuu kabla ya kugombea umakamu
mwenyekiti wa chama hicho (Bara), mwaka jana na kushinda.
Mbio za urais
Profesa Safari hajatangaza rasmi kuwa atagombea
urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lakini ni mmoja wa viongozi wa
Chadema wanaotajwa kuwa wana sifa, uwezo na vigezo vya kwenda Ikulu na
wakaipeleka nchi mbele. Kwa sababu lengo la safu hii ni kuwachambua wale
wote waliotangaza kugombea urais na wale wanaotajwa, ndiyo maana na
yeye yumo.
Nilipomuuliza ikiwa maoni hayo ya wana Chadema
anaweza kuyafanyia kazi alisisitiza kuwa muda ukifika tutajua, maana
chama chake kina taratibu za kufuata.
Nguvu yake
Kwanza, Profesa Safari ni mwanasheria na msomi
aliyebobea kwa kiwango cha juu. Ni moja ya hazina kubwa za utaalamu wa
sheria hapa Tanzania. Nakumbuka tulipokuwa naye kwenye Bunge Maalumu la
Katiba na tukiwa kwenye vikao vya pembeni, yeye peke yake ndiye
aliyekuwa na uwezo mzuri wa kunyoosha hoja za Tundu Lissu ambaye
mwanasheria mzuri. Profesa Safari ni mbobezi wa hali ya juu, anaweza
kukueleza masuala ya sheria na ukayaelewa kwa lugha rahisi na huenda kwa
uwezo huo wa kisheria, anaweza pia kuutumia katika kujenga uongozi
imara wa nchi.
Jambo la pili ambalo ni sifa na nguvu ya Profesa
Safari ni utulivu na busara za hali ya juu. Moja ya sifa kubwa ya
kiongozi wa nchi ni kutokurupuka katika kutoka uamuzi. Huyu si mtu wa
kukurupuka, anafanya kila jambo kwa wakati na kwa utulivu mkubwa.
Mathalan, alipojiondoa CUF mwaka 2009 alikaa chini kwa takriban miaka
miwili kabla ya kujiunga na Chadema. Wanasiasa wengi hudhani kuwa siasa
ni biashara, mtu akihama chama hiki leo, kesho amejiunga chama kingine
kama biashara ya karanga. Baadhi ya wahadhiri niliozungumza nao pale
Chuo cha Diplomasia, wameniambia kuwa wao pia wanamfahamu hivyo. Hili ni
jambo muhimu kwa rais yeyote anayetaka kuifikisha mbali nchi yake.
Lakini jambo la tatu ambalo ni muhimu pia, Profesa
Safari anapenda na kuthamini sanaa na utamaduni wa mtu mweusi na ni
moja ya masuala ambayo ametumia muda wake mwingi kuyakuza. Licha ya kuwa
ni msomi wa sheria kwa ngazi ya uzamivu, ni mwandishi wa vitabu vya
kawaida vya Kiswahili, kamusi na miswada mbalimbali yenye lengo la
kukuza na kuimarisha lugha hiyo, kama alama muhimu ya Taifa. Mara nyingi
amekuwa pia akifanya vipindi vya televisheni na redio kuelimisha
wananchi juu ya umuhimu wa kuendelea kukuza na kukitumia Kiswahili.
Binafsi namuona kama mwanasheria na mwanazuoni anayekipigania Kiswahili
kuliko hata baadhi ya wabobezi wa lugha hiyo wenye shahada za uzamivu.
Kwa sababu Taifa letu limeshaondoka katika misingi ya kujali utu, udugu,
utamaduni na hadhi ya Mwafrika, huenda watu wenye mtizamo kama wake
wanaweza kuwa sahihi kwa Tanzania tuitafutayo.
Mwisho, msomi huyu ni mpiganaji na mpambanaji
ambaye anathubutu kwa kadri awezavyo. Mathalan, akiwa mwajiriwa wa Chuo
cha Diplomasia kinachomilikiwa na Serikali, alimtetea Profesa Lipumba
katika kesi ya uchochezi ya mwaka 2001 ambayo ilitokana na mauaji ya
Zanzibar ya Januari 2001. Amenieleza kuwa kitendo kile kilisababisha
kufukuzwa kazi mwaka huohuo.
Nilipomuuliza kama hakujua kuwa kitendo kile
kingetafsiriwa hivyo na Serikali, alinijulisha kuwa utetezi wa mtu
anayeonewa katika hali ngumu kama ile haukuwa unakwepeka na kwamba hata
leo haukwepeki. Uthubutu huu wa Profesa Safari, kuwa tayari kupoteza
kazi ili kulinda na kuimarisha demokrasia ndani ya nchi unamfanya awe
mmoja wa viongozi wa kupigiwa mfano na labda wanaohitajika kuongoza
nchi.
Udhaifu wake
Nini kinaweza kumfanya apitishwe?
Nini kinaweza kumwangusha?
Udhaifu wake
Moja ya jambo ninalolitizama kama udhaifu wa
Profesa Safari ni kuwa na misimamo mikali katika baadhi ya masuala ya
kisiasa anayoyaamini. Tunatambua kuwa kiongozi wa nchi anapaswa kuwa na
misimamo imara na inayoeleweka, lakini misimamo hiyo inapokuwa michungu
inageuka na kuanza kuwa na madhara.
Kwa mfano, kutokana na kukosekana kwa tume huru ya
uchaguzi na mizengwe ambayo chama kinachoongoza dola kimekuwa
kikiitenda dhidi ya vyama vya upinzani, Profesa Safari aliwahi
kukaririwa akivieleza vyombo vya habari kuwa msimamo wake ni vyama vya
upinzani kutoshiriki uchaguzi mkuu wa mwaka 2010. Safari aliwahi tena
kuhojiwa kwenye kipindi kimoja cha televisheni na akasisitiza kuwa vyama
vya upinzani visiishie kulalamika kwa maneno, vinapaswa kususia
uchaguzi ili CCM wachaguane wao wenyewe.
Msimamo ule wa Profesa Safari ulinishangaza kwa
sababu anajua historia ya Afrika, kwamba kufanya hivyo hapa Afrika ni
kuwaneemesha watawala na kuwabinya wananchi wa kawaida. Lakini pia watu
niliozungumza nao na waliowahi kufanya naye kazi UDSM, Diplomasia na
hata Chadema wanasisitiza sifa hii kwa Profesa Safari, sijui kama leo
hii akiulizwa tena kuhusu hali ile anaweza kudai vyama vya upinzani
visuse uchaguzi.
Lakini udhaifu wa pili wa Profesa Safari ni
kutopenda kufahamika. Wakati mwingine sifa kubwa ya mwanasiasa ni
kufahamika kwa watu wanaomzunguka. Yeye si mtu wa kupenda malumbano na
mapambano ya maneno kama wanavyoweza kufanya wanasiasa wengi duniani na
nadhani hapendi kushambuliwa kwa mambo ambayo anadhani anayajua vizuri.
Kwa siasa za Afrika, mwanasiasa imara lazima awe tayari kwa malumbano
mazito yanayokaribia hata kushikanisha miili. Aina ya tabia ya kuhitaji
siasa ziwe safi na kuzishiriki zikiwa safi, ni jambo ambalo halipo
Afrika na kwa hiyo kutokuthubutu kuzifanya kwa nguvu kila inapohitajika
na utaratibu kila unapohitajika utaratibu, ni udhaifu wa kutosha.
Nini kinaweza kumfanya apitishwe?
Moja ya mambo yanayoweza kumfanya apitishwe
kuwania urais kupitia Chadema na hata Ukawa ni ikiwa chama hicho ndicho
kitaachiwa jukumu la kutoa mgombea urais. Naamini kabisa, yeye ni mmoja
wa wana Chadema wachache wenye sifa na uwezo wa kuongoza nchi ikiwa
atapewa nafasi hiyo.
Pili, kwa sababu Profesa Safari amefanya kazi
Diplomasia kwa miaka mingi amekuwa na uzoefu mkubwa wa kushughulikia
masuala ya kimataifa, kwa muktadha huo ana sifa za ziada za kupewa fursa
hiyo na Chadema na baadaye Ukawa.
Tatu, yeye ni mmoja wa Watanzania wanaoifahamu
vizuri historia ya nchi yetu, amefanya tafiti nyingi kuhusu maendeleo na
utamaduni wa nchi katika mikoa mbalimbali na kufanya kazi serikalini
kwa muda mrefu. Kwa hivyo nadhani anaifahamu Serikali na namna
inavyofanya kazi, lakini pia anawafahamu wafanyakazi na wananchi wa
kawaida kiasi cha kutosha kujua nini kiini cha shida na umaskini wao.
Nini kinaweza kumwangusha?
Jambo la kwanza ambalo litamuondoa Profesa Safari
katika mtanange wa kusaka urais wa Tanzania ni ikiwa Katibu Mkuu wa
chama hicho, Dk Willibrod Slaa atapewa jukumu la kupeperusha bendera ya
Ukawa kupitia Chadema. Kwa sababu ndani ya vyama huwa kuna taratibu
zake. Huenda akajikuta anampisha kwa utaratibu huo.
Jambo jingine linaloweza kumuengua ni ikiwa Ukawa
itakubaliana kusimamisha mgombea urais kutoka vyama vya NLD, CUF au
NCCR. Hili nalo lina maana kuwa Profesa Safari atalazimika kumuunga
mkono mgombea wa moja ya vyama hivyo.
Asipochaguliwa (Mpango B)
Hitimisho
Jambo la tatu ambalo naliona nadra kutokea ni ikiwa Ukawa itapa
mgombea kutoka Zanzibar, hili nalo linamhukumu Profesa Safari kwani ni
Mbara.
Ndiyo kusema kuwa, kama mambo hayo matatu
hayatatokea basi Profesa Safari anaweza kuwa na fursa kubwa ya kutumwa
na Ukawa kusaka kura na hatimaye kuwa Rais wa Tanzania ikiwa umoja huo
utapewa ridhaa hiyo.
Asipochaguliwa (Mpango B)
Anaweza kuwa na mambo matatu ikiwa hatapita kwenye mchujo wa Ukawa kuwania urais wa Tanzania.
Mpango wa kwanza utakuwa ni kuendelea na shughuli
za uwakili kwa kesi za vyama vya Ukawa na nyingine za wananchi kwa
ujumla. Tukumbuke kuwa Profesa Safari ni mmoja wa mawakili wazoefu na
waliwahi kusimamia kesi kubwa zilizotikisa vyombo vya habari, ikiwamo
ile ya kiongozi wa Chadema Jimbo la Kinondoni, Henry Kilewo ya ugaidi
kule mkoani Tabora. Akijikita huku, ataendelea kutoa mchango mkubwa
kwenye ukuaji wa demokrasia.
Lakini pia anaweza kuendeleza kwa nguvu juhudi za
uandishi wa vitabu. Tayari ameshaandika vitabu kadhaa vya sheria na vya
taaluma zisizo za sheria ikiwamo vya lugha. Kutogombea urais na labda
kutoingia Ikulu kutampa fursa hii adhimu.
Mwisho, Profesa Safari ni msomi mwenye mchango
ambao bado unahitajika. Kama hataingia kwenye urais, ana fursa ya
kipekee kujipanga kushiriki uchaguzi katika ngazi ya jimbo, akitafuta
tiketi ya kuwa mbunge na kuwawakilisha wananchi, kazi ambayo inaweza
kumpeleka mbali kisiasa.
Hitimisho
Namtazama Profesa Safari kuwa ni Mtanzania
anayependa zaidi kushiriki katika harakati za kidemokrasia na kushauri
namna bora ya kuzifanya kuliko kuwa mstari wa mbele akiongoza.
Tulipokuwa Bunge Maalumu la Katiba, hata kama viongozi kadhaa wa vyama
visivyoongoza dola hawakuwapo, yeye hakuchukua jukumu la kuongoza
mijadala na vikao, badala yake alikuwa anapenda kupendekeza vijana
wafanye kazi hiyo huku akiwa msikilizaji na mshauri
Namtakia Profesa Safari kila la heri katika
kukamilisha mipango muhimu ya kidemokrasia katika uchaguzi wa mwaka huu
na chaguzi zijazo.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment